Friday, January 3, 2014

Mgeni Njoo Mwenyeji Akome.



Salaam nawasalimia. Najua mwaka wa jana umekwenda na najua wengi wenu bado mngali kwenye zile nyumba zenu zenye baridi ya kutengeneza huku mkijituma wengine kuijenga na wengine kuivunja kaya ya wadanganyika na ati bado mwashangaa kwanini jengo halikamiliki. Mwashangaa nini?. Nasema ikiwa walio wengi mnafanya kazi ya kubomoa ilhali wachache tena wenye nguvu chache wanafanya kazi ya kujenga si ajabu itawachukua miaka dahali walau kulifikisha jengo kwenye ‘renta’ ila humo miye simo bali salaam nawasalimia. Shikamoooni Wadanganyika. 

Nisemeje!?. Mwataka nirudie kuwakumbusha madhila yaliyotukuta kwa mwaka uliopita?. Katu. Nasema siendi safari ya maili kumi elfu kinyumenyume asomaye na afahamu ila mi salaam nawasalimia. Jana imepita na kesho si yetu lakini ikitumika vyema leo walau kesho yaweza kuwa na matumaini na miye hapa nawasalimia. Kwa mwaka huu naapa sitasema matukio bali mazoea na tabia zenu maana tabia hutengeneza utamaduni wa jamii na miye nakuulizeni enyi wana  wa Mdanganyika Mlipakodi nani aliyekundanganyeni kwamba kuna kaya nyingine mtakwenda baada ya Danganyika yenu hii?. Ala! Washangaa nini?. Kwani si miye nakuoneni mnavyoishi kama watalii tu hapa kwenye kaya yetu kila mmoja akijaribu kuwa kama wale waliowatawala babu zetu bila kujua kwamba twatofautiana siyo tu ngozi bali mtizamo na miye humu nitoeni.

Ha ha ha ha ha ha!!!! Nakumbuka Mkulu wa Kaya kabla ya ule “Uchafuzi Mkuu” wa mwaka uleeeee ulitukasirisha sisi Wadanganyika hata tukapiga kura na kumpa yeye aslimia zaidi ya thamanini ya ‘kula’ zetu huku tukisahau kwamba tuna zaidi ya asilimia tisini ya familia za kulishwa na ‘kula’ hizo za bwelele, alituahidi ajiira makumi mia na sasa leo twalalama na miye nauliza twalalama nini?. 

Mwaka wa jana Chokoraa wa Muhangaikaji wa Mlalahoi wa Pangupakavu wa Kabwela wa Mdanganyika Mlipakodi nimezunguka majalala yote tangu yale ya uswahilini kwetu kunakotupwa miiba ya dagaa hadi yale ya waishiwa kunakotupwa boflo na mapande ya nyama ati kwa vile yamekaa sana kwenye jokofu yakakosa radha, naapa mwakufuru enyi wana. Kwani mabucha hamkuyaona hadi mwanunua vyakula na kisha kuvitupa kwa kujifanya uzungu usio tija!?. Simo naapa. Kwani msipotupa Chokoraa miye nitakula nini? Lakini walau jifunzeni kumheshimu Mwenyezi aliyekupeni nyie kusaza siyo kwamba mtupe jalalani bali mtupe siye tusio hata na kidogo na miye humo nahusikaje?. Simo.
Nasema katika kuzurura kwangu nimejifunza jambo moja kuu na hapa salaamu nawasalimu wale sungu sungu wa mipaka yetu na wale manyapara wenye jukumu la kusimamia vibarua vya kaya yetu, shikamooni waishiwa. Nauliza, hivi waishiwa nyie mnafahamu  uzito na upana wa majukumu yenu au kwavile kama wasemavyo  wadogo zangu wale akina Mzembe na Mzururaji kwamba kaya imeuzwa basi na nyie mmeamua kuuza na utu wetu? Naapa humu miye nisihusishwe. 

Nasema kuanzia kule kwa akina Ngosha kwenye viwanda vya samaki hadi kwa akina Nchumali kwenye Korosho wadanganyika nyie hamna chenu  ati kisa mnatekeleza sera ya ‘Ukewenzaji’ na miye nauliza mbona ‘Ukewenzaji’ huu mwabakwa nyie na sisikii hata lalamiko?. Ha ha ha ha ha ha!!!!! Ninyamaze miye maana si ajabu mkaniuliza kanituma nani wakati miye ni salaam tu nawasalimia. 

Hivi wakati mlipoamua ‘kubinua na kufisha’ viwanda vyetu vyote tulivyorithi kutoka kwa wazee wetu Waishiwa nyie mliamua kubinua na kufisha hata ajira zetu?. Ha ha ha ha ha!!! Chokoraa miye nimepita na kukutana na wageni wakikaa kwenye majumba ya viyoyozi huku wakiwa hawajui hata kuandika idadi ya mali inayoingia na kutoka viwandani zaidi ya utaalamu wa kujua kuvaa na tabasamu za kikoloni na ujasiri wa macho wa kuwatazameni usoni mnaposhikana mikono kusalimiana na miye nauliza, hivi hakuna kati ya Wadanganyika wataalamu wa kufanya kazi hizi hadi mwatuletea wataalamu “feki” wenye kujua tu tabasamu na “hendisheki” ilhali utendaji wote wafanywa na akina “sabani” asomaye na afahamu?!!! Simo humu. 

Nani hakumbuki jinsi ambavyo kwenye migodi ya dhahabu kulikuwa na wageni waliokuwa wakiitwa “sekyurite sipeshialisiti” ati kwa vile wanatokea Unepali ilhali kwao walikuwa makplo na masajenti huku makapteni na maluteni wetu wastaafu wakisota mitaani kutafuta ugali wa kulisha watoto!? Naapa historia inajurudia na miye humu simo. 

Bado kidogo. Sijamaliza, naomba kuuliza wakati “wakewenzaji” hawa wanapoleta msururu wa “wataa haramu” hawa na kuwavusha kwenye stendi za mabasi ya hewani, wanawaeleza wataalamu wetu wa uhamiaji kwamba wanakuja ‘kuisaidia’ kaya yetu kwa lipi?. Au ndiyo yale yale ya kiazi kuitwa kwa lugha ya kitaalamu “potato”?!!!!. Naapa sihusiki.  Haya, endeleeni na michezo hii ya mbuni ya kuficha vichwa mchangani ili mkirudishe kizazi chetu kwenye ukoloni kule ambako babu zetu walipigana kufa na kupona kututoa sisi halafu na nyie mtakapolala na baba zenu mkiiendea njia ya watu wote mkumbukwe kama wasaliti wa juhudi za wazee wenu na miye humo nisihusishwe maana simo tena simo kabisaaaaa, sihusiki. 

Haya, na nyie mjiitao wakulu wa kazi na ajira wa kaya yetu, mmeshindwa nini kutengeneza torati ya kulinda ajira za wadanganyika wenzenu na kuzisimamia?. Ha ha ha ha ha ha!!!! Najua, najua mwaniona mjinga kwa vile wadogo wakisimamisha pembe wakubwa wapewa bahasha na mambo yanakwisha na miye humo nahusikaje? Lakini niseme miye nisijehukumiwa na kizazi kijacho kuwa mnafiki maana najua kama mungetaka kuyatenda yawapasayo yangetendeka lakini hiyari yashinda shuruti na miye humu nahusikaje?. Simo naapa. 

Haya, leo akina "Sabani" wamebaki kufukia hivyo "vidigirii" chini ya magodoro ya bibi zao huku wakipika chai na kufagia na kisha kwenda kufanya kazi za taaluma zao ili kuwafurahisha "mabosi" wasiojua hata kusoma na kuandika lakini wenye vibali halali tena vya kufanya kazi za taaluma kwenye kaya yetu na miye humu nahusikaje maana simo. Nauliza katika kutembea kwenu kote huko mwendako mmeshindwa kujifunza kwamba kaya za wenzetu hata kabla hujaenda wanakupima hata magonjwa wajiridhishe juu ya usalama wao na watu hao?. Nani aliyekurogeni enyi wana wa kushi?. Simo naapa. 

Ni mimi ndugu yenu Chokoraa wa Muhangaikaji wa Mlalahoi wa Pangupakavu wa Kabwela wa Mdanganyika Mlipakodi nawasalimia, Shikamooni Wadanganyika Walipakodi.