Saturday, January 14, 2012

Wadanganyika na Kelele za Mlango.

Ngoja kwanza nicheke. Ha ha ha ha ha ha ha!!! Nacheka miye Chokoraa wa Muhangaikaji wa Mlalahoi wa Pangu Pakavu wa Kabwela wa Mdanganyika.  Leo, tofauti na siku zote ni furaha. Ndiyo, mwaka huu umeanza kwa mafanikio makubwa na kwa hilo namshukuru ‘Mulungu’. Ona huyu naye anakereka ati  kwa vile nimemwita kikwetu huyu ambaye yeye angetaka aitwe “God” ili ajiridhishe kwamba yeye ni mtumwa. Naapa simo. 


Nina furaha kwa vile mwaka huu Chokoraa nimepanda daraja, halafu nimepanda daraja mwanzoni mwa mwaka, ha ha ha ha ha ha!! Unashangaa!! Kwa sasa Chokoraa silali tena kwenye mitaro na huko hunikuti, nimepanga kichumba changu kimoja huku kwetu Uswazi kwenye kajumba ka mama Chausiku na hivyo silali tena chini ya daraja. Nani kasema hilo ni jambo dogo!?
Japo misosi yangu ni kule kule majalalani kama kawaida, lakini mara hii nafikiri hata majalala yangu itabidi yabadilike kidogo hasa kwa vile inabidi niwe kibiashara zaidi ili niweze kulipa kodi. Hilo nitakuhadithia ila leo, nataka kukueleza kero moja tu iliyonikuta. Kero ya mlango.


Kila mara “Ng’waaaaa!! Ng’waaaaaa!! Mlango huu wa bati unapiga kelele kila unapofunguliwa na Chokoraa hili linanikera  lakini kinachonishangaza ni kwamba mama Chau na watoto wake wala hilo haliwasumbui, nasema kweli mi nashangaa sana.  Ene wei, baada ya kuishi hapa walau kwa wiki mbili, nimeanza kuzoea hali hii na hivyo na mimi sasa naweza kulala na hiyo kelele hainisumbui sana isipokuwa pia hunisaidia nyakati fulani fulani, hilo nitakueleza siku nyingine.
Ndipo siku moja nikiwa nimejilaza hapa kwenye kitanda change cha kamba na hasa kwa vile siku hiyo nilikuwa sijatia kitu kinywani hadi hiyo saa sita ya usiku, nikabaki kuhesabu ‘kenchi’ na misumari na kupata nafasi ya kutafakari na hata kuzilinganisha kero za hapa kwa mama Chau na kero za kelele za wadanganyika walipa kodi kama ambavyo nimekuwa nikishuhudia kwenye kurasa za magazeti. 


Ngoja kwanza! Nani kasema Chokoraa huwa sisomi magazeti!? Mwongo. Huwa sinunui magazeti hasa kwa vile matukio mengi yanayotokea huku mtaani huwa nayaona mwenyewe na sitaki kuyanunua tena yakishatiwa nakshi za wino hasa kwa vile huwa tayari yamechakachuliwa ili kuleta radha ya si hasa, lakini huwa nasoma magazeti na hapa kwangu si ajabu ukakuta magazeti kadha wa kadha  kuanzia yale yaliyofungiwa maandazi, vitumbua, samaki au hata chips dume na kila nipatapo nafasi huwa najisomea hivyo vipande na usiniambie eti siyo magazeti. 


Ndiyo. Nakumbuka Wadanganyika walivyokuwa wamedanganyika na kuhamasika hadi kutaka kuingia barabarani  kuandaa mana ili iliwe na watoto wao baada yao ati kwa vile walichoshwa kula nyama ilhali wakifyatua matofari ya utumwa na hivyo wakajiandaa kuandaa mana. Weeee!!! Koma. Kwani waliandaa mana hata hivyo!? Wapiii!! Walifanya maandalizi yao yoote na matangazo na kila kitu halafu ati kuna jamaa mmoja mwema katika wema wake akagundua kuna mashababi mjini wanataka ati kuwadungua wadanganyika wote watakao andaa mana, basi kwa wema wake akawaonya wadangayika na wao wakanyewa kimyaaa!!  Ama kweli rahisi sana kuwadanganya wadanganyika.


Ni juzi tu wakati nasoma hiki kipande cha gazeti kuhusu hayo maandalizi ya kuandaa mana na jinsi yalivyozimwa kwa wema wa mwema na vijana wake, ndipo nilipogundua kumbe  wadanganyika wengi wanaishi kama milango ya nyumba ya mama Chausiku. Nasema usidhani nakutusi ewe mdanganyika mlipa kodi, lakini nakuuliza, ziko wapi zile hasira ulizokuwa nazo na kampeni kubwa ulizofanya ili kuandaa mana kwa ajiri ya kizazi kijacho baada yako hasa kwa kuzingatia kwamba ikiwa hivyo vijisenti yako uchwara vingelipwa kwa ajiri ya kusafisha hilo “Doa la Nzi” kwenye shati jeusi lenye harufu ya kinyesi, basi vizazi vijavyo vingepata hasira itokanayo na hasara na hata kufikia kuukana udanganyika wao?! Kwani hao mashababi walikuwa wangapi hata nchi nzima inasiamama wima kuwaacha hawa jamaa wapite!? Hata kama walikuwa wengi na waliojisheheneza sira nzitonzito na za maangamizi, walikuwa wapi na walikusudia kukaa muda gani au ndiyo wamehamia na hivyo sasa hatuwezi kufanya lolote kwa sababu kila tutakapojaribu kutoka nje ya milango yetu basi tutapambana na hawa mashababi!!? Nafikiri katika wema wake, huyu nduyu yetu mwema angetwambia basi kwamba hawa mashababi ama wamedibitiwa au wamekwishaondoka na hivyo tuendelee na maandalizi yetu ya kuandaa mana ili kizazi chetu kisifie jangwani kwa ukosefu wa chakula!. Humu mimi simo. 


Nikakumbuka pia kwamba baada ya maandalizi ya mana kushindikana,  waheshimiwa wawili akina Mbu na Nge nao wakaja kwa umoja wao wa Mbu-Nge kutaka nyogeza ya posho na hapa wadanganyika wakakasirika hadi povu kuwatoka midomoni. Nikahisi labda mara hii, wadanganyika hawa hawatadangayika. Wapi!! Kwa mara nyingine wakazidiwa na kile kibinti huwa nakiona kwenye vile visanduku vya picha kikisema kwa sauti kubwa “Sidanganyikiii” maana wandanganyika ghafla wakadanganyika na matukio ya mafuriko na mengineyo na kusahahu kwamba kuna visenti vyao kibao vyaliwa na ule umoja wa “Mbu-Nge”  na wao wakibakia kuwa wadanganyika walipa kodi. 


Mara mlango wa nje wa hapa nyumbani kwa mama chiku ukasukumwa ila mara hii polepole nafikiri kwa vile huyu anayefungua anajua kwamba watu wameanza kulala na hataki kuwasumbua na hivyo japo ulipiga kelele kama kawaida yake, lakini bado nasikia mikoromo ya usingizi ya mama Chiku na vitegemezi vyake ndipi nikakumbuka, kweli kele za mlango, hazimzuii mwenye nyumba kuuchapa.

Mi ninaomba kuuliza, hivi Wadanganyika mnaugua ugonjwa gani huu!!? Nasema usikasirike na wala usininune na hata ukinuna mi nina manati ya ndhungu sikuogopi ng'o! wacha nikuuliza na jibu nalitaka. Kwanza, mlitaka kuandamana ili kushinikiza sirikali isiwalipe "Doa la Nzi" mabilioni ya visenti vyenu vya madafu, mkachapwa mkwara na yule jamaa mwema mwenye kuwatendea wema hata wasio wema akiwaambia ati kulikuwa na tishio la wale mashababi, mkanywea. Hivi hilo tishio halijesha au ndo mmekubali kuliwa enyi 'wapinga kula'!? Nasema yule mwema katika wema wake atwambie kama wale mashababi wamekwishaondoka na kurudi kupamba na Kenya na Amisomi ili Chokoraa niandamane maana bado nataka kuandamana. Hamtaki kuhoji nawauliza wadanganyika mwaumwa ugonjwa gani?!. Wabunge walipojiongezea posho, mkaandika mpaka kwenye bulogu zenu, mkanuna hadi sura kuwavimba na kisha haoooo mkanywea. Nawauliza, hivi juhudi zenu zimefikia wapi ama mmebakia kuwa milango ya bati na bawaba kavu zenye kupiga kelele nyingi hata kwa kuguswa na mende ilhali mkiwaacha wenye nyumba yenye siri kali walele fofofo!!? Simo, nasema simo tena mntioe humu simo kabisaaaaaaaa.

Salaam nakusamilia,  ni mimi nduguyo Chokoraa wa Muhangaikaji ,wa Mlalahoi, wa Pangu Pakavu, wa Kabwela ,wa Mdanganyika.

Tuesday, January 3, 2012

Usalama usio salama wa Barabarani.


Kiherehere hiki!
Leo ati Chokoraa na mimi nimejikusanya na baadhi ya wananzengo hapa mtaani kwetu, tumekazunguka haka kasanduku kanakoonyesha sura za watu wakiongea na sauti zao twazisikia ati ninyi mwaita tivii. Uliza sasa tunaangalia nini! Duh! Nachoka miye mwana wa Muhangakaji kitukuu  wa Kabwela. 

Tumekaa tunaangalia Taarifa na Habari. Wewee!! Nani kasema nimekosea?! Nani!!! Tena!!! Angalia usiniudhi mapema nikazira kukuhadithia hata tukio lenyewe. Kwani ile ni “Taarifa ya Habari, Taarifa za Habari, Taarifa na Habari?!!. Nadhani lile baraza la wanaokifahamu Kiswahili kuliko sisi wengine inabidi watusaidie kwenye hili. 

Ala! Unaona sasa!! Hadi nimesahau nilichotaka kukwambia kwa vile umenitia hasira. Hata hivyo nadhani nimejaribu sana kutumia lugha yenu ya kistaarabu sana ilhali mi siifahamu hiyo lugha yenyewe. Wacha nitwange kichokoraa sasa ndo tuelewane. Simo.

Nasema kwenye hili la kulalamika na kunung’unika kwa kila kitu simo, tena simo hata kidogo, simo kabisaaaaa! Ala! Hivi, si kila mwisho na mwanzo wa mwaka kumekuwapo na lundo la ajari barabarani na nyingi zikisababishwa pamoja na mambo mengine uzembe wa madereva na kukosa ujuzi na sifa stahiki za kuendesha magari!? Kwani kuna mtu kati yetu hajui kwamba hali hii imechangiwa kwa kiasi kikubwa na uzembe wa vyombo vyetu vya ulinzi na usalama hasa wa barabarani yaani  ile mamlaka ya kuzibiti barabara na maji almaarufu kama ‘chuma tule’  na vikosi vya ‘usaha alama za barabarani’ kwa umoja wao? Hilo halinikasirishi hata hivyo.

Linalonikasirisha hadi nimewaandikia waraka huu, ni hili la wadanganyika walipa kodi kujifanya kulaumu “sirikali” kwa kila kinachofanywa hata kama ni kizuri. Hivi si nimeona mkipaza sauti mishipa ya shingo kuwasimama mkilalamikia kukatizwa safari zenu kwa sababu ya zoezi la ukaguzi wa “liseni’ za udereva ili kujua wale walio ‘liseni’ darasani kabla ya kuanza kuendesha na wale ambao wanaendesha bila kuanza ‘kuliseni’!! Nasema kwa hili mnitoe. 

Ona sasa. Yaani wakati watendanaji wa ‘sirikali’ walipojipanga ki ‘stratejiki’ kabisa kwa kuzingatia ‘taimingi’ ya muda ambao ajari zinazidi na kujaribu kuokoa maisha ya wadanganyika, mwalalama! Mwalalama nini enyi wana wa danganyika yetu!? Naapa simo humu.  Ona hyu naye anachukia ati kwa vile nachanganya kikoloni katikati ya sentensi zangu. Utajuaje kwamba “Nshomile mpaka fomu fooo!!!” Kalagabaho kama hujaelewa, kwani hilo mi Chokoraa lanihusu!? Simo nasema.

Nasema kwenye hili, badala ya hasira zangu kuzielekeza kwa hawa wana usalama japo si salama, ningezielekeza kwa wamiliki wa haya madude yaliyofanyika wajumbe wa malaika mtoa roho kila mwanzoni mwa kila mwaka. Washangaa nini!! Ningezielekeza hasira zangu kwao kwa vile kila mwajiri anapomwajiri dereva anamuuliza kuhusu leseni na ikiwa mwenye gari anaruhusu dereva asiye na leseni kuendesha gari lake, mwataka nisimwelekezee hasira zangu kwa nini!!? Naapa kwa hili tutashindana sana, lakini simo.

Halafu!! Ebu niwaulize enyi wana wa usalama japo si salama, huu utaratibu wenu wa kuvamia tu maeneno na kuanza kutekeleza majukumu yenu bila hata kuzingatia kwamba Chokoraa miye mwana wa Muhangaikaji, naam, mimi huyu mjukuu wa Mlalahoi kilembwe wa Kabwela, mara nyingine ninatoka nyumbani na tiketi tu na ziada ya shilingi elfu mbili kwa ajiri ya maji na nauli ya ‘bodaboda’ nikifika huko niendako na hayo mengine namuachia maulana, mmeianza lini!?

Naapa kwa ubabe huu sina hakika kama mnafanya ‘upolisi jamii’ kwa sababu mnashindwa kuzingatia mahitaji ya jamii yenyewe katika utekelezaji wa majumu yenu kwa sababu hasa mahitaji ya Chokoraa miye hayaishii kwenye kusafiri na kufika salama bali pia kuzingatia matumizi ya kila ‘shekeli’ (iite ‘sinyingi’ kama hilo ndilo jina ulipendalo) ninayoitumia na ninavyoitumia wakati wa safari na ndiyo maana japo naona kama lengo lilikuwa zuri lakini kwenye utekezaji wake simo, tena simo kabisaaa!.

Nasema iweni na huruma na maisha ya sisi wajukuu wa Pangu Pakavu kwa sababu kila mara tumekuwa tukisema tieni mchuzi lakini hamtaki, naapa simo. Hivi mnadhani wale wadogo zangu akina Mzembe na Mzururaji ambao walikuwa wameng’ng’ana kuishi mjini humu kwa kuningezea shughuli ya kuwalinda na kuwahudumia mimi kaka yao Mkubwa, tajiri wa ukoo kwa kipato cha kunanga, Chokoraa wa Kabwela, na sasa walikuwa wameamua kurudi kijijini, si wamehairisha baada ya magari kuchelewa kuondoka na wamerudi  kwenye lile pagala tunakojikusanya usiku na kujirundika tukipitiwa na usingizi ilhali tukiita huko ni kulala!?. Nasema hamjui ni kiasi gani ya gharama na maumivu ya moyo mmeniongezea mwaka huu na ndiyo kwanza unaanza. Naapa mpaka umelizike, tutaonana wabaya. Simo. 

Na nyie ‘chuma tule’ hivi kweli na akili zenu zoote  mmeshindwa kutengeneza ‘mpango mkakati’ (naogopa kusema ‘sitrateji’ msijesema napenda sana kikoloni) wa jinsi ya kukagua walio ‘liseni’ na kuwa lessen wale wasio nazo bila kunisumbua miye Mdanganyika Mlipa kodi!!? Naapa utaalamu umesafiri kwenye inchi ya wadanganyika walipa kodi. Simo, tena simo kabisaa.

Haya, tekelezeni majukumu yenu na wala msijesema mimi nawakataza kutekeleza majukumu yenu maana nafahamu mnayo sheria ya kuitumia kuniyamazisha miye hati kwa vile nimekuwa domo kaya wakati huyo ni mpwa wangu mimi jina langu ni lile lile le siku zote, Chokoraa wa Mdanganyika wa Muhangaikaji wa Mlalahoi wa Pangu pakavu wa Kabwela.

Haha ha ha ha ha ha ha! Nicheke niongeze siku miye.

Salaam nawasalimia, 

Chokoraa wa Muhangaikaji.