Wednesday, October 9, 2013

Wana Haraka tu!!!!!!!!

Salaam nawasalimia. Karibuni kwenye kilinge cha Chokoraa enyi Wadanganyika wana wa Mlipakodi mnisikize kaka yenu Chokoraa mwana wa Muhangaikaji, maana niyaonayo miye huku majalalani yatosha kunitia fahamu na kutaka salam kuwatumieni, Salaam wadanganyika. 

Ukiamka asubuhi huku tumbo lakusumbua, usikimbilie kupiga ramli ama kufakamia kikombe cha babu bali tafakari ulichokula jana yake na hiyo ndiyo busara enyi wana, salaam ndugu yenu Chokoraa wa Muhangaikaji wa Mlalahoi wa Pangupakavu wa Kabwela wa Mdanganyika Mlipakodi nawasalimia.
Ati!. Wakataa nini? Kwamba wewe si Mdanganyika ama si mwana wa Mlipakodi!?. Ha ha ha ha ha!!! Nicheke miye kitukuu wa Kabwela maana nijuavyo Wadanganyika nyie sasa mwahoji hata asili ya mzazi wa mzee Utaifa wa Uzalendo wa Uadilifu na miye humu nahusikaje!?. Ndiyo, kwani siku hizi si Wadanganyika wote wamekuwa ‘wana haraka tu’?.  

Nani alinidanganya nikadanganyika Chokoraa miye kwamba harakaharaka haina Baraka maana siku hizi ati mwauthamini zaidi msemo ule kwamba ngojangoja yaumiza matumbo pasina kutafakari kwamba ‘haraka tu’ zenu za kula hata visivyoliwa na wazee wenu kabla yenu, ndiyo sababu ya matumbo yenu kukusoketeni na wala si subira yenye kuvuta heri iliyo chanzo cha mgogoro wa matumbo yenu!?. Naapa humu miye msinhusishe maana simo. 

Siku hizi ati kila Mdanganyika ni ‘mwana haraka tu’ na miye nauliza, hizi haraka zenu zakupelekeni wapi enyi wana mbona mwanishangaza!. Nasema mapema ili yatokeapo msijenihusisha mchakuraji miye maana miye yangu majalala huku nikichakurachakura nione ikiwa nitapata kipande cha boflo nipooze njaa ya tumbo langu. 

Ama kweli kusoma kwingi si kujua mengi bali maisha ndiyo kipimo cha akili kama walivyosema wale waliokuwa kabla yangu miye mwana wa Muhangaikaji. Najiuliza hivi mbona kila siku kwaibuka ‘wana haraka tu’ na mbona wote waibuka kunifunda kudai haki na hakuna kati yenu awekezaye muda walau kiduchu kunifunza wajibu!?. Nani alikudanganyeni kwamba haki huja bila wajibu wenyi wana mbona mwapotea njia mchana kweupe kwa uzembe wa kuuliza?. 

Haki ya mtoto, haki ya mwanamke, haki ya kichaa, haki ya mlevi, haki…. na miye nakuulizeni haki zenye kuja bila wajibu mwayajua madhala yake nyie?. Ha ha ha ha ha!!! Oneni sasa mnavyolalama kwamba ati Yule mzee wa siku nyingi wa kaya yetu almaarufu Maadili ya Mdanganyika yu taabuni kama si taabani. Mwalalama nini ikiwa mmeshindwa kujua kwamba hamuwezi kuendelea kumlisha mzee huyu sumu iliyomuua Maadili ya Wageni na mkataraji ati kwa vile huyu na yule wafanana majina tu lakini si ndugu basi sumu itageuka kuwa dawa kwenu!?.  Simo nasema. 

Nasema ijapo mtasema wajuaje weye tofauti ya uchafu na chakula bora ama dawa na sumu kali ilhali wala majalalani na kulala mitaroni lakini nasema hekima si kama pesa kwamba ukiwa nayo yakutia kiburi na dharau na maneno ya mwenye hekima ni bora ijapokuwa hekima ya maskini haithaminiwi na hata maneno yake hayasikizwi na ndiposa nawasalimu, shikamooni Wadanganyika. 

Haya, nakumbuka wakati wa kukua kwa wadogo zangu wale akina Mzembe na Mzururaji na hata mimi kaka yao Chokoraa wa Muhangaikaji, fimbo ilikuwa ufunguo uliiondoa ujinga kichwani mwa mtoto lakini sasa mwasema ni haki ya mtoto kutopigwa bali ipigwe ngoma na miye nakuungeni mikono na miguu yote, lakini wacheni kulalama basi ikiwa heshima ya juzi na jana zina tofauti maana hiyo ni haki ya mwendawazimu peke yake. Ala! Kwani si haki ilipaswa kuja na wajibu!?. Nasema ikiwa mwanifunda tu juu ya haki yangu na kudhani wajibu wangu nitaufahamu ikiwa tu nitapewa haki yangu, jiandaeni basi kwa madhila ya kizazi cha nipe nipe maana ndivyo mtakavyo na miye humu nahusikaje!?.  
Ati! Wengine mnalalama ni kwanini kila mkirejea majumbani mwenu mwakuta ‘ndoo’ zimevunjika na sasa vijana hamzitaki hata ‘ndoo’ zenyewe badala yake mwanunua mabeseni ya karatasi ambayo mkiishaogea mwayatupa huko huko maliwatoni!?. Mwalalama nini!?. Kwani mlipoamua kutangaza haki na usawa kati ya jinsi zenu bila hata kufafanua yale yapasayo kuwa sawa na yale yasiyopasa na badala yake mmeifanya jamii yote kuwa na watu wenye maumbile ya Adamu na Hawa lakini wenye kufikiri kama Adamu tu mlidhani madhara yake nini!?. Nasema chakula cha fahamu ni maneno na mifano na kile wanachokisikia wanenu na kukuoneni nyie mkitenda ndicho watakachotenda na wao kwa juhudi kubwa kuliko watangulizi wao na miye humu mnitoe maana simo. 

Wacha nikomee hapa hadi tutakapokutana juma lijalo kwenye kijiwe hiki, wacha nijaribu kumeza vipande vya boflo hivi na maji ya chumvi ila salaam zangu zikufikieni enyi Wadanganyika.
Wasalaam, ni mimi ndugu yenu Chokoraa wa Muhangaikaji wa Mlalahoi wa Pangupakavu wa Kabwela wa Mdanganyika, nawasalimia. Shikamooni Wadanganyika.

No comments:

Post a Comment