Friday, June 28, 2013

"SHIKAMOO" MKULU WA GUNIA.



Shikamoo Mkulu wa Gunia. 

Shikamoo si salaam mwana wa Muhangaikaji  nilikataa tangu zama ila sasa, shikamoo mkulu wa gunia. Nasema shikamoo si kwa kukuamkua maana ningekuamkua ningesema salaam nakusalimia lakini nasema tena kwa sauti ya juu unisikie ijapo kusema kweli akina kaka Muishiwa wamenifungia juu ya dari ya nyumba tena kwenye paa la choo ili nisionekane mbele yako, ila naamini sauti yangu itakufikia ewe mkuu wa gunia hili tambala bovu tuishilo sisi wana wa Adamu, shikamoo mkulu wa gunia. 

Ha ha ha ha ha ha!!! Nimekumbuka zamani enzi zile wakati wazee wangu hasa mama yangu Shida wa Matatizo wa Taabu Malingumu alipokuwa akiniamsha lukwiri ili niende huko kwenye jando la kikoloni kufundwa ujinga wa kuidharau ‘ilimu’ ya babu na babu zangu kwa kuuita ushenzi ilhali tamaduni za mgeni zikiitwa uungwana, hilo si lengo la waraka huu, shikamoo mkulu wa gunia. 

Nakumbuka enzi hizo ikiwa Mkulu wa kaya ama wasaidizi wake walitembelea kijiji chetu, wote tuliambiwa tuoge, tuchane nywele zetu kwa mitindo ya kurithishwa na wakoloni wenyewe ati wakiita ‘kisasa’ bila kuheshimu ukweli kwamba hakuwezi kuwapo na sasa bila zamani na mjukuu ni matokeo ya babu, humu namo simo ila, shikamoo mkulu wa gunia. 

Tulijipanga mabarabarani na enzi hizo barabara zenyewe zilikuwa za vumbi tupu na ole wetu ikiwa ulikuwa msimu wa mvua na siye na shati zetu nyeupe kwa weupe wa mkorogo, letu lilikuwa tope na maji machafu wakati walinzi wa ‘mkulu wa kaya’ wakipita na magari yao na siye tukijitahidi kupunga mikono na kulazimisha tabasamu nasema enzi ni enzi na kumbe historia hujirudi, shikamoo mkulu wa gunia. 

Mkulu wa Gunia, mwana wa wana wa Hamu ndugu wa Shemu na Yafethi kwa mujibu wa misaafu iliyoletwa na wale uwatawalo leo, nimemua kupaza sauti kwanza nikukumbushe japo najua wajua ya kwamba shikamoo humaanisha niko chini ya miguu yako na hilo ndilo ninalotaka kukwambia leo, niko chini ya miguu yako na kusema kweli unanikanyaga. Sikulaumu. Wala! Hata kidogo. Nani kasema nakulaumu? Miye sikulaumu kwa vile kama walivyofanya babu zako ambao walipokuja wageni wenye pua ndefu na tabasamu za unafiki uonekanao kama urafiki, waliwakuta babu zetu wakiwazika machifu mikononi mwa walio hai na waliozikwa hao ati kumsindikiza chifu kwenye safari yake ya mwisho walikufa kwa ujasiri ati kwa vile walikuwa mashujaa na mimi ni shujaa mtukufu mkulu wa gunia. 

Mimi ni shujaa ila si shujaa wako bali shujaa wa kaka Muishiwa kwa vile tangu ulipotangaza kwamba waja huku kwetu mimi niko chini ya miguu yako na hata mkate wa wanangu niliokuwa nimeukumbatia kifuani kwangu nao sasa umesagika kwa kule tu mimi kuwa chini ya miguu yako. 

Ha ha ha ha ha ha!!! Usitake nikutajia jina la marehemu bibi yangu mzaa mama yangu wewe aliyeniambia mbwa mwitu na mbuzi hukaa kundi moja tena bila kuchokozana ama kuogopana Simba anapoingia kichakani na sasa kwa sehemu nasadiki.

Ati! Nasema uji wako kwenye ardhi ya wadanganyika walipa kodi umenikumbusha mambo mengi mojawapo ni mzee yule aliyekuwa mwenye kigoda cha kijiji chetu. Pamoja na kuwa mtu mkubwa sana wa enzi zake lakini hakuwa na shati hata moja lisilo na tobo mabegani na siku moja Mkufunzi alipotembelea darasa lake na kuamua kukagua usafi, yule mzee kwa vile alijua Mkufunzi angekagua mavazi alikuwa amevaa koti zuri juu ya shati lake ila kwa vile mkufunzi alipoamuru huyo mzee avue koti lake ndipo tukagundua kumbe mabega na mgogo vilikuwa wazi. Ha ha ha ha ha ha!!! Nicheke kama mazuri Chokoraa miye. 

 Najua!!! Najua, najua unashangaa kusikia Mkufunzi alitutembelea na kumvua yule mzee shati lake kwenye ukaguzi wa usafi wakati unajua mkufunzi huwa anakagua wanafunzi pekee ila ulichosahau ama kudharau ni kwamba wakati huo kaya yetu yote ilikuwa shule na mkufunzi alikuwa mmoja akituongoza kama Mussa na Israel hayo unayajua kwa hiyo , shikamoo mkulu wa gunia. 

Wacha nikumalizie kisa hicho halafu ninyamaze maana najua akina kaka Muishiwa kwa sasa wamenuna ati Chokoraa nampigia kele mgeni na ndiyo maana ati kwa vile miye siujui ‘ustaarabu’ wamenikataza kuja mjini. Mkufunzi baada ya kumvua koti yule mzee na kumkuta amevaa shati lililochanika akaamuru atandikwe viboko sita pale pale na mimi nikajihoji, kwanini kumtandika mtu aliyejaribu kujiheshimu mbele ya mgeni!? Mkufunzi akanisikia wakati najihoji inawezekana nilijisahau nikawa nazungumza kwa sauti, akaniita mbele. Weeeee! Hukuwapo maana ungecheke sana jinsi nilivyokuwa nikitetema.

 Nilijua leo na miye vyangu sita ninavipata lakini mzee yule Mkufunzi alikuwa heshi visa, ati akaanza kunifafanulia Chokoraa miye ni kwanini alimtandika mzee yule viboko sita. Akasema kwa kitendo cha mzee yule kuficha shati lake lililochanika, mkufunzi angeondoka kijijini ameridhika kwamba mambo yako barabara maana hata mwenye kigoda kava suti kumbe ndani malapulapu na hivyo asingetuma tena “kilimpilini” pale kijijini mwaka huo labda baada ya miaka sita na hivyo aliamua kumtandika kwa vile mwenyekigoda alimficha ukweli wa mambo. Ha ha ha ha ha ha!!! Natamani na wewe mkulu wa gunia ungekuwa na busara ya kujua kilichojificha nyuma ya jiji safi unalolipitia unapotokea kwenye stendi ya mwewe! Lakini waaaapi! Kwani watakwambia!?.

Hata wakikwambia kwani utawafanyaje zaidi ya kuwapongeza kwa juhudi ya kusafisha jiji? Nasema uchafu waliouondoa ni mimi na ndugu zangu akina Seremala, makenika, machine na yule Ntilie, mdogo wake na mama yao Mama Lishe, na miye nauliza, kwani sisi sasa ni takataka kwenye kaya yetu wenyewe ati kwa ajiri ya ujio wako? Naomba kujua unaoga maji ama maziwa!?. Ila bado zijajiinua wasijeniangushia vitu vilipukavyo, bado niko chini ya miguu yako mkulu wa gunia. 

Nasema kumbe ukweli na uwazi ni mchezo mgumu kuucheza na yawezekana wanaohofia na wanachokihofia miye nakijua. Ati! Sikia huyu naye! Ati wanahofia usalama wako? Nani kasema! Hawana mashaka na usalama wako maana kama wao wenyewe tu wako salama iweje wewe na maguvu yote uliyo nayo na ‘utukutu’ uliojifunika nao usiwe salama katika kaya ya amani na utulivu!? Na huyu, ati wanahofia maandamano na si hasa!? Hilo nalo si kweli maana hayo yaweza kutokea popote na vyovyote ila wadanganyika siye hatuna kawaida ya kuwafanzia fujo wangeni kuuana twauana wenyewe lakini mgeni yuko salama.

 Wanachohofia mimi nitakwambia ijapo najua ukiondoka nitakiona cha mtema kuni. Ndiyo, ukiwapo hawanigusi kwa vile, niko chini ya miguu yako. 

Wanaogopa usije ukawauliza zile shekel, noti na mifedha kedekede uliyowapa walete kuboresha maisha ya wadanganyika imefanya nini ikiwa miaka hamsini ati baada ya bendera bado wadanagnyika wanaishi chini ya nusu dola kwa siku!? Nani kasema wanaishi chini ya dola moja? Kwani dola moja si sawa na “si nyingi” zetu harufu mbili! Naapa wako wadanganyika miongoni mwetu ambao wanaamka na kuzitafuta “si nyingi” tamo mia na wasizipate hao wanaishije chini la dola moja!?.  Wanaogopa utawauliza kuhusu magari yao ya kifahari wanayoendesha ilhali mama Ntilie na Machinga hawajui watakula nini na hivyo wanapotuondoa akina siye mjini utakaoukutana nao ni “wao” na hivyo hutojua kundi la akina siye tuko wapi na kuondoka ukidhani na “sisi” ni kama “wao” kumbe pana tofauti kubwa. Natamani kuendelea kusema lakini naonga kama uzito wako unaongezeka na mimi pumzi zinapungua kwa sababu, niko chini ya miguu yako. 


Wasalaam, ni mimi Chokoraa wa Muhangaikaji wa Mlalahio wa Pangupakavu wa Kabwela wa Mdanganyika nakusalimia. Shikamoo Mkulu wa Gunia.