Saturday, February 4, 2012

NAWEKA MOJA CHEMBA.


Chokoraa wa Muhangaikaji wa Kabwela wa Mlalahoi nilipoamua kuwa natembea nimeshikilia "manati ya ndhungu", kuna waliodhani sasa nimeanza kuingia kwenye kutafuta shekeli kwa matumizi ya mabavu, humu nakataa simo. Simo kwa sababu matumizi ya mabavu kwa kutumia hii manati ni hatua nisiyoitaka kabisa, lakini leo nimekuja kijijini hapa kutangaza rasmi kwamba naweka moja chemba. Ndiyo, naweka moja chemba kwa sababu naona sasa ama kuna watu kwa maskudi kabsaaa wanamchezea kichwa mkulu wa kaya na kwa hivyo wanatuchezea vichwa wanakaya wote ama mkulu wa kaya mwenyewe hajali matatizo ya wadanganyika walipa kodi wake na humu naapa sihusiki. Ala! Hivi mwataka ati niendelee kuelekeza mtutu wa hii manati chini ilhali "waishiwa" wanyonya damu ya wadanganyika (mbu) na watema sumu hatari (nge) wamekutana kwa karibu siku saba sasa na hawataki kuzungumzia hali ya afya ya vitegemezi vyangu ilhali wao ndiyo walikuwa tegemeo langu la mwisho kwenye ulimwengu huu wa kupiga domo class 'A'. Nakataa simo. Hivi mnachotaka kuniambia Chokoraa miye mwana wa Kabwela ni kwamba ile timu nzima ya 'ivitaki' pale kwenye "chikale" haijui kwamba wadanganyika tumekuwa kwa juma zima tukimsubiria mkulu wa kaya aseme kitu kuhusu hawa akina "kalumanzila" wa kaya yetu waliogoma kuzama porini kuchimba mizizi na kutoa michemsho kwa matumbo ya watoto!!?. Ati anakuja na nyie mwampeleka moja kwa nne kwenye kufungua majumba ya hela!? Hela gani mtaweka humo ikiwa wadanganyika nguvu kazi ya kaya yetu wanakufa kwa vile hakuna "mshana" unaotolewa huko kilingeni?? Nitoeni humu. Simo, tena simo, simo, simo kabisaaaaaaaaaaaaa. 
Naapa mwaka huu mtakiona cha moto wadanganyika walipa kodi nyie maana mmekuwa nyasi kwenye uwanda wa mapambano ya mafahali wa Nyati na Faru na humu simo.  Bhaaaa!! Yaani ati kwa vile ninyi mwatibiwa nje ya mipaka ya kaya yetu hii mkituacha wadanganyika tukitaabika, basi mwatuona pia hatuna akili wala uwezo wa kupambanua mambo! Ama kweli ukitaka kumuua mbwa ua kwanza pua zake, nanyi mmeshindwa kunusa harufu ya hasira na chuki za wadanganyika na kwa hili simo.
Nasema, wadanganyeni wengine wooote lakini si mimi mwana wa Muhangaikaji maana mimi ninayo macho, tena makubwa kama ya bundi naona vyema usiku kuliko mchana na hivyo hamnidanganyi enyi mchekao nasi mchana ilhali usiku mwatuua gizani na kuhudhuria mazishi mchana mkivalia sura za uongo na kweli muonekane wahuzunika nasi, nasema simo. 

Ha ha ha ha ha, nacheka miye kitukuu wa Kabwela kwa sababu nawajua ninyi hata kutokea mbali maana macho yangu ya ndani yanaona hata mjapo ninyima kuona kwa macho ya nje  mtendapo mtendayo  kwa siri na hila, lakini nikiuona mwisho, naujua mwanzo wake na kwa hili nasema mnitoe!.  Ala! Kwani si ni nyie wenyewe wana wa ‘ifitaki’ mliokuwa hapo mwanzo mkimweka mkulu wa kaya mbele ya luninga zetu huku mkimfanya kuongelea mambo ambayo yalipaswa kuongelewa na liwali wala si mkulu wa kaya na kutufanya wenye akili kushangaa kwa nini mwamvunjia heshima namna hii!!? Yuko wapi sasa kuzungumzia madhira yenye kuwagusa wadanganyika, madhira ambayo neno lake tu, roho za wadanganyika arobaini milioni na ushee zingepona, nasema kwa hili mimi nakuwa wa kwanza kusema “Amina”. 

Ndiyo nasema amina maana musa alitangulia kuwajua enyi wana na akaandika akigiaza walaaniwe wampotezao mgeni njia na watu wote waseme amina na mimi kwenye hili ni wa kwanza “Amina”.

Najua mtasema nabwabwaja mambo nisiyoyajua lakini haya ninayoyajua ninayajua na ninayasema kwa usahihi ili mwenye masikio asikie, mmempoteza njia aliyepaswa kuongoza njia na humu simo. Nasema simo kwa vile wote twasafiri na tuendako wote twapajua, basi kelele na manung’uniko haya sit u ni mazao ya ‘ domo ghasia’ kama msemavyo ili msadikiwe na wazandiki wenye kuwapa vipande vya chupa ilhali wakiondoka na almasi yenu, bali ni hisia za wazi kwamba wadanganyika waliokuwa siku zote wakijua kwamba ni wadanganyika na kujivunia kudanganyika, sasa wamechoka na wanataka uhakika na kwenye hili nasema mnitoe.

Mnitoe, tena simo kabisa. Naam, kwa sababu najua mnajua ya kwamba hamna majibu ya maswali yaulizwayo na sasa mnataka tunyamaze tusiulize si kwa vile tunauliza upuuzi bali kwa vile hamkujua kwamba wakati unakuja tutawauliza kwa habari ya talanta ya “kula” mlizopewa na wenye kukasirika na kupiga ‘kura’ ili wapate kula kuambulia kuliwa, humu namo simo.
Ala! Hivi nyie ndugu wawili wa mdanyika yaani Mbu na Nge mmeanza lini tabia hii!!? Ha ha ha ha ha ha ha ha, nacheka miye maana najua wadanganyika walidanganyika walipodhani kwamba wakiwaweka ninyi pamoja yaani mbu kwa sababu ya sauti yako nzuri ya kubembeleza huku ukinyonya damu na kuwacha virusi, basi ungenyonya kwa wanyonyaji na kuacha virusi kwao ili ulete faida kwa wadanganyika, sasa najua kwamba walidanganyika, na ninaapa simo. Walidanyika walipodhani Mbu na Nge wakiwekwa pamoja wataleta uwezo wao wa kunyonya damu na kutema sumu hili kuleta nafuu kwa niaba ya wadanganyika walipa kodi kumbe hawakujua kwamba kwenye kijiji cha waishiwa kuna kaugonjwa ka ‘metamofisisi’ kanakowabadili wadanganyika wanaoingia kijijini humo kuwa ‘waishiwa’ na kusahau udanganyika wao na humu nakataa kuwamo. 

Wacha nicheke miye maana najua sasa wakati u karibu. Ndiyo, wakati wa Chokoraa kuambiwa anyamaze na asiseme anayosema na kama bado anataka kusema basi aseme watakayosema wale wenye mamluki na si mamlaka ya kusema na humu nasema sitakuwamo maana simo.  Nasema wakati wanaosema sasa watakapotakiwa kunyamaza na walionyama kutakiwa kusema, wanaodanganyika sasa watakapotakiwa kuambiwa ukweli na wakweli kudanganywa, wakati huo mjomba shangazi na binamu hawatafanya tena maamuzi kwenye jumba kuu la mashauri na hapo walau hadhi na heshima ya mdanganyika itarejea, lakini kwa vile njia ni ndefu yenye kugharimu machozi jasho na damu, Chokoraa najitoa, simo, tena simo kabisaaaaaaa!!

Salaam, ni mimi nduguyo wa damu, Chokoraa wa Muhangaikaji wa Mlalahoi wa Pangu pakavu wa Kabwela wa Mdangayika, nakusalimia.