Wednesday, July 10, 2013

Mwala magengeni mwezi huu; Vyungu vya nini!?





Nasema mapema kwa hili wana wa Danganyika hii mmenikera na ndiyo sababu miye sitaki kuhusika maana simo tena simo kabisaaaaa. Ala! Kwani  si mwezi  mtukufu wa ramadhani si umeingia na ati siku moja kabla ya mwezi kuanza wengi wenu mlikuwa na sherehe ya kuvunja vyungu kwa vile kwa mwezi mzima hamtakula!?. Naapa mwamtania Mungu enyi wana. 

Naapa kwa jina la Babu yangu mzee Mlalahoi wa Pangupakavu wa Kabwela wa Mdanganyika, nyie mwamtania Mungu. Nasema mmemgeuza Mungu kuwa babu yenu na miye humo msinihusishe. Ala! Si nimeshuhudia mwenyewe ambavyo jana wengi wenu hamkuwamo majumbani kwenu na hata mmedhulumu haki za 'ndoo' za wenzi wenu kwa kuvunja vyungu vyote ati kwa vile mwezi huu hampiki ila mwala magengeni na sasa vungu vya nini!? Naapa laana mmelaaniwa enyi wana na miye humo simo. Sitaki, tena nasema sitaki kuwashawishi mkubaliane na mimi katika kila nisemacho lakini ni kweli kwamba ama hizi dini zimekuwa kwenu kama kongwa la utumwa ni vyema mungelizivua mkatembea huru katika uhuru wa mwendawazimu kuliko huu wazimu wa usiku muufanyao naapa mmenikera enyi wana. Na sasa najiuliza wakati ninapowatakia wale wenye nia safi Ramadhani karim, nyie wengine ambao jana mmefanya kufuru ya kuvunja vyungu vyetu niwaambieje? Poleni na starehe?. Simo.

Nasema kwa kitendo chenu hiki nashindwa kujua niwaiteje maana kuwaita wafuasi wa dini itakuwa kuikosea adabu dini yenyewe maana ikiwa hao mitume walioleta kwenu dini hiizi wangefufuka leo, bila shaka na ongezeko hili la magonjwa yasiyokuwapo enzi zao wangekufa mara ya pili mara hii kwa magonjwa ya moyo kama si sononi na humu najitoa maana simo.

Haya, wacheni nijiropokee maana humu ndani naweza kuropoka tu bila hofu kwa vile mimi ni Mdanganyika tena mlipakodi na ninafahamu nyie wenye kuvunja vyungu vyetu ili wote tushinde njaa kama ninyi hamna mahusiano ya karibu na wale wasiojulikana na hivyo sikuogopeni katu. Nasema nyie si wafungaji ni washinda njaa na mwaiongoezea kaya yetu mzigo wa kuuguza wagonjwa wa vidonda vya tumbo na magonjwa yake kwa kujisindisha njaa ilhali nafsi zenu zili dhalili na humu mnitoe. 

Ala! Kwani hayakuwatosheni maovu ya mwaka mzima hadi mlipoamua kufanya kufuru za mwaka mzima “ini advansi” kwa vile funga imekurubia?. Ha ha ha ha ha ha ha!!!! Najiuliza wadanganyika nyie mwajidanganya na nini kuwaza kwamba huyu Mungu anawaza kama muwazavyo ninyi na hivyo atawaosheni na maovu yenu ya makusudi muyatendayo kwa kujikinahi!?. Hayo nakuachieni nyinyi maana hata mimi ni muovu mwana wa uovu na yamkini hata mimba yangu ilitungwa hatiani lakini kwa hili msijifananishe name maana simo.
Nasema mimi na ninyi hatufanani kwa sababu binafsi najifahamu kwamba sihitaji kujishindisha njaa kwa sheria tu ilhali nikiwa muovu na hivyo wakati wenzangu jana mmevunja vyungu vyote mtaani, mimi nimenunua magudulia ya chuma nasonga ugali nile nishibe ili nikuchekeni nyie wenye kujivisha ngozi za kondoo ilhali ndani ni mbwa mwitu wakali. 

Hivi, nyie si ndiyo wale mliohusiwa juu ya vita vilivyo bora zaidi  yaani vita vya kuishinda nafsi!? Mbona sasa mmekuwa watumwa wa nafsi zenu wakati ingekuwa rahisi kwenu kula mkashiba mkafanya kazi na kuongeza uchumi wa jamii zenu huku mkiwa na afya njema na nafsi safi bila kulazimika kuwa wanafiki!? Naapa huu wa wavunja vyungu ni unafiki tena unafiki mtupu!. 

Kasirikeni mkasirikavyo lakini jueni kwamba mwana wa muhangaikaji kwa hili mmenikera lakini sina hasira sana kama nilivyo na huruma. Ninawahurumia na ndiyo sababu ya kukuandikieni waraka huu ili mwenye masikio ya kupona asikie hizi dawa lakini ikiwa ni wa kufa basi ziba masikio kwa hasira na visingizio. Ndiyo, najua mtaleta visingizio kwamba ati Chokoraa miye nimeitusi dini nasema huo utakuwa ni unafiki wa radaja la pili maana miye siitusi dini ila nawauliza wenye kujifanya mwaifuata dini kana kwamba kwa shuruti huku mkifanya kufuru, mmejihoji ni wangapi kati yenu mliokumbuka kula pipi zenu kwenye maganda ama huko nako mlivunja vyungu!? Naapa ikiwa na hilo nalo mlilivunjia vyungu, basi jiulizeni ni wangapi kati yenu mlioambukizwa kale kaungonjwa na mnaojiandaa kunilaumu Chokoraa nikikataa kuja kuwaona mlazwapo hospitali na wengine kusema nawanyanyapaa!? Kwa hili naapa niiteni mnyanyapaa lakini hata kwa Mungu sina hatia ikiwa nitawanyanyapaa kwa kujisulubisha wakati wa kuvunja vyungu maana kuna tofauti ya makusudi na bahati mbaya msiolijua hilo jilaumuni wenyewe na humu simo.

Haya, na wale ambao mliwatoroka wazazi wenu na kwenda kwa vibwana vyenu huku mkidhani mwawafurahisha kumbe mwajitafutia majukumu ya ulezi msiyoyaweza bado na mwisho wa siku mwataka jamii ibebe mzigo wa kunilea Chokoraa miye na wadogo zangu akina mzembe na mzururaji!? Hivi na hili nalo linahitaji “sirikali” kukupeni onyo mapema?. 

Komeni. Nasema komeni hasa nyie mjiitao “wana haraka tu” kuipigia kele ‘siri kali’ ati kwa kutofanya chochote kuwasaidia ‘watoto wa mitaani’. Nasema mkome. Ndiyo, najua wengine ni rafiki zangu lakini nisikilizeni maana kwa hili siropoki nasema hakuna mtoto wa mtaani maana kila mtoto ana baba na mama yake na ni lazima wawajibike wao kwanza kuondoa watoto wao mitaani na ndipo sisi wengine tutafuata!?. Ala! Mwataka tu nyie mfanye fujo zenu na kuvunja vyungu vyetu bila mipango wala mikakati ya kukabiliana na matokeo ya uvunjaji vyungu huo kisha siye tuwajibike!? Nani kasema!?. Simo humu namo. 

Ha ha ha ha ha ha!!! Hongera zenu wajasiria mlo maana nina hakika kwa siku ya jana nyie jana mlikuwa na “ugeni” mkubwa na hata wengine walilala sebleni na hata wako waliopitisha muda wao kwenye maliwato na huko kote wakivunja vyungu. Kwani viliwakosea nini?. Ama kosa la vyungu hivi ni kuwapikieni mwaka mzima na sasa kwa vile mwezi huu mwabadili ratiba ya kula basi vyungu havina thamani tena?. Nasema nyie mliovunja vyungu jana hamjafunga hata kidogo. Mmebadili tu muda wa kula kwa kuacha kula mchana mzima huku mkifakamia milo yote usiku maana kufunga huanzia kwenye nafsi na nyie nafsi zenu mmeziuza kwenye kuvunja vyungu. 

Haya, najua wako wale ambao kwa nia ya kweli ujio wa ramadhani umewakuta wamejiandaa nafsi zao kwa ajiri ya muumba wao. Kwenu nyie salamu zangu ni chache tu. Muombeni huyo Mwenye Enzi yote aliyevifanya vyote atufanyie wepesi hasa kwenye kaya yetu hii itafunwayo kila siku na dini huku wote tukifanya juhudi kumtafuta Mungu huyo huyo. Kwenu nyie nasema ‘kun faya kun’ mnisamehe ikiwa neno hili limekosewa lakini ikiwa yeye mwenye kusema kuwa likawa angetaka wote tuwe dini moja isingeshindikana na hivyo muombeni aturudishie mioyo ya subira tujue kuvumiliana na kuchukuliana katika kutofautiana kumwamini kwentu maana Mungu ni mmoja tu hajakuwako mwingine kabla wala baada yake hatakuwako mwingine sasa sisi twagombea nini? Twagombea mapokeo yaliyoletwa na wale walioleta tena kwa maslahi yao binafsi wakituchonganisha ili watuibie? Naapa huo nao ni uduni wetu wa kufikiri na humo miye simo.
Tuombeeni. Wala smituombee atujaze mapesa mifukoni maana amani na furaha ya kweli haitokani na kuwa na mifedha kedekede lakini atujaalie akili njema na uwezo wa kuziona na kuzitumia fursa kujitendea na kuwatendea wengine mema. Tuombeeni atujaalie kujua kwamba yaliyowekwa wazi ni yetu na watoto wetu ili tuyatende nay ale yaliyofichwa ni yak wake ili tumche na kumwabudu na siri ya kwanini Chokoraa namwamini hivi na wewe waamini vile si yetu ni yake tuache kuyachokonoa yasiyo yetu. 

Mwisho niombeeni na mimi ndugu yenu Chokoraa mwana wa Muhangaikaji walau nitengeneze mkate hata kama ni wa unga wa mahindi badala ya kuokoteza kila siku maana akina kaka muishiwa hawataki kunitupia tena vipande vikubwa wanasema nikishiba sana nawapigia kele na hivyo nile kidogo ili nguvu zinipungue wanitawale. 

Ni mimi ndugu yenu, Chokoraa wa Muhangaikaji wa Mlalahoi wa Pangupakavu wa Kabwela wa Mdanganyika nawasalimu. Ramadhani Karim.Salaam nawasalimia.

No comments:

Post a Comment