Rafiki yangu kipenzi Udadisi Chautundu
Nimepata barua yako rafiki yangu kipenzi tuliyekua pamoja na kucheza pamoja “kidaso” yaani naona hata aibu kukuita rafiki maana wewe ni ndugu yangu. Umenilaumu kweli kwenye barua yako kwamba ndugu yako nimekusahau na hata jina lako huna hakika kama ningali nikilikumbuka, lakini nakuhakikishia hata ningeamshwa usingizini ghafla na kutakiwa nimtaje rafiki yangu wa karibu, ningekutaja wewe kwanza kaka yangu Udadisi Chautundu. Hata hivyo ni siku nyingi kweli tangu tulipoonana na nimegundua baada ya kusoma barua yako, kwamba kuna mambo mengi uliyoyasahau kuhusu mimi na kuna mengi pia yametokea ambayo hujayajua na inawezekana kama ungekuja mjini kunitafuta basi bila shaka ungenikosa.
Nakupongeza hata hivyo ulivyoamua kubaki kijijini. Ndiyo, nakupongeza kwa sababu huku mjini kuna watu wana roho mbaya sana kiasi ningekuwa sina tetesi kuhusu wazazi wao, basi nisingesita kukwambia hawa si binadamu na hawakuzaliwa lakini kwa bahati kuna tetesi nyingi kuhusu wazazi wao. Kuna huyu Maisha Magumu. Huyu jamaa unapoingia tu mjini ndiye wa kwanza unayekutana naye na nakwambia huyu jamaa ni maarufu humu mjini kuliko hata ‘mkulu wa kaya’ yetu na kila siku umaarufu wake unaongezeka.
Ha ha ha ha!! Unaona sasa, umeanza kumfananisha huyu jamaa na yule mzee pale kijijini ambaye wewe rafikiri yangu Udadisi ulinifanya kila siku nifikirie maana ya jina lake bila majibu mpaka nilipokuja huku mjini. Si yule mzee alikuwa na koti lefu jeusi na kofia ambayo japo hatukujua aliifua saa ngapi lakini haikuwa ikionekana chafu kila alipoivaa!! Usijifanye umemsahau bwana, mzee Malingumu wa Maliyatabu.
Huyu maisha magumu wala hana uhusiano na hao wawili. Yeye huyu hajulikani vizuri hasa nasaba yake maana wako wanaosema anatoka kwenye ukoo wa yule mzee mwenye kitambi mheshimiwa Kiongozi Mrafi na eti ni mtoto wa mke mkubwa wa huyu mzee Bi Rushwa wa Mlungula.
Wangine wanasema hapana, Mheshimiwa Kiongozi Mrafi anasaidia tu kumlea huyu mtoto kwa sababu wakati anamuoa mke wake Bi Rishwa wa Mlungula, Bi Rushwa alikuja na huyu mtoto kutoka kwenye ndoa yake ya kwanza kwa yule mzee kiburi sana hapa mjini Bw. Ubadhirifu wa Maliyauma. Vyovyote iwavyo, huyu jamaa amejifunza vyema kwa mama yake maana tabia zake mnh! Nitakueleza siku nyingine, leo nataka tu kujibu barua yako.
Kwanza nikuhakikishie kwamba sijakusahau ndugu yangu na unapoona sikuandikii hata barua, ni kwa sababu ndugu yako siku hizi naishi kwenye kitongoji kimoja hapa mjini ambacho ni maarufu kwa kuwa na shughuli nyingi wenyewe wanaita “bize”. Basi mwenzako nashinda bize tangu asubihi hadi jioni na kila uzingizi ukinizidia ‘naangusha gari’ hapo hapo ninapokuwa na nikaimka naendeleza libeneke. Lakini pia yule mdogo wangu Uzembe naye anachangia hii hali ya mimi kutokukuandikia barua, lakini usijari kwa sababu sasa hivi mimi na uzembe tuna ugomvi tena mkubwa, basi nadhani kwa muda mrefu kidogo ataniacha peke yangu na hivyo nitapata nafasi ya kukuandikia kila mara.
Unashangaa tuna ugmvo gani!!? Si ndo hayo sasa ninayokwambia ndugu yangu kwamba siku hizi kuna mambo mengi yamenitokea na wewe huyajui!! Hata! Wala sikulaumu. Najua unanipenda sana na ungependa kujua kila kinachonipata swahiba wako Chokoraa wa Muhangaikaji, lakini mara nyingine huwa nalazimika kukuficha mengine maana najua yatakuumiza hasa kwa vile wewe ulivyo Mdadisi kama jina lako, najua utaumia sana moyo ndiyo maana huwa mengine namezea.
Haya basi, kwa vile umelazimisha, wacha nikwambia tuna ugomvi gani na Uzembe halafu hayo mengine nitakuandikia waraka ujao. Ilikuwa usiku kamaa saa tatu na nusu hivi na tulikuwa watatu tunatokea kwenye soko la “bize” kurejea ‘gheto’ kwa ajiri ya kupumzisha mbavu zetu. Basi bwana, mara ghafla tukakutana na watumishi wa ‘siri kali’ wenye jukumu la kulinda amani. Mimi soga zilikuwa zimenikolea mwenyewe hata sikuwaona hadi walipokuwa wameshatufikia karibu, kutahamaki, Uzembe na Uzururaji wakatimua mbio na kuniwacha peke yangu. Kwanza sikufahamu kwa nini walikimbia, lakini kama unijuavyo ndugu yako Chokoraa huwa sina hofu na walinzi wa mheshimiwa Dola.
Nikasimama kwa ujasiri kabisa tena kwa kujiamini si ninajua sina matatizo mimi na mwenyekiti wetu Mheshimiwa Dola! Wapi!! Nakwambia yaani hawa walinzi hata kabla hatujasilimiana nikasikia mmoja ambaye nadhani alikuwa kubwa wao akisema kwa sauti ya ukali na ya kushutumu “Hivi hili si ndiyo linaitwa Chokoraa litoto na yule mzee marehemu Mhangaikaji?”. Akajibiwa “Ndiyo” hata sikujua ni nani aliyejibu maana tayari alishaanza kunitandika makofi huku akinipa amri mfululizo “kaa chini kachini…mikono juu.. una nini mfukoni we Chokoraaa?... huna majani mfukoni kweli wewe….?”.
Sikujua hata nijibu swali lipi kwanza na sikujua hata kosa langu, mara nikawasikia wakizungumza maneno fulani kwenye vilongalonga vyao na lugha yenyewe hata sikuifahamu ila nahisi kitakuwa ni kigagagigikoko maana sikuambulia hata sentensi moja, mara gari hilo likaja limejisheheneza walinzi wengine na hata mmoja wao akiwa amebeba ‘manati ya ndhungu’. Niliogopa nilipoiona hiyo manati wewe!!! Asikudanganye mtu ndugu yangu, manati ya ndhungu inatisha ikiwa kwenye mikono ya watu wenye hasira kama hawa walinzi wa dola. Basi bwana, nikapakiwa kwenye gari tena kwa kusukumizwa kama mzigo hadi kwenye kituo kikuu cha hawa walinzi, hapa napo nikapokelewa na maneno kadhaa ya kejeli “Mmelitoa wapi hili Chokoraa!!?” mmoja wao akauliza huku akinikwida na kunizungusha nyuma ya meza kuuubwa ajabu! Mwingine akadakia, “kwani ni Chokoraa au Jambazi kabisa hili?”.
Ala! Sasa hasira zangu zikanipanda na povu likaanza kunitoka mdomoni. Yaani wananifananisha na yule adui yangu mkubwa ambaye ndiye aliyemuua baba yangu marehemu Muhangaikaji? Nimekuwa nikimtafuta huyu jamaa na hata walinzi wa Dola waliniahidi kwamba wangemtia mbaroni sasa ni mwaka sijui wa ngapi hajapatikana na nasikia anaishi mjini humu humu tena rafiki zake wengine wanajulikana na ati ndiyo sababu ameshindikana kukamatika, leo hawa wananifananisha naye! Haiwezekani.
Nikafumbua kinywa hivyo hivyo na mapovu mdomoni. “Mimi siyo jambazi, mimi ni Chokoraa wa Muhangaikaji. Hata mimi namtafuta huyu Jambazi kwa sababu alimuua baba yangu miaka kadhaa iliyopita…” hata sikumaliza, sori ya kiatu ikatua mgongoni na kunituliza chini, nikaona ili kuokoa uhai wangu bora nikae kimya hadi nitakapofika kuonana na liwali kesho maana hawa jamaa hata hawatakki kunisikiliza. Itaendelea
No comments:
Post a Comment