Thursday, August 22, 2013

Pole kwa Msiba Muishiwa Mkulu wa Kaya.



Salaam nakusalimia. Hizi ni Salamu kwako wewe, ndiyo wewe mkulu wa kaya ya Wadanganyika walipa kodi kutoka kwangu Chokoraa wa Muhangaikaji wa Mlalahoi wa Pangupakavu wa Kabwela wa Mdanganyika nakusalimu, Shikamoo Mheshimiwa. 

Nasema tena kama nilivyowahi kusema hapo kabla kwamba shikamoo si salaam bali mazao ya ukoloni mkongwe lakini wacha niitumie kwako kwa vile hasa ni ukweli usiopingika kwamba niko chini ya miguu yako, shikamoo Muishiwa, aha! Samahani, shikamoo Mheshimiwa. 

Nataka , nimesema nataka wala siombi maana Chokoraa miye sifungwi na ‘proto kali’ ninapotaka kuzungumza na mkulu wa kaya yangu kwa vile yaliyonijaa moyoni ni mazito maana yanatishia heshima ya Mdharauliwa miye kwako wewe Mheshimiwa sana mkulu wa kaya yangu na hapa salaam nakusalimia. 

Hivi! Kwani heshima ni kitu cha bure kama wasemavyo waswahili wa Danganyika yetu!? Si kweli. Naapa ni uongo kuniambia ati heshima ni kitu cha bure maana nijuavyo miye mwana wa Muhangaikaji heshima hulipiwa gharama kubwa ya juhudi, utu, kujituma, kutenda mema na kutumia nafasi na vipawa ulivyojaaliwa na mwenyezi  na pia kuaminiwa na wadanganyika wenzako kwamba waweza kusema na hata kutenda kwa niaba yao na hapa salaam nakusalimia. 

Wala! Wala usinichukulie miye mwana wa Mdanganyika kuwa mmoja wa waungaji mkono wako mbumbumbu ambao hawawezi katu kukwambia ukweli pale unapovurunda katika kutenda yale tuliyoyakasimu kwako kutenda lakini pia si mnafiki miye kitukuu wa Mlalahoi wa kutokusifia unapotenda zaidi ya nilivyotaraji. Nimesema unapotenda zaidi siyo unapotenda kwa kiwango tarajari na humu sasa najitoa maana simo. Nasema kwangu kama unayo masikio ya popo basi yafunike maana ikiwa nitayaona nitasema hadharani kwamba mfalme ana masikio kama popo. 

Hilo si lengo la waraka wangu leo hata hivyo hizo zilikuwa salaam tu na kusalimia mkulu wa kaya ya Wadanganyika Walipa Kodi. Leo ninataka kukueleza kuhusu Heshima ya Mheshimiwa wewe ambaye Mdharauliwa miye ili nikufikie na kukusalimu ni lazima kwanza nitambae mwendo mrefu nikijiangusha chini kila baada ya hatua kadhaa ati kwa vile heshima siku hizi ni shikamoo, basi shikamoo Mheshimiwa.
Nasema ni juzi tu hapa Yule Mnyarwanda alikutupia matusi ya nguoni kwa kumshauri jinsi ya kuishi vyema nyumbani kwake ati kwa kisingizio cha kwamba unaingilia mambo yake ya ndani ilhali kila anapogombana na mkewe wewe ndiye unawapa wanae malazi na chakula. Nadhani huyu ameifanya hii kuwa mbinu ya wewe kumlelea wanae na hii si hoja yangu lakini ni sehemu ya salamu, shikamoo Mheshimiwa. 

Kilichonifanya nikuandikie leo ni kukupa pole kwa msiba, msiba mzito wa walinzi wa kaya yetu hii ya wadanganyika walipa kodi nasema kwa hili wakati ninapoandika Chokoraa machozi yanilengalenga. Silii kwa sababu ya msiba wenyewe maana twafwa sote tu kama upepo upitao na kwenda zake na siku zetu si nyingi juu ya dunia gunia letu hili lakini kinachonisikitisha ni mazingira yenyewe ya vifo vyao.
Najiuliza ni wapi ulipochorwa ule mstari mwekundu unaoweka tofauti kati ya amani na vita na ikiwa kwa hili mstari huu haujavukwa maana mbele naona giza, ila bado nakusalimu, shikamoo mheshimiwa.
Hivi hawa wanaopigana na kuuana kila kuitwapo leo “watwawala” wao si wameamua kwa makusudi kuwateketeza vijana wao walio matumaini ya jamii yao kwa maslahi binafsi hadi pale walipokuja kushtuka maji yashazidi unga na wakaomba kuwapo kwa msaada kutoka kwa jirani?. Ndiyo, na sisi tukawatumia wajumbe wa amani na nani alisema ni mjumbe hauawi!? Naapa aliyenena hili ama alitudanganya au tulijidanganya wenyewe kwa kumsadiki maana wajumbe wa amani wameuawa kwenye uwanja wa vita na mimi nasema huu ni upuuzi. 

Ndiyo. Ni upuuzi kumtuma mwalimu darasani bila chaki wala kitabu ama mkulima shambani bila jembe au hata Chokoraa jalalani bila mfumo wa Rambo asomaye na afahamu na sasa ndugu zetu hawa wamekwenda. 

Ndugu zetu hawa wamekwenda tena walio wengi wamekwenda na ndoto zao, na matumaini yao ya kesho yamezimika na hata wale waliobaki nyumbani ambao matumaini yao yalifungwa kwa hawa basi hawa waliokwenda wamekwenda nayo na itawachukua waliobaki miaka kama si dahali kujenga matumaini mapya na kama ilivyo kovu alisafishwi kwa sabuni likaisha, hawa wamekwenda. 

Kinachonifanya nikuandikie siyo tu kukupa pole bali kukutaka ujivike wewe viatu vya wale waliobaki nyuma ya hawa waliokwenda na ambao siku za usoni pia watakwenda kama ambavyo pia mimi na wewe tutakwenda hiyo njia ya watu wote lakini kwa sasa tuvae viatu vya walio hai maana waliokwenda wamekwenda na hakuna njia ya kurudia huko waendako watu wote. 

Najua, najua utataka kutumia tena busara kwenye hili na hapa mwana wa Muhangaikaji naomba nijitoe maana simo. Ala! Kwani si nimeona tangu umekalia kitu hicho jinsi ambavyo matumizi ya busara yamezaa hasara nyingi kuliko faida ama wataka nikukumbushe kidogo!?. Haya, ebu kumbuka wale walioanza kuhubiri upuuzi wa kipuuzi na kutugawa kwa misingi ya dini, kwani habari hizi hazikufika mezani kwako kwa wakati na ukaamua kutumia busara kukabiliana nao!? Ona sasa tulipofika ambapo hata majalalani Machokoraa twaulizana dini kabla ya kupeana kipande cha boflo na wali uliolala ukatupwa asubuhi. Humu namo simo. 

Tazama, tazama jinsi ambavyo wale waliotuhumiwa kwa ufisadi mkubwa na wakathibitika ulivyotumia busara ya kuwataka warudishe walichoiba badala ya kufichua mwizi na kumwadhibu kwa kadri ya miiko na vijiko vya kaya yetu na mwisho wa siku ni hao hao waliotangaza ati wewe ni dhaifu na hasira zikawapanda wale walio na ngazi za kupandisha hasira hizo miye nikajitoa kama ambavyo hata sasa najitoa. 

Ona jinsi ambavyo ati baada ya fedha kedekede za wadanganyika kutumika kununua Rada na hawa wadanganyika tukatakiwa kula nyasi kama Mbuzi kwa ajiri hiyo bado wanyama wetu walipakiwa kwenye dege tena la kijeshi na kurushwa nje ya kaya yetu na hata sasa bado imetumika busara. Sitaki kusemea wale walioua waandishi na wengine wengi na madhila ya kila leo yawapatayo wadanganyika ilhali wewe mkulu wa kaya ukiwa unaendelea kutumia busara. 

Leo sicheki, nasema sicheki kwa vile nina huzuni na hasira maana nakumbuka kuna wakati wako walioomba ati uwe mkali walau kiduchu tu ili heshima ya uheshimiwa ilindwe lakini naamini hata hao nao ulitumia busara kutowasikiliza kama ambavyo unatumia busara kuwaachilia wale waliokuwa kituoni na wenye wajibu wa kulinda raia na mali zao wanapovamiwa na kuibiwa na hata sasa bado busara ingali inatumika na ndiyo maana najitoa. 

Nakuandikia nikuombe kwa hili muishiwa, aha! Nisamehe, mheshimiwa sana mkulu wa kaya ya Danganyika ya Wadanganyika walipa kodi usitumie busara hata kidogo. Nasema si sahihi kuwa sahihi mara zote maana hilo humaanisha kwamba ustaarabu kwa mpumbavu huonekana kuwa uoga na ndiyo maana hata wale tuliowale na kuwalisha leo wanatutukana na wewe unatumia busara ilhali matusi yao hayaishii kwako tu maana shati ulilovaa kipande chake nimevaa mimi na wadogo zangu wengine watoto wa baba yetu Mdanganyika na hivyo utomvu wao wa nidhamu watuchafua wote japo kusema kweli wewe wachafuka sana maana uko hukoooo mbele yetu. 

Kwani hatuwajui wakuu wa hawa wauaji waliowaua vijana wetu? Wako wapi akina Sikamona na wenzie ama waliishia tu kwenye mawazo ya akina Mtobwa na hivyo Danganyika yetu haina tena mashujaa wa Salaamu toka kuzimu ili wawapelekee salamu wajinga hawa kwa ujinga wao wa kuwaua wajumbe wetu wa amani ilhali wanajua fika mjumbe hauawi!?. 

Nasema ni wakati sasa vijana wetu wavuke mipaka wakawatafute wahalifu hawa na kuwaleta hapa kwenye kaya yetu ili tuwakalishe kwenye ule mbuyu mkubwa na kuwazodoa kwa mawe na maembe mfu na ujumbe ufike kwa jirani kwamba kila atakayemgusa Mdanganyika pasipo kuzingatia taratibu atazodolewa. 

Nasema sisi kwa sisi tugombane na kuumizana maana mwanao ukimpiga mwenyewe unajua kiwango cha adhabu lakini anapopigwa na jirani huna budi kujua sababu vinginevyo umeshindwa kuwa baba na kumfunda mwanao kuwalinda wanawe baada yake na humu miye simo ila salaamu nakusalimia.
Nasikia umemtumia salaam mkulu mwenzio wa kaya ya jirani afanye “haraka” kumtafuta nyoka aliyeuma vijana wetu maana yumo humo ndani mwake na kwamba ikiwa atashindwa kumpata “haraka” basi utawatuma vijana wako kumkamata mwenyewe huyo nyoka na Chokoraa nauliza tafsiri yako ya “haraka” mara hii inamaanisha nini !!?. 

Ni mimi Mdharauliwa wako, Chokoraa wa Muhangaikaji wa Mlalahoi wa Pangupakavu wa Kabwela wa Mdanganyika  Mlipakodi nakusalimia. Shikamoo Mheshimiwa.