Thursday, May 23, 2013

Kaka Mkulu wa Kaya, Salaam Nakusalimia.



Kaka  Mkulu wa Kaya, salaam nakusalimia,
Nasema kuwa huru si rahisi kama ilivyo si rahisi kuwa rais na sasa Chokoraa nawasalimia. Kubadili majalala huku kuna siku nitaingia kwenye jalala la tindikali naapa kwa jina la bibi yangu mzaa mama yangu Shida wa Matatizo msinihusishe. Nasema msitake niseme kwa mtiririko maana yaliyonijaa kwenye koo ni mengi na njia ya ama kuyameza ama kuyatema ni ndogo na hivyo wacheni niyatapike liwalo na liwe maana ni bora moja kuliko sifuri na humu miye nahusikaje!?. 

Kwani nani kaiona ramani ya kaya yetu, ile ramani halisi ya Danganyika ya Wadanganyika tuliyoachiwa na wazee wetu kabla haijabadilishwa na hawa wenye kujitangazia uhuru kila uchao kisa “uhuru na haki za raia” na mimi nauliza ni nini uhuru na haki za rais na kwa hili mnitoe maana simo. 

Kaka mkulu wa kaya, nimetumwa na wadogo zangu akina Muuza Mayai na Karanga, na hata mama yangu mdogo Mama Ntilie kanituma nikusalimie.  Hawa wawili wanasema wanakumbuka kabla ya kufariki baba wa kaya yetu na kabla ya wewe kuteuliwa na kikao kilichopita cha ukoo kuwa Mkulu wa Kaya na kuongoza kundi la akina kaka Muishiwa wa Maadili na Kiongozi Mbadhilifu katika kuiwakilisha kaya yetu hii, tulikuwa sisi wote ni wamoja watoto wa mzee Mdanganyika Mlipakodi na mama yetu Bi Mzalendo.  

Ati wanasema baada ya kufariki baba yetu, kundi lenu likiongozwa na akina kaka Muishiwa walimpendekeza kaka yenu mkubwa Mtukutu kutuelekeza kule yalikofichwa maisha tarajari ya kaya yetu na ati baada ya siku chache kaka yetu huyu kujitangaza kuwa ‘Mtukufu’ watu wakaogopa lakini kwa vile ati kilikuwa kizazi kilicholelewa vyema na marehemu baba yetu kwa kutohoji yale yafwanywayo na wale wenye kuvaa lile joho lefu la baba na wenzake lenye rangi ya Kiongozi, basi wakakaa kimya. Hata hivyo yale yaliyotendeka ati yalitendeka na hata akina Mlalahoi wakaanza kujenga maghorofa kwa kuuza vitunguu swaumu nisikuchoshe na historia, salaam nakusalimia. 

Baadaye ndipo kijiti alipopewa kaka mkubwa Muishiwa. Wanasema ati huyu naye kwa sehemu alizingatia sehemu ya mafunzo ya marehemu mama yetu Mzalendo binti Mdanganyika ijapokuwa ni kweli kwamba yeye kijiko chake kilikuwa kikubwa maakulini ukizingatia na sisi wengine, lakini walau alijenga daraja na siyo ukuta, nasema nisikuchoshe ila salaam nakusalimia. 

Sasa kuna Yule dada yetu mkubwa ambaye hasa ndiye aliyenifanya nikuandikie waraka huu hasa kwa vile binafsi naweza nisipate nafasi ya kuonana na wewe mwaka huu, si kwa sababu sipendi ama ati kwa vile naogopa wale walinzi wako kama mjomba, lah! Bali kwa vile lile daraja kutoka huku kwetu kuja huko kwenu lina mushkeli kidogo hasa baada ya juzi tu wadanganyika kuchoshwa na kuamua kutenda watendavyo mradi iwe iwavyo, salaam nakusalimia. 

Nasema watu wakichoshwa ni heri ya punda mzee kubeba mzigo yeye na mwana kuliko mtu ama aliyeshiba mema au asiyekula kabisa maana wote huwa na wazimu kwa sababu tofauti na mimi humu sihusiki. 

Dada yetu mkubwa Mjasiriamali ameniagiza nikusalimie na kisha nikueleze kwamba kwake yeye ijapokuwa hapendi hata kidogo jinsi ati unavyotuhumiwa kwa mjomba na shangazi kuwa na sauti nzito kuliko wewe kwenye  kaya yetu, lakini walau alikuwa bado angali na imani na ile “Siri kali” labda kwa vile ilikuwa imefichwa na haikujulikana kwake na hivyo si kwamba aliiamini “Siri kali” bali aliamini kwamba kuna siku na yeye atakuwa sehemu ya wale wenye kuifahamu siri hiyo ifichwayo kwa udi na uvumba na hilo linanifanya salaam nakusalimia. 

Anasema baada ya hivi majuzi watu wasiojulikana kujitangazia mamlaka bila madaraka na kuufunga mji wa Mtwara tena pasina kupata upinzani wowote kutoka kwa walinzi wa “Siri kali”, dada yangu mjasiriamali amejiuliza maswali kadhaa ambayo machache yake amenitaka nikuulize na mimi sasa nakuuliza; Hivi ni kweli kwamba ile “Siri kali” yetu imevuja na sasa kila aliyeko nje anaona ndani kama aliyeko ndaniaonavyo nje!? Nasema usijesema miye sina adabu ninazo tena tele lakini najiuliza inawezekanaje kwamba genge la “wahuni” linafunga mji kiasi Chokoraa wa Muhangaikaji wa Mlalahoi wa Pangupakavu wa Kabwela wa Mdanganyika na hata dada yangu chakaramu Mjasiriamali hatuwezi kutoka ndani na kwenda kuokoteza mkate wa siku? .
Samahani unisamehe, si hoja yangu ya msingi ikiwa ni sahihi kwako kujenga njia ya panya na kupitisha gesi, oil ama mafuta hiyo kwangu si hoja. Nasema yafaa nini mimi kuhoji ikiwa hilo ni sahihi ama si sahihi ikiwa mimi Mdanganyika sina haki wala hadhi ya kuhoji usahihi ama tafsiri ya usahihi wenyewe?.

Kinachonikera mimi na dada yangu Mjasilia ni kwanini na hasa inawezekanaje kwamba ‘watu wasiojulikana’ wanaweza kufunga mji na biashara zake zote na hadi sasa wakawa bado “hawajajulikana”?.   

Ati! Utani wa kuniambia tena ati ni “kundi la wahuni” wanaohatarisha maisha ya wadanganyika wa Ntwara tafadhali tuuacheni maana wahuni hawa sasa wamepevuka mno kutoka daraja la kawaida la uhuni sasa wanaelekea kuwa ‘waahini’ na mimi humo sihusiki. Hivi inawezekanaje kwamba watu ‘wasiojulikana’ ama “wahuni” kama ambavyo baadhi yenu mtataka nisadiki, kwa kutumia ‘vikaratasi’tu  wameufunga mji na biashara zote kusimama?. 

Nasema kwa hili msinihusishe hata kidogo. Haya, ebu niwaze kichokoraa. Hivi wakati ‘tanchi’ la kwanza lilipopigwa, vipeperushi si vilikuwa vimeanza kusambazwa tangu jumatatu na tanchi lilipigwa ijumaa! Nani kasema unahitaji ‘kadigirii’ kujua kwamba hapo katikati kulikuwa na jumla ya siku tatu nzima na jumla ya saa sabini na mbili za kuwasaka na kuwatia ‘mtaroni’ agha! Samahani, kuwatia mbaroni ‘wahuni’ wanaoongoza vitendo hivi!? Hivi siku hizi wale ‘sungusungu’ wako wa kaya nao wamekuwa butu hawana meno kazi yao imebakia kututishia siye vitukuu wa mdanganyika lakini linapokuja suala la usalama wa kaya nao hawajui cha kufanya!? Kama ni kweli wanafanya kazi “araundi ze kloku” kama msemavyo ninyi, nini kilifanya hadi ‘tanchi’ la ijumaa 17 likatokea? 

Ha ha ha ha ha ha ha!!! Nicheke kama mazuri. Kwani hamkujua kwamba kwa kuruhusu watu hawa ‘wasiojulikana’ kuufunga mji siku moja mliwatumia salaam kwamba wanaweza kufunga mji wakati wowote watakao! Haya sasa wameanza kuufunga kila wanapotaka na mimi humu sasa nahusikaje?. 

Haya, hili sasa limekwishatokea. Lakini hivi ni kweli kwamba wale wanaohamasisha vurugu hizi wanatumia maneno matupu kama mnavyotaka niamini miye kitukuu wa Pangupakavu!? Naapa humu miye sihusiki. Nakataa kuhusika maana ikiwa ni uhafidhina wangu ama ni kweli waliyosema wale waliosema kale, basi “maneno matupu hayavunji mfupa” sasa nyie mwaniambiaje ati wanaoshawishi vurugu hizi wanasema maneno matupu yasiyo mashiko!? Sasa mbona mfupa unanjika!? Nitoeni nasema. 

Au mwataka niamini upinduzi  kwa kutumia ‘propara lenye maganda’ kwamba  wadogo zake na Nchumali wa Chipoku ni wachoyo wa ‘asili mali’ zilizoko kwenye ardhi yao ilhali wao wamefaidi za wenzao? Nasema na kwa hili mnitoe. Haya, basi tumieni wingi wa busara mlizojaaliwa na hata tukawaamini kuwavisha majoho mvaayo kujibu walau kwa kiwango cha uelewa wao ni kwanini viwanda vya sangara viko Mwanza, migodi ya Dhahabu iko Geita na Mara na viwanda vya Pamba na Kahawa viko mahala pa mazao hayo lakini vile vya kusindika Gesi vyajengwa huko kwingineko!? Sisemi hamna majibu ya swali hili, lakini yatoeni basi na kwa namna ya kueleweka hili na mimi nisishangae kama ninavyoendelea kushangaa. Bhaaaaa!! Mwanishangaza enyi wana.

Nasema mzaha mzaha hutumbua usaa, au kwa vile ninyi ni wa kisasa mwaamini mzaha mzaha huwafanya watu kucheka na hivyo kuongeza siku za kuishi!? Naapa ninyi ni kizazi cha wenye hekima na mtakapokufa ninyi basin a hekima nayo itakoma na humo nitoeni. 

Haya, nijuzeni na nyie wenye kufunga mji mwamkomoa nani!? Nasema hawa waliishauza nafsi zao na konzi la kifaranga halimuumizi Kicheche enyi wana. Kwani mnadhani ikiwa mmefunga bishara na kuharibu uchumi wenu kwa siku kadhaa ndipo mmeweza kuwakomesha hawa ‘wezi’ wenu? Naapa wao walikwishashiba halali na mlungula kilichowasalia wao ni heshima na uishiwa na labda kesho ya vizazi vyao ambayo wao wanakusudia kuipata iwe kwa kumaliza vizazi vyenu ama kuharibu kesho ya wanenu, basi tumieni busara badala ya mabavu ilhali mli hali dhoofu kwa kula kidogo na kutenda kazi sana. 

Wacha niyamaze miye maana nasikia kaya yetu hii mama mkwe akitembea uchi unaruhusiwa tu kuwaza kwamba mama mkwe yu utupu lakini ukisema hivyo dhambi. Ati! Kwani mnadhani kama kweli mngekuwa mnaitia mafuta bawaba enyi wenye nyumba, zingetoka wapi kele za mlango ijapokuwa kusema kweli haziwakoseshi usingizi!?. Simo nasema. 

Basi kaka yetu, mkulu wa kaya hii ya Wadanganyika walipa kodi. Wacha nikomee hapa nikatafute sehemu ya kuegesha kichwa changu maana lile pagala nililokuwa nikilala juzi na jana mmelibomolea mbali wakati wenye “siri kali” mlipokuwa mkipambana na “wahuni” katika kujaribu kulinda “siri kali” yenu isivuje pasina kujiuliza kinachoivujisha ni sakafu iliyoloa ama tundu kwenye chombo chenye kutunza “siri” yenyewe?. Ama kweli fahari wawili wapiganapo, ziumiazo nyasi na mara hii Chokoraa nimekuwa nyasi kavu kwenye uwanja wa vita vya fahari wa Faru na Sisimizi. Simo.

Salaam Mheshimiwa, ni mimi mdharauliwa wako Chokoraa wa Muhangaikaji wa Mlalahoi wa Pangupakavu wa Kabwela wa Mdanganyika nakusalimia.