Tuesday, May 1, 2012

Ama kweli hamna adabu enyi wana.


Najua! Najua umekuwa muda sasa tangu nimepitia kijiweni hapa walau kukusalimia na si kwamba nilikusahau, ila nilikuwa kwenye ule mchezo wa sasa ambao kila mtu ni lazima acheze tangu mdogo hata mkubwa, maskini ama tajiri, msomi kama wewe ama mbumbumbu kama Chokoraa, nao ni mchezo wa kuwa “bize’. Naapa simo. Si kwamba simo kwenye mchezo wenyewe, isipokuwa kwa vile wako ambao wako ‘bize’ kila siku na wapata chochote kitu ilhali wengine wako ‘bize’ waambulia umaarufu wa harufu, humu namo simo. 

Ha ha ha ha ha ha!! Nicheke miye Chokoraa wa Muhangaikaji wa Mlalahoi wa Pangu pakavu wa Kabwela wa Mdanganyika si kana kwamba nina furaha, lakini nani kasema hii “gunia” yetu ni kama ile ya babu yangu Pangu pakavu ambapo walioweza kupata habari, wachilia mbali walioweza kutoa habari walikuwa wachache sana na wenye daraja fulani katika jamii!!? Washangaa nini! Nakumbuka miaka hiyo kulikuwa na vyombo vichache sana vya habari na vyote vilikuwa kwenye ‘siri kali’ vikitumiwa tu na ‘watwawala’ kuwapelekea amri ‘watwaliwa’ na hata sheria ikaweka kwamba ili iwe sheria ni lazima kwanza itangazwe kwenye gazeti la ‘siri kali’. Ha ha ha ha ha ha!!! Leo watu wasema na sisi kupitia ‘ubunifu wa Buibui’ na mwana wa Muhangaikaji nasikika kupitia kamchezo hako ka mdudu Buibui na bado wataka ati nisicheke! Simo humu.   

Haya, wacha basi nikupe pole kwa msiba maana siku hizi kwa ajiri ya wadanganyika woote kuhama mitaani na vijijini kwao wakishinda “bize” na kurudi jioni ama usiku mwingi, basi utamaduni wetu umebadilika na hata misiba haihudhuriwi kama ilivyokuwa zama na ndiyo maana hata Chokoraa sikuwa nimepata nafasi ya kukupa pole ya misiba. He! Ona huyu ati hajui kwamba kwenye ‘inji’ hii tumepata misiba mikubwa kadhaa na ya kitaifa kwa sababu ati naye alikuwa ‘bize’ kiasi cha kushindwa kusoma ‘udaku’ na kutazama kasanduku ka picha ama kusikiliza ile radio ya mwenyekigoda wa kijiji chao, hata alipoingia kwenye makaazi ya Buibui yaani ‘mtandaoni’ hakupata nafasi ya kusoma ‘niuzi’ zaidi ya kupata ‘esi emu esi’ kadhaa kwa BBM na kuishia kulala ili adamke mapema na kukimbilia ‘bize’, naapa utamaduni wa binadamu unafirisika kila kukicha na humu simo. 

Nasema mnitoe kwenye huu mufirisi wa ustaarabu wenu enyi wadanganyika maana mtu asite utamaduni ni mfungwa wa kifungo cha nyumbani walau hivyo ndivyo nijuavyo Chokoraa wa Muhangaikaji wa Mlalahoi na kwa hili naapa tutashindana sana lakini simo. Hivi si ulikuwa utamaduni wenu enyi wadanganyika wa kuheshimu watangulizi wenu iwe ni wazazi nyumbani ama viongozi kwenye hizo ‘siri’ zenu ‘kali ‘ na hata mlikuwa na ‘proto kali’ ya kutokunywa kahawa kama mwenyekigoda hajafika? Nasema huo unaoonekana kama upuuzi kwenu ninyi masharo wa sasa ndiyo ulikuwa misingi ya uzalendo wa watu wa  inji hii na hata kujitolea kufa kwa ajiri ya ‘udanganyika’ wao kwa sababu walau walijua ‘legasi’ yao ingebaki. Sasa naapa kila mmoja anataka kuwa “msanii” na nimtumie pole ‘mzee wa ukweli usio wazi’ kwa juhudi zake za kutaka ati kuifanya ‘danganyika’ yake isiitwe tena ‘bongo’ kwa vile ati ‘usanii’ ulizidi. Nani anataka kuwa ‘hiro ov ze nesheni’ (naonyesha msisitizo) kwa kutumikia inji hii ilhali anaweza kuacha ‘ligasi’ kwa watoto wake kwa kuwa muuza sura luningani nasema mnitoe. Ati wakulu wote wa kaya wakajikusanya na kujirundika kwenye msiba wa ‘msanii’ na kuishushia heshima ya ‘kiifitaki’ misiba ya mashujaa wa inji hii hadi wale walioliongoza ‘geshi la waheshiwa tangu zamani’ naapa humu simo. Nasema kwa hili Chokoraa nitasema na kurudia kwamba adabu si shikamoo na uungwana ni vitendo, kizazi hiki kimekosa adabu kwa watangulizi wake na namuomba jalali awajaalie mzeeke ili muone jinsi inavyoumiza kwa kizazi kinachofuata baada yenu ‘kuikanya legasi’ yenu chini ya nyao za miguu, siyo nawalaani nawaombea maisha mema na ya neema ila kwenye hili la dharau mimi simo, tena simo kabisaaa. 

Nasema kama mgekubali kuwa wanafunzi mgejifunza maana waalimu wako wengi waliotenda vyema kabla yenu ili muone na kujifunza kwao lakini nani kasema adabu inauzwa ama hukwanguliwa kama vocha!? Naapa simo. Ala! Kwani wakati ‘mzee wa kuruhusu’ alipoamua ‘kushtuka’ (naogopa kusema kizanaki msijesema natumia vibaya lugha ya taifa) na kujiweka pembeni ‘kuepusha msongamano’ ilimnyima nini kuwa ‘mkulu wa kaya’ wakati ulipowadia!? Au ni kwa sababu ninyi sasa mmeendela sana na mnaamini “riziki kama ipo ichukue kama haipo ilazimishe” na hivyo mwaona kung’atuka ni aibu?. 

Labda ni kweli kwamba hamna heshima kwa ‘wazee’ wenu tena enyi wana wa danganyika maana nani hakusikia wakati mlipowatazama usoni wazee wenu na kuwahoji sababu ya wao kutotumia hayo mawazo mazuri wanayokupeni kipindi cha ‘wakati wao’ mkisahau kwamba wakati ukuta?. Naapa mna zaidi ya kiburi enyi wana. Nasema kama ilivyokwisha kusemwa kwamba sokoni hupatikana vyote yaani chakula na uchafu na cha pili si aghali kupatikana kwake japo matumizi yake ni adimu na ninyi mmejifunza kwa watangulizi wenu lakini kama waenda sokoni mmechukua uchafu mkaacha chakula ashakumu si matusi, humu simo. Ala! Kwani si mmeamua kwa makusudi kujifunza kwa wale waliojitokeza hadharani mbele ya visanduku vyetu vya picha, tena tunavyoviwasha kwa umeme tunaoulipia sisi wakitwambia wala si kutuomba kwamba tugeuke mbuzi na ng’ombe tule nyasi lakini wao wanunue “mwewe” kwa ajiri ya ‘mkulu wa kaya?”. Nasema mmejifunza kwa hao na mmefaulu na humu mimi nakataa kuhusika, simo tena simo kabisa.
Ni hivi juzi tu, mlikulana na kuparurana makucha huko kwenye jumba la maamuzi na kutaka hata kuvuana nguo na wala hii si mara ya kwanza ama ya pili walau kwa siku za karibuni, lakini tofauti na mwanzo wakati watu walipojipachika majina kama “Bangusiro’ na mengineyo, ninyi mmekataa kuwa ‘mbuzi wa sadaka’ na badala yake mmekuwa ‘ngangari’ kwenye kuendeleza ‘yale yote ambayo kwa moyo na nia thabiti mmekuwa mkiitendea inji hii’ na kwa hili nakupongezeni ila mi mnitoe maana simo. Naam, mioyo na nia zenu ni thabiti katika kutenda lakini mnatenda kama waenda sokoni maana pana faida gani kuendelea kuonyesha njia mbele ya mtu ambaye hayuko tayari kukufuata?  Naapa nilidanganyika. Ndiyo, ni uzembe wangu kwamba nilidanganywa nikadanganyika kwamba kiongozi wa domo daraja la kwanza ama domo class A huzingatia misingi ya ‘domo class A’ yaani utawala wa watu kupitia watu kwa ajiri ya watu, kumbe sivyo na humu simo tena simo kabisa. Nakataa kuwamo kwa sababu kama watu (kupitia mawakala wao) wamekataa kwamba fulani na fulani hatutaki muendelee kutangulia huko mbele, si adabu basi kwamba mjitenge na kuwaacha watu wachague watu wengine wa kuongoza njia ya watu kwa ajiri ya watu ama ninyi mnayo tafsiri nyingine ya ‘domo krasi ei’? 

Sitaki kuongea sana wacha haya machache yatoshe kwa leo na niwape pole wadanganyika walipa kodi kwa misiba mikubwa ya kitaifa iliyowakuteni ikiwamo kuondokewa na wazee wetu, waliojitolea kufa na kupona, waliorudisha fedha za serikali kwa sababu waliamini kwamba wamelipwa zaidi ya walivyotumia na hatuwezi kwa na mfano bora zaidi wa uwajibikaji na uzalendo kama huu. Nasema jifunzeni kwa hawa kama bado mmebakiza sehemu ya kuingiza mafunzo mapya kwenye fahamu zenu lakini ikiwa tayari mmekwishakuwa mbwa wazee wasiofunzwa mbinu mpya, sina jingine la kuwaambieni isipokuwa kuwasalimiwa.
Wasalaaam, ni mimi ndugu yenu Chokoraa wa Muhangaikaji wa Mlalahoi wa Pangu pakavu wa Kabwela wa Mdanganyika, nawasalimia.