Tuesday, September 3, 2013

Salaam Mkulu wa Sungu Sungu.



Nimepata ujumbe  unasema nijihadhari na haya ‘matakataka’ yangu niyamwagayo  kwenye milango ya majumba ya ‘waishiwa’ maana ati yanatoa harufu mbaya yenye kuwakela waishipo kwenye mahekalu yao hayo ambayo ati nayo wameyapata si kwa halali. Nimekusikia ndugu yangu  na ndiyo maana sijathubutu kwa karibu majuma kadhaa sasa kupita mitaani kwao ila leo nimelazimika kuja kumsalimu mkulu wa sungusungu wa kijiji, mkulu salaam nakusalimia, shikamoo mkulu wa sungusungu. 

Wanasema ati wewe umetumia muda wako mwingi tangu ulipotoka pale kwenye jando la kijiji lililoko Mlimani, ukiwa nje ya kaya yetu  hii ati tena ukifanya kazi na wale wenye rangi nyeupe na kutudanganya siye kwa tabasamu na hivyo mkulu wa kaya alipokuteua wewe kuwa mshika “manati za ndhungu” mkuu wa kitengo hiki cha sungu sungu, Wadanganyika walipakodi walikuwa na matumaini makubwa na wewe lakini ati kwa kadri siku zilivyokwenda sasa Wadanganyika hawa hawa wanawaogopa vijana wako kiasi wewe hawakuogopi bali wanakuabudu na humo miye simo maana nimekuja tu kukusalimu, shikamoo mkulu wa sungusungu. 

Ndiyo nasema na wewe mtoto wa mtu Mwema ambaye kwa wema wake alikutuma wewe kwenye jando la kijiji ili ukiisha kuyapata mafunzo ya jando  uje tena hapa kwenye kaya yetu utusaidie sisi watoto wa mzee Mdanganyika Mlipa kodi na ati vile visenti vilivyokupeleka wewe jandoni vilikopwa kwa baba yetu mzee Mdanganyika  wa Mlipa kodi na ndiyo maana miye nakusalimu, shikamoo mkulu wa sungusungu. 

Ngoja! Nielewe na uniamini  ewe mwana maana sina dhihaka hata kidogo nisemapo “niko chini ya miguu yako” kwa vile ni kweli unanikanyaga na wala siwezi hata kujaribu kujiinua maana ni bora unikanyage wewe kuliko nidunguliwe na ‘manati’ za vitegemezi vyako na humo miye unitoe maana simo. 

Kinachonitisha miye si kule kujua kwamba hata salaam hizi zaweza ama kupelekea miye kudunguliwa na manati za ndhungu zilizo mikononi mwa vitegemezi vyako ati kwa vile miye “nimewakosea adabu” sungusungu wa kaya yetu, lakini nasikia ati huko uliko wewe mkulu wa sungusungu mumeanzisha mchezo wa kuoshana maji moto mkibabuana sura kama mwataka kutengeneza staftahi kwa sura za wenzenu na miye humo msinihusishe maana simo. 

Wacha niliseme hili walau niondoe funda lililonikaba kooni maana uhai naupenda na uzima kuliko maradhi lakini uhuru wa kweli huja kwa fikra sahihi na hizo huja kwa lugha sahihi na miye humu sasa nahusikaje?. Aala! Usinitanie. Nasema mzaha wako utatumbua usaha we mwana sikiliza Chokoraa nikueleze yaliyo ya kweli maana unajua yaliyokuwa kwa wale waliokuwa kwenye kiti chako kabla yako na jinsi ambavyo leo hawana heshima isipokuwa nyumbani kwao na hivyo limetanguka lile lililonenwa na manabii kuwa nabii hana heshima kwao, ama hawakuwa manabii na hivyo haliwahusu hilo la nabii kukosa heshima kwao. 

Nani hajui kwamba zilikuwa enzi katika kaya yetu hii hii ambazo watu ati alitumwa tu binti ‘fatuma’ akavunja malango ya watu na wafuasi wakanyang’anya mali na uhai!? 

Hayo sasa yamepita na sasa mwamwagiana ‘mtindi mkali’ na humu miye sasa nahusikaje!?. Simo naapa. Nasema Wadanganyika sasa wamehama makwao wanaishi nyumba za jirani yao Yule mzee mwenye sura mbaya Hofu wa Uoga ati kwa vile kuishi kwao uwaogofya sana hadi wamezoea kuishi “na” kama si kuishi “kwa” Hofu na ndiyo maana miye salaam nakusalimia. 

Nasema ingawa umewapunguzia mzigo wadogo zangu wale wawili Mzembe na Mzururaji wenye  umaarufu wa harufu na hata majina yao siyasikii yakitajwa sana kama ilivyokuwa kwa watangulizi wako, lakini ati kaka yangu Machinga wa Muhangaikaji siku hizi ndiye amechukua zamu ya kusumbuliwa, na ati wadanganyika wanadai imekuwa sawa alivyosema Mkufunzi enzi za uhai wake kwamba ati ‘siri kali’ ikiishakuwa imetoboka inavuja basi hubakia kukimbizana na vijitu vidogo mabarabarani, kwa vile akina kaka mkubwa Mstahiki wa Mtukuka huwa ati wewe na vijana wako mwaogopa kuwagusa kwa vile watakataa “kuja” ila miye humo simo. 

Nasema mimi jina langu halisi ni Chokoraa wa Muhangaikaji naomba msinifananishe na wale vijana wawili wa mzee Si Hasa akina Mchochezi na Mropokaji ingawa tumekua pamoja ila mwenzao  majalala yamenifunda kuwa na adabu ndiposa mkulu miye nakusalimia, shikamoo mkulu wa sungusungu. Sisemi, ndiyo, sisemi kwamba akina mzembe na mzururaji na hata kaka yangu Machinga wa Muhangaikaji wanaruhusiwa kukosa adabu ati kwa vile akina kaka Mstahiki na hata Yule kaka yetu mkubwa Muishiwa wa Mbadhilifu wanaukosea adabu msaafu na mafunzo ya kaya yetu, lakini nasema imekuwaje hata imekuwa kwamba nyie wenye kuijua siri ya mzazi wa Amani bi Haki binti Wajibu na nyie mmekuwa ndumilakuwili mkiufuata msemo wa waswahili kwamba haja kubwa ya ng'ombe mbolea ya bata uchafu!?. 

Haya, nasikia sasa si salama hadi kwenye viota vyenu wenyewe na miye nasema hivi na nyie mlishiriki kula pesa ya sanda ya marehemu Uadilifu hata mkasababisha mzee yule kuzikwa pasipo sanda!?. Ha ha ha ha ha ha ! Nicheke miye maana ikiwa na nyie mlio na taa haramu ya kumulika ili wengine tuone mwatembea gizani kwa uzembe wa kuitia kandiri mafuta, itakuwaje basi yule mama yangu bi kikongwe Shida wa Matatizo wa Taabu wa Muhangaikaji!?. 

Naona kama muda unaniishia nachelea nisikute paka na mbwa wamemaliza vile vilivyotupwa jana jalalani ndiyo maana nakuomba uniruhusu tena juma lijalo nije nikuletee ujumbe nilioagizwa na dada na kaka zangu watoto wa Mdanganyika. Ndiyo, nitakuja tena kwa ajiri ya kukuletea salaam baada ya kuuguza vidonda vya mkong’oto niliopokea kutoka kwa vijana wako nilipojaribu kuukaribia mlango wa afisi yako ili nikusalimu. Mmoja wa vijana wako aliponiona ati akaniita jina si langu eti “we kibaka, watafuta nini karibu na Muishiwa Mkulu wa Sungusungu?”, ile kujaribu kujieleza kwamba miye ni Chokoraa wa Muhangaikaji na si Kibaka, kidundo nilichoambulia ukichanganya na uzito wa ujumbe nilio nao kutoka huko kwetu, ndiyo maana sauti yanitetema nizungumzapo ingawa nina hakika salaam zitafika, salaam nakusalimia. 

Ni mimi mdharauliwa wako, Chokoraa wa Muhangaikaji wa Mlalahoi wa Pangupakavu wa Kabwela wa Mdanganyika wa Mlipakodi nakusalimia, shikamoo mkulu wa Sungusungu.