Wednesday, October 9, 2013

Wana Haraka tu!!!!!!!!

Salaam nawasalimia. Karibuni kwenye kilinge cha Chokoraa enyi Wadanganyika wana wa Mlipakodi mnisikize kaka yenu Chokoraa mwana wa Muhangaikaji, maana niyaonayo miye huku majalalani yatosha kunitia fahamu na kutaka salam kuwatumieni, Salaam wadanganyika. 

Ukiamka asubuhi huku tumbo lakusumbua, usikimbilie kupiga ramli ama kufakamia kikombe cha babu bali tafakari ulichokula jana yake na hiyo ndiyo busara enyi wana, salaam ndugu yenu Chokoraa wa Muhangaikaji wa Mlalahoi wa Pangupakavu wa Kabwela wa Mdanganyika Mlipakodi nawasalimia.
Ati!. Wakataa nini? Kwamba wewe si Mdanganyika ama si mwana wa Mlipakodi!?. Ha ha ha ha ha!!! Nicheke miye kitukuu wa Kabwela maana nijuavyo Wadanganyika nyie sasa mwahoji hata asili ya mzazi wa mzee Utaifa wa Uzalendo wa Uadilifu na miye humu nahusikaje!?. Ndiyo, kwani siku hizi si Wadanganyika wote wamekuwa ‘wana haraka tu’?.  

Nani alinidanganya nikadanganyika Chokoraa miye kwamba harakaharaka haina Baraka maana siku hizi ati mwauthamini zaidi msemo ule kwamba ngojangoja yaumiza matumbo pasina kutafakari kwamba ‘haraka tu’ zenu za kula hata visivyoliwa na wazee wenu kabla yenu, ndiyo sababu ya matumbo yenu kukusoketeni na wala si subira yenye kuvuta heri iliyo chanzo cha mgogoro wa matumbo yenu!?. Naapa humu miye msinhusishe maana simo. 

Siku hizi ati kila Mdanganyika ni ‘mwana haraka tu’ na miye nauliza, hizi haraka zenu zakupelekeni wapi enyi wana mbona mwanishangaza!. Nasema mapema ili yatokeapo msijenihusisha mchakuraji miye maana miye yangu majalala huku nikichakurachakura nione ikiwa nitapata kipande cha boflo nipooze njaa ya tumbo langu. 

Ama kweli kusoma kwingi si kujua mengi bali maisha ndiyo kipimo cha akili kama walivyosema wale waliokuwa kabla yangu miye mwana wa Muhangaikaji. Najiuliza hivi mbona kila siku kwaibuka ‘wana haraka tu’ na mbona wote waibuka kunifunda kudai haki na hakuna kati yenu awekezaye muda walau kiduchu kunifunza wajibu!?. Nani alikudanganyeni kwamba haki huja bila wajibu wenyi wana mbona mwapotea njia mchana kweupe kwa uzembe wa kuuliza?. 

Haki ya mtoto, haki ya mwanamke, haki ya kichaa, haki ya mlevi, haki…. na miye nakuulizeni haki zenye kuja bila wajibu mwayajua madhala yake nyie?. Ha ha ha ha ha!!! Oneni sasa mnavyolalama kwamba ati Yule mzee wa siku nyingi wa kaya yetu almaarufu Maadili ya Mdanganyika yu taabuni kama si taabani. Mwalalama nini ikiwa mmeshindwa kujua kwamba hamuwezi kuendelea kumlisha mzee huyu sumu iliyomuua Maadili ya Wageni na mkataraji ati kwa vile huyu na yule wafanana majina tu lakini si ndugu basi sumu itageuka kuwa dawa kwenu!?.  Simo nasema. 

Nasema ijapo mtasema wajuaje weye tofauti ya uchafu na chakula bora ama dawa na sumu kali ilhali wala majalalani na kulala mitaroni lakini nasema hekima si kama pesa kwamba ukiwa nayo yakutia kiburi na dharau na maneno ya mwenye hekima ni bora ijapokuwa hekima ya maskini haithaminiwi na hata maneno yake hayasikizwi na ndiposa nawasalimu, shikamooni Wadanganyika. 

Haya, nakumbuka wakati wa kukua kwa wadogo zangu wale akina Mzembe na Mzururaji na hata mimi kaka yao Chokoraa wa Muhangaikaji, fimbo ilikuwa ufunguo uliiondoa ujinga kichwani mwa mtoto lakini sasa mwasema ni haki ya mtoto kutopigwa bali ipigwe ngoma na miye nakuungeni mikono na miguu yote, lakini wacheni kulalama basi ikiwa heshima ya juzi na jana zina tofauti maana hiyo ni haki ya mwendawazimu peke yake. Ala! Kwani si haki ilipaswa kuja na wajibu!?. Nasema ikiwa mwanifunda tu juu ya haki yangu na kudhani wajibu wangu nitaufahamu ikiwa tu nitapewa haki yangu, jiandaeni basi kwa madhila ya kizazi cha nipe nipe maana ndivyo mtakavyo na miye humu nahusikaje!?.  
Ati! Wengine mnalalama ni kwanini kila mkirejea majumbani mwenu mwakuta ‘ndoo’ zimevunjika na sasa vijana hamzitaki hata ‘ndoo’ zenyewe badala yake mwanunua mabeseni ya karatasi ambayo mkiishaogea mwayatupa huko huko maliwatoni!?. Mwalalama nini!?. Kwani mlipoamua kutangaza haki na usawa kati ya jinsi zenu bila hata kufafanua yale yapasayo kuwa sawa na yale yasiyopasa na badala yake mmeifanya jamii yote kuwa na watu wenye maumbile ya Adamu na Hawa lakini wenye kufikiri kama Adamu tu mlidhani madhara yake nini!?. Nasema chakula cha fahamu ni maneno na mifano na kile wanachokisikia wanenu na kukuoneni nyie mkitenda ndicho watakachotenda na wao kwa juhudi kubwa kuliko watangulizi wao na miye humu mnitoe maana simo. 

Wacha nikomee hapa hadi tutakapokutana juma lijalo kwenye kijiwe hiki, wacha nijaribu kumeza vipande vya boflo hivi na maji ya chumvi ila salaam zangu zikufikieni enyi Wadanganyika.
Wasalaam, ni mimi ndugu yenu Chokoraa wa Muhangaikaji wa Mlalahoi wa Pangupakavu wa Kabwela wa Mdanganyika, nawasalimia. Shikamooni Wadanganyika.

Tuesday, September 3, 2013

Salaam Mkulu wa Sungu Sungu.



Nimepata ujumbe  unasema nijihadhari na haya ‘matakataka’ yangu niyamwagayo  kwenye milango ya majumba ya ‘waishiwa’ maana ati yanatoa harufu mbaya yenye kuwakela waishipo kwenye mahekalu yao hayo ambayo ati nayo wameyapata si kwa halali. Nimekusikia ndugu yangu  na ndiyo maana sijathubutu kwa karibu majuma kadhaa sasa kupita mitaani kwao ila leo nimelazimika kuja kumsalimu mkulu wa sungusungu wa kijiji, mkulu salaam nakusalimia, shikamoo mkulu wa sungusungu. 

Wanasema ati wewe umetumia muda wako mwingi tangu ulipotoka pale kwenye jando la kijiji lililoko Mlimani, ukiwa nje ya kaya yetu  hii ati tena ukifanya kazi na wale wenye rangi nyeupe na kutudanganya siye kwa tabasamu na hivyo mkulu wa kaya alipokuteua wewe kuwa mshika “manati za ndhungu” mkuu wa kitengo hiki cha sungu sungu, Wadanganyika walipakodi walikuwa na matumaini makubwa na wewe lakini ati kwa kadri siku zilivyokwenda sasa Wadanganyika hawa hawa wanawaogopa vijana wako kiasi wewe hawakuogopi bali wanakuabudu na humo miye simo maana nimekuja tu kukusalimu, shikamoo mkulu wa sungusungu. 

Ndiyo nasema na wewe mtoto wa mtu Mwema ambaye kwa wema wake alikutuma wewe kwenye jando la kijiji ili ukiisha kuyapata mafunzo ya jando  uje tena hapa kwenye kaya yetu utusaidie sisi watoto wa mzee Mdanganyika Mlipa kodi na ati vile visenti vilivyokupeleka wewe jandoni vilikopwa kwa baba yetu mzee Mdanganyika  wa Mlipa kodi na ndiyo maana miye nakusalimu, shikamoo mkulu wa sungusungu. 

Ngoja! Nielewe na uniamini  ewe mwana maana sina dhihaka hata kidogo nisemapo “niko chini ya miguu yako” kwa vile ni kweli unanikanyaga na wala siwezi hata kujaribu kujiinua maana ni bora unikanyage wewe kuliko nidunguliwe na ‘manati’ za vitegemezi vyako na humo miye unitoe maana simo. 

Kinachonitisha miye si kule kujua kwamba hata salaam hizi zaweza ama kupelekea miye kudunguliwa na manati za ndhungu zilizo mikononi mwa vitegemezi vyako ati kwa vile miye “nimewakosea adabu” sungusungu wa kaya yetu, lakini nasikia ati huko uliko wewe mkulu wa sungusungu mumeanzisha mchezo wa kuoshana maji moto mkibabuana sura kama mwataka kutengeneza staftahi kwa sura za wenzenu na miye humo msinihusishe maana simo. 

Wacha niliseme hili walau niondoe funda lililonikaba kooni maana uhai naupenda na uzima kuliko maradhi lakini uhuru wa kweli huja kwa fikra sahihi na hizo huja kwa lugha sahihi na miye humu sasa nahusikaje?. Aala! Usinitanie. Nasema mzaha wako utatumbua usaha we mwana sikiliza Chokoraa nikueleze yaliyo ya kweli maana unajua yaliyokuwa kwa wale waliokuwa kwenye kiti chako kabla yako na jinsi ambavyo leo hawana heshima isipokuwa nyumbani kwao na hivyo limetanguka lile lililonenwa na manabii kuwa nabii hana heshima kwao, ama hawakuwa manabii na hivyo haliwahusu hilo la nabii kukosa heshima kwao. 

Nani hajui kwamba zilikuwa enzi katika kaya yetu hii hii ambazo watu ati alitumwa tu binti ‘fatuma’ akavunja malango ya watu na wafuasi wakanyang’anya mali na uhai!? 

Hayo sasa yamepita na sasa mwamwagiana ‘mtindi mkali’ na humu miye sasa nahusikaje!?. Simo naapa. Nasema Wadanganyika sasa wamehama makwao wanaishi nyumba za jirani yao Yule mzee mwenye sura mbaya Hofu wa Uoga ati kwa vile kuishi kwao uwaogofya sana hadi wamezoea kuishi “na” kama si kuishi “kwa” Hofu na ndiyo maana miye salaam nakusalimia. 

Nasema ingawa umewapunguzia mzigo wadogo zangu wale wawili Mzembe na Mzururaji wenye  umaarufu wa harufu na hata majina yao siyasikii yakitajwa sana kama ilivyokuwa kwa watangulizi wako, lakini ati kaka yangu Machinga wa Muhangaikaji siku hizi ndiye amechukua zamu ya kusumbuliwa, na ati wadanganyika wanadai imekuwa sawa alivyosema Mkufunzi enzi za uhai wake kwamba ati ‘siri kali’ ikiishakuwa imetoboka inavuja basi hubakia kukimbizana na vijitu vidogo mabarabarani, kwa vile akina kaka mkubwa Mstahiki wa Mtukuka huwa ati wewe na vijana wako mwaogopa kuwagusa kwa vile watakataa “kuja” ila miye humo simo. 

Nasema mimi jina langu halisi ni Chokoraa wa Muhangaikaji naomba msinifananishe na wale vijana wawili wa mzee Si Hasa akina Mchochezi na Mropokaji ingawa tumekua pamoja ila mwenzao  majalala yamenifunda kuwa na adabu ndiposa mkulu miye nakusalimia, shikamoo mkulu wa sungusungu. Sisemi, ndiyo, sisemi kwamba akina mzembe na mzururaji na hata kaka yangu Machinga wa Muhangaikaji wanaruhusiwa kukosa adabu ati kwa vile akina kaka Mstahiki na hata Yule kaka yetu mkubwa Muishiwa wa Mbadhilifu wanaukosea adabu msaafu na mafunzo ya kaya yetu, lakini nasema imekuwaje hata imekuwa kwamba nyie wenye kuijua siri ya mzazi wa Amani bi Haki binti Wajibu na nyie mmekuwa ndumilakuwili mkiufuata msemo wa waswahili kwamba haja kubwa ya ng'ombe mbolea ya bata uchafu!?. 

Haya, nasikia sasa si salama hadi kwenye viota vyenu wenyewe na miye nasema hivi na nyie mlishiriki kula pesa ya sanda ya marehemu Uadilifu hata mkasababisha mzee yule kuzikwa pasipo sanda!?. Ha ha ha ha ha ha ! Nicheke miye maana ikiwa na nyie mlio na taa haramu ya kumulika ili wengine tuone mwatembea gizani kwa uzembe wa kuitia kandiri mafuta, itakuwaje basi yule mama yangu bi kikongwe Shida wa Matatizo wa Taabu wa Muhangaikaji!?. 

Naona kama muda unaniishia nachelea nisikute paka na mbwa wamemaliza vile vilivyotupwa jana jalalani ndiyo maana nakuomba uniruhusu tena juma lijalo nije nikuletee ujumbe nilioagizwa na dada na kaka zangu watoto wa Mdanganyika. Ndiyo, nitakuja tena kwa ajiri ya kukuletea salaam baada ya kuuguza vidonda vya mkong’oto niliopokea kutoka kwa vijana wako nilipojaribu kuukaribia mlango wa afisi yako ili nikusalimu. Mmoja wa vijana wako aliponiona ati akaniita jina si langu eti “we kibaka, watafuta nini karibu na Muishiwa Mkulu wa Sungusungu?”, ile kujaribu kujieleza kwamba miye ni Chokoraa wa Muhangaikaji na si Kibaka, kidundo nilichoambulia ukichanganya na uzito wa ujumbe nilio nao kutoka huko kwetu, ndiyo maana sauti yanitetema nizungumzapo ingawa nina hakika salaam zitafika, salaam nakusalimia. 

Ni mimi mdharauliwa wako, Chokoraa wa Muhangaikaji wa Mlalahoi wa Pangupakavu wa Kabwela wa Mdanganyika wa Mlipakodi nakusalimia, shikamoo mkulu wa Sungusungu.

Thursday, August 22, 2013

Pole kwa Msiba Muishiwa Mkulu wa Kaya.



Salaam nakusalimia. Hizi ni Salamu kwako wewe, ndiyo wewe mkulu wa kaya ya Wadanganyika walipa kodi kutoka kwangu Chokoraa wa Muhangaikaji wa Mlalahoi wa Pangupakavu wa Kabwela wa Mdanganyika nakusalimu, Shikamoo Mheshimiwa. 

Nasema tena kama nilivyowahi kusema hapo kabla kwamba shikamoo si salaam bali mazao ya ukoloni mkongwe lakini wacha niitumie kwako kwa vile hasa ni ukweli usiopingika kwamba niko chini ya miguu yako, shikamoo Muishiwa, aha! Samahani, shikamoo Mheshimiwa. 

Nataka , nimesema nataka wala siombi maana Chokoraa miye sifungwi na ‘proto kali’ ninapotaka kuzungumza na mkulu wa kaya yangu kwa vile yaliyonijaa moyoni ni mazito maana yanatishia heshima ya Mdharauliwa miye kwako wewe Mheshimiwa sana mkulu wa kaya yangu na hapa salaam nakusalimia. 

Hivi! Kwani heshima ni kitu cha bure kama wasemavyo waswahili wa Danganyika yetu!? Si kweli. Naapa ni uongo kuniambia ati heshima ni kitu cha bure maana nijuavyo miye mwana wa Muhangaikaji heshima hulipiwa gharama kubwa ya juhudi, utu, kujituma, kutenda mema na kutumia nafasi na vipawa ulivyojaaliwa na mwenyezi  na pia kuaminiwa na wadanganyika wenzako kwamba waweza kusema na hata kutenda kwa niaba yao na hapa salaam nakusalimia. 

Wala! Wala usinichukulie miye mwana wa Mdanganyika kuwa mmoja wa waungaji mkono wako mbumbumbu ambao hawawezi katu kukwambia ukweli pale unapovurunda katika kutenda yale tuliyoyakasimu kwako kutenda lakini pia si mnafiki miye kitukuu wa Mlalahoi wa kutokusifia unapotenda zaidi ya nilivyotaraji. Nimesema unapotenda zaidi siyo unapotenda kwa kiwango tarajari na humu sasa najitoa maana simo. Nasema kwangu kama unayo masikio ya popo basi yafunike maana ikiwa nitayaona nitasema hadharani kwamba mfalme ana masikio kama popo. 

Hilo si lengo la waraka wangu leo hata hivyo hizo zilikuwa salaam tu na kusalimia mkulu wa kaya ya Wadanganyika Walipa Kodi. Leo ninataka kukueleza kuhusu Heshima ya Mheshimiwa wewe ambaye Mdharauliwa miye ili nikufikie na kukusalimu ni lazima kwanza nitambae mwendo mrefu nikijiangusha chini kila baada ya hatua kadhaa ati kwa vile heshima siku hizi ni shikamoo, basi shikamoo Mheshimiwa.
Nasema ni juzi tu hapa Yule Mnyarwanda alikutupia matusi ya nguoni kwa kumshauri jinsi ya kuishi vyema nyumbani kwake ati kwa kisingizio cha kwamba unaingilia mambo yake ya ndani ilhali kila anapogombana na mkewe wewe ndiye unawapa wanae malazi na chakula. Nadhani huyu ameifanya hii kuwa mbinu ya wewe kumlelea wanae na hii si hoja yangu lakini ni sehemu ya salamu, shikamoo Mheshimiwa. 

Kilichonifanya nikuandikie leo ni kukupa pole kwa msiba, msiba mzito wa walinzi wa kaya yetu hii ya wadanganyika walipa kodi nasema kwa hili wakati ninapoandika Chokoraa machozi yanilengalenga. Silii kwa sababu ya msiba wenyewe maana twafwa sote tu kama upepo upitao na kwenda zake na siku zetu si nyingi juu ya dunia gunia letu hili lakini kinachonisikitisha ni mazingira yenyewe ya vifo vyao.
Najiuliza ni wapi ulipochorwa ule mstari mwekundu unaoweka tofauti kati ya amani na vita na ikiwa kwa hili mstari huu haujavukwa maana mbele naona giza, ila bado nakusalimu, shikamoo mheshimiwa.
Hivi hawa wanaopigana na kuuana kila kuitwapo leo “watwawala” wao si wameamua kwa makusudi kuwateketeza vijana wao walio matumaini ya jamii yao kwa maslahi binafsi hadi pale walipokuja kushtuka maji yashazidi unga na wakaomba kuwapo kwa msaada kutoka kwa jirani?. Ndiyo, na sisi tukawatumia wajumbe wa amani na nani alisema ni mjumbe hauawi!? Naapa aliyenena hili ama alitudanganya au tulijidanganya wenyewe kwa kumsadiki maana wajumbe wa amani wameuawa kwenye uwanja wa vita na mimi nasema huu ni upuuzi. 

Ndiyo. Ni upuuzi kumtuma mwalimu darasani bila chaki wala kitabu ama mkulima shambani bila jembe au hata Chokoraa jalalani bila mfumo wa Rambo asomaye na afahamu na sasa ndugu zetu hawa wamekwenda. 

Ndugu zetu hawa wamekwenda tena walio wengi wamekwenda na ndoto zao, na matumaini yao ya kesho yamezimika na hata wale waliobaki nyumbani ambao matumaini yao yalifungwa kwa hawa basi hawa waliokwenda wamekwenda nayo na itawachukua waliobaki miaka kama si dahali kujenga matumaini mapya na kama ilivyo kovu alisafishwi kwa sabuni likaisha, hawa wamekwenda. 

Kinachonifanya nikuandikie siyo tu kukupa pole bali kukutaka ujivike wewe viatu vya wale waliobaki nyuma ya hawa waliokwenda na ambao siku za usoni pia watakwenda kama ambavyo pia mimi na wewe tutakwenda hiyo njia ya watu wote lakini kwa sasa tuvae viatu vya walio hai maana waliokwenda wamekwenda na hakuna njia ya kurudia huko waendako watu wote. 

Najua, najua utataka kutumia tena busara kwenye hili na hapa mwana wa Muhangaikaji naomba nijitoe maana simo. Ala! Kwani si nimeona tangu umekalia kitu hicho jinsi ambavyo matumizi ya busara yamezaa hasara nyingi kuliko faida ama wataka nikukumbushe kidogo!?. Haya, ebu kumbuka wale walioanza kuhubiri upuuzi wa kipuuzi na kutugawa kwa misingi ya dini, kwani habari hizi hazikufika mezani kwako kwa wakati na ukaamua kutumia busara kukabiliana nao!? Ona sasa tulipofika ambapo hata majalalani Machokoraa twaulizana dini kabla ya kupeana kipande cha boflo na wali uliolala ukatupwa asubuhi. Humu namo simo. 

Tazama, tazama jinsi ambavyo wale waliotuhumiwa kwa ufisadi mkubwa na wakathibitika ulivyotumia busara ya kuwataka warudishe walichoiba badala ya kufichua mwizi na kumwadhibu kwa kadri ya miiko na vijiko vya kaya yetu na mwisho wa siku ni hao hao waliotangaza ati wewe ni dhaifu na hasira zikawapanda wale walio na ngazi za kupandisha hasira hizo miye nikajitoa kama ambavyo hata sasa najitoa. 

Ona jinsi ambavyo ati baada ya fedha kedekede za wadanganyika kutumika kununua Rada na hawa wadanganyika tukatakiwa kula nyasi kama Mbuzi kwa ajiri hiyo bado wanyama wetu walipakiwa kwenye dege tena la kijeshi na kurushwa nje ya kaya yetu na hata sasa bado imetumika busara. Sitaki kusemea wale walioua waandishi na wengine wengi na madhila ya kila leo yawapatayo wadanganyika ilhali wewe mkulu wa kaya ukiwa unaendelea kutumia busara. 

Leo sicheki, nasema sicheki kwa vile nina huzuni na hasira maana nakumbuka kuna wakati wako walioomba ati uwe mkali walau kiduchu tu ili heshima ya uheshimiwa ilindwe lakini naamini hata hao nao ulitumia busara kutowasikiliza kama ambavyo unatumia busara kuwaachilia wale waliokuwa kituoni na wenye wajibu wa kulinda raia na mali zao wanapovamiwa na kuibiwa na hata sasa bado busara ingali inatumika na ndiyo maana najitoa. 

Nakuandikia nikuombe kwa hili muishiwa, aha! Nisamehe, mheshimiwa sana mkulu wa kaya ya Danganyika ya Wadanganyika walipa kodi usitumie busara hata kidogo. Nasema si sahihi kuwa sahihi mara zote maana hilo humaanisha kwamba ustaarabu kwa mpumbavu huonekana kuwa uoga na ndiyo maana hata wale tuliowale na kuwalisha leo wanatutukana na wewe unatumia busara ilhali matusi yao hayaishii kwako tu maana shati ulilovaa kipande chake nimevaa mimi na wadogo zangu wengine watoto wa baba yetu Mdanganyika na hivyo utomvu wao wa nidhamu watuchafua wote japo kusema kweli wewe wachafuka sana maana uko hukoooo mbele yetu. 

Kwani hatuwajui wakuu wa hawa wauaji waliowaua vijana wetu? Wako wapi akina Sikamona na wenzie ama waliishia tu kwenye mawazo ya akina Mtobwa na hivyo Danganyika yetu haina tena mashujaa wa Salaamu toka kuzimu ili wawapelekee salamu wajinga hawa kwa ujinga wao wa kuwaua wajumbe wetu wa amani ilhali wanajua fika mjumbe hauawi!?. 

Nasema ni wakati sasa vijana wetu wavuke mipaka wakawatafute wahalifu hawa na kuwaleta hapa kwenye kaya yetu ili tuwakalishe kwenye ule mbuyu mkubwa na kuwazodoa kwa mawe na maembe mfu na ujumbe ufike kwa jirani kwamba kila atakayemgusa Mdanganyika pasipo kuzingatia taratibu atazodolewa. 

Nasema sisi kwa sisi tugombane na kuumizana maana mwanao ukimpiga mwenyewe unajua kiwango cha adhabu lakini anapopigwa na jirani huna budi kujua sababu vinginevyo umeshindwa kuwa baba na kumfunda mwanao kuwalinda wanawe baada yake na humu miye simo ila salaamu nakusalimia.
Nasikia umemtumia salaam mkulu mwenzio wa kaya ya jirani afanye “haraka” kumtafuta nyoka aliyeuma vijana wetu maana yumo humo ndani mwake na kwamba ikiwa atashindwa kumpata “haraka” basi utawatuma vijana wako kumkamata mwenyewe huyo nyoka na Chokoraa nauliza tafsiri yako ya “haraka” mara hii inamaanisha nini !!?. 

Ni mimi Mdharauliwa wako, Chokoraa wa Muhangaikaji wa Mlalahoi wa Pangupakavu wa Kabwela wa Mdanganyika  Mlipakodi nakusalimia. Shikamoo Mheshimiwa. 

Wednesday, July 10, 2013

Mwala magengeni mwezi huu; Vyungu vya nini!?





Nasema mapema kwa hili wana wa Danganyika hii mmenikera na ndiyo sababu miye sitaki kuhusika maana simo tena simo kabisaaaaa. Ala! Kwani  si mwezi  mtukufu wa ramadhani si umeingia na ati siku moja kabla ya mwezi kuanza wengi wenu mlikuwa na sherehe ya kuvunja vyungu kwa vile kwa mwezi mzima hamtakula!?. Naapa mwamtania Mungu enyi wana. 

Naapa kwa jina la Babu yangu mzee Mlalahoi wa Pangupakavu wa Kabwela wa Mdanganyika, nyie mwamtania Mungu. Nasema mmemgeuza Mungu kuwa babu yenu na miye humo msinihusishe. Ala! Si nimeshuhudia mwenyewe ambavyo jana wengi wenu hamkuwamo majumbani kwenu na hata mmedhulumu haki za 'ndoo' za wenzi wenu kwa kuvunja vyungu vyote ati kwa vile mwezi huu hampiki ila mwala magengeni na sasa vungu vya nini!? Naapa laana mmelaaniwa enyi wana na miye humo simo. Sitaki, tena nasema sitaki kuwashawishi mkubaliane na mimi katika kila nisemacho lakini ni kweli kwamba ama hizi dini zimekuwa kwenu kama kongwa la utumwa ni vyema mungelizivua mkatembea huru katika uhuru wa mwendawazimu kuliko huu wazimu wa usiku muufanyao naapa mmenikera enyi wana. Na sasa najiuliza wakati ninapowatakia wale wenye nia safi Ramadhani karim, nyie wengine ambao jana mmefanya kufuru ya kuvunja vyungu vyetu niwaambieje? Poleni na starehe?. Simo.

Nasema kwa kitendo chenu hiki nashindwa kujua niwaiteje maana kuwaita wafuasi wa dini itakuwa kuikosea adabu dini yenyewe maana ikiwa hao mitume walioleta kwenu dini hiizi wangefufuka leo, bila shaka na ongezeko hili la magonjwa yasiyokuwapo enzi zao wangekufa mara ya pili mara hii kwa magonjwa ya moyo kama si sononi na humu najitoa maana simo.

Haya, wacheni nijiropokee maana humu ndani naweza kuropoka tu bila hofu kwa vile mimi ni Mdanganyika tena mlipakodi na ninafahamu nyie wenye kuvunja vyungu vyetu ili wote tushinde njaa kama ninyi hamna mahusiano ya karibu na wale wasiojulikana na hivyo sikuogopeni katu. Nasema nyie si wafungaji ni washinda njaa na mwaiongoezea kaya yetu mzigo wa kuuguza wagonjwa wa vidonda vya tumbo na magonjwa yake kwa kujisindisha njaa ilhali nafsi zenu zili dhalili na humu mnitoe. 

Ala! Kwani hayakuwatosheni maovu ya mwaka mzima hadi mlipoamua kufanya kufuru za mwaka mzima “ini advansi” kwa vile funga imekurubia?. Ha ha ha ha ha ha ha!!!! Najiuliza wadanganyika nyie mwajidanganya na nini kuwaza kwamba huyu Mungu anawaza kama muwazavyo ninyi na hivyo atawaosheni na maovu yenu ya makusudi muyatendayo kwa kujikinahi!?. Hayo nakuachieni nyinyi maana hata mimi ni muovu mwana wa uovu na yamkini hata mimba yangu ilitungwa hatiani lakini kwa hili msijifananishe name maana simo.
Nasema mimi na ninyi hatufanani kwa sababu binafsi najifahamu kwamba sihitaji kujishindisha njaa kwa sheria tu ilhali nikiwa muovu na hivyo wakati wenzangu jana mmevunja vyungu vyote mtaani, mimi nimenunua magudulia ya chuma nasonga ugali nile nishibe ili nikuchekeni nyie wenye kujivisha ngozi za kondoo ilhali ndani ni mbwa mwitu wakali. 

Hivi, nyie si ndiyo wale mliohusiwa juu ya vita vilivyo bora zaidi  yaani vita vya kuishinda nafsi!? Mbona sasa mmekuwa watumwa wa nafsi zenu wakati ingekuwa rahisi kwenu kula mkashiba mkafanya kazi na kuongeza uchumi wa jamii zenu huku mkiwa na afya njema na nafsi safi bila kulazimika kuwa wanafiki!? Naapa huu wa wavunja vyungu ni unafiki tena unafiki mtupu!. 

Kasirikeni mkasirikavyo lakini jueni kwamba mwana wa muhangaikaji kwa hili mmenikera lakini sina hasira sana kama nilivyo na huruma. Ninawahurumia na ndiyo sababu ya kukuandikieni waraka huu ili mwenye masikio ya kupona asikie hizi dawa lakini ikiwa ni wa kufa basi ziba masikio kwa hasira na visingizio. Ndiyo, najua mtaleta visingizio kwamba ati Chokoraa miye nimeitusi dini nasema huo utakuwa ni unafiki wa radaja la pili maana miye siitusi dini ila nawauliza wenye kujifanya mwaifuata dini kana kwamba kwa shuruti huku mkifanya kufuru, mmejihoji ni wangapi kati yenu mliokumbuka kula pipi zenu kwenye maganda ama huko nako mlivunja vyungu!? Naapa ikiwa na hilo nalo mlilivunjia vyungu, basi jiulizeni ni wangapi kati yenu mlioambukizwa kale kaungonjwa na mnaojiandaa kunilaumu Chokoraa nikikataa kuja kuwaona mlazwapo hospitali na wengine kusema nawanyanyapaa!? Kwa hili naapa niiteni mnyanyapaa lakini hata kwa Mungu sina hatia ikiwa nitawanyanyapaa kwa kujisulubisha wakati wa kuvunja vyungu maana kuna tofauti ya makusudi na bahati mbaya msiolijua hilo jilaumuni wenyewe na humu simo.

Haya, na wale ambao mliwatoroka wazazi wenu na kwenda kwa vibwana vyenu huku mkidhani mwawafurahisha kumbe mwajitafutia majukumu ya ulezi msiyoyaweza bado na mwisho wa siku mwataka jamii ibebe mzigo wa kunilea Chokoraa miye na wadogo zangu akina mzembe na mzururaji!? Hivi na hili nalo linahitaji “sirikali” kukupeni onyo mapema?. 

Komeni. Nasema komeni hasa nyie mjiitao “wana haraka tu” kuipigia kele ‘siri kali’ ati kwa kutofanya chochote kuwasaidia ‘watoto wa mitaani’. Nasema mkome. Ndiyo, najua wengine ni rafiki zangu lakini nisikilizeni maana kwa hili siropoki nasema hakuna mtoto wa mtaani maana kila mtoto ana baba na mama yake na ni lazima wawajibike wao kwanza kuondoa watoto wao mitaani na ndipo sisi wengine tutafuata!?. Ala! Mwataka tu nyie mfanye fujo zenu na kuvunja vyungu vyetu bila mipango wala mikakati ya kukabiliana na matokeo ya uvunjaji vyungu huo kisha siye tuwajibike!? Nani kasema!?. Simo humu namo. 

Ha ha ha ha ha ha!!! Hongera zenu wajasiria mlo maana nina hakika kwa siku ya jana nyie jana mlikuwa na “ugeni” mkubwa na hata wengine walilala sebleni na hata wako waliopitisha muda wao kwenye maliwato na huko kote wakivunja vyungu. Kwani viliwakosea nini?. Ama kosa la vyungu hivi ni kuwapikieni mwaka mzima na sasa kwa vile mwezi huu mwabadili ratiba ya kula basi vyungu havina thamani tena?. Nasema nyie mliovunja vyungu jana hamjafunga hata kidogo. Mmebadili tu muda wa kula kwa kuacha kula mchana mzima huku mkifakamia milo yote usiku maana kufunga huanzia kwenye nafsi na nyie nafsi zenu mmeziuza kwenye kuvunja vyungu. 

Haya, najua wako wale ambao kwa nia ya kweli ujio wa ramadhani umewakuta wamejiandaa nafsi zao kwa ajiri ya muumba wao. Kwenu nyie salamu zangu ni chache tu. Muombeni huyo Mwenye Enzi yote aliyevifanya vyote atufanyie wepesi hasa kwenye kaya yetu hii itafunwayo kila siku na dini huku wote tukifanya juhudi kumtafuta Mungu huyo huyo. Kwenu nyie nasema ‘kun faya kun’ mnisamehe ikiwa neno hili limekosewa lakini ikiwa yeye mwenye kusema kuwa likawa angetaka wote tuwe dini moja isingeshindikana na hivyo muombeni aturudishie mioyo ya subira tujue kuvumiliana na kuchukuliana katika kutofautiana kumwamini kwentu maana Mungu ni mmoja tu hajakuwako mwingine kabla wala baada yake hatakuwako mwingine sasa sisi twagombea nini? Twagombea mapokeo yaliyoletwa na wale walioleta tena kwa maslahi yao binafsi wakituchonganisha ili watuibie? Naapa huo nao ni uduni wetu wa kufikiri na humo miye simo.
Tuombeeni. Wala smituombee atujaze mapesa mifukoni maana amani na furaha ya kweli haitokani na kuwa na mifedha kedekede lakini atujaalie akili njema na uwezo wa kuziona na kuzitumia fursa kujitendea na kuwatendea wengine mema. Tuombeeni atujaalie kujua kwamba yaliyowekwa wazi ni yetu na watoto wetu ili tuyatende nay ale yaliyofichwa ni yak wake ili tumche na kumwabudu na siri ya kwanini Chokoraa namwamini hivi na wewe waamini vile si yetu ni yake tuache kuyachokonoa yasiyo yetu. 

Mwisho niombeeni na mimi ndugu yenu Chokoraa mwana wa Muhangaikaji walau nitengeneze mkate hata kama ni wa unga wa mahindi badala ya kuokoteza kila siku maana akina kaka muishiwa hawataki kunitupia tena vipande vikubwa wanasema nikishiba sana nawapigia kele na hivyo nile kidogo ili nguvu zinipungue wanitawale. 

Ni mimi ndugu yenu, Chokoraa wa Muhangaikaji wa Mlalahoi wa Pangupakavu wa Kabwela wa Mdanganyika nawasalimu. Ramadhani Karim.Salaam nawasalimia.

Tuesday, July 9, 2013

Udini Tanzania; Viongozi wa Dini Oneni Haya.



Najua, najua kwamba hatutakubaliana wote lakini kwenye hili ni lazima ukweli usemwe na kama hakuna anayeusema ukweli basi tunabaki gizani na si rahisi kusogea na huenda hiki ndicho baadhi yenu mnachotaka, kwamba tuendelee kuwa gizani na ninyi mliopaswa kumulika mishumaa mwaiwasha huku mmeifunika vitambaa vyeusi. 

Tuwe wakweli, Tanzania inatafunwa na ugonjwa mbaya kuliko yote na huu ni ugonjwa wa ‘Udini’ na sina shaka kusema haya ni matokeo ya  matendo na hata maneno ya viongozi wa dini. Nakumbuka kipindi fulani Waziri Mkuu wa Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania aliwataka viongozi wa dini wasiilaumu serikali kwa kuwapo kwa tuhuma nyingi za rushwa ndani ya taasisi zake kwa vile wala rushwa hao ni waumini wa viongozi wa dini na wako waliombeza, lakini nasema kwa hili Mheshimiwa Mizengo Pinda alisema ukweli isipokuwa tu kwa sababu wengi wa watanzania sasa hivi tunapenda kusikia maneno laini na matumaini matupu kuliko ukweli uumizao, basi alibezwa. 

Kwani ni kipi alichosema Waziri Pinda wakati huo ambacho hakikuwa na ukweli wowote?. Ebu tutafakari pamoja. Ni ukweli ulio wazi kwamba dini inayo athari kubwa ya jinsi ambavyo mtu anaishi na kuishi kunajumuisha kutekeleza majukumu yake ya kila siku akitumia elimu na vipawa vya kimaumbile aliyojaaliwa na mwenyezi Mungu. Hili si jambo la Tanzania peke yake, ni jambo linalogusa hata mataifa makubwa duniani kama Marekani  taifa lenye kujionyesha kuwa kinara wa demokrasia duniani. 

Kwenye gazeti la Los Angels Times la huko Marekani la tarehe 16/03/2007, msemaji wa mgombea urais wa wakati huo  na aliye sasa Rais wa taifa hilo Barak Obama, Bw. Robert Gibbs katika waraka wake kwa waandishi wa habari, aliwaambia wapiga kura kwa kuwahakikishia kwamba Barak Obama alikuwa Mkristo na kwamba hajawahi kuwa Muislamu. Alisema katika waraka huo kwamba “Obama siyo na wala hajawahi kuwa Muislamu” na walio wengi wakajiuliza kama ambavyo wanaendelea kujiuliza leo kwamba je, kama Obama angekuwa muislamu asingechaguliwa kuwa rais?. Je, ikiwa leo rais Obama atatangaza kubadili dini yake na kuwa muislamu basi ataondolewa madarakani? Na kadhalika na kadhalika. Jambo moja ni wazi hata hivyo, kwamba dini inao mchango mkubwa kwenye maisha ya kisiasa ya wanadamu na hatuwezi kuitenga dini na siasa. 

Binafsi naona dini na siasa kufanana kwenye maeneo mengi ikiwamo ukweli kwamba viwili hivi vinaendeshwa kwa misingi ya imani. Ndiyo. Mfuasi wa chama chochote cha siasa anaamini kwamba sera za chama chake na uongozi mzuri wa chama hicho ndiyo msingi wa maendeleo yake na  ndiyo maana anakipigia kura kimtawale. Vivyo muumini wa dini yoyote anaamini kwamba dini yake ndiyo bora kuliko ile ya mwenzake na ndiyo maana anayaacha mafundisho ya dini hiyo kutawala matendo na hata maneno yake.
Kwa hiyo ni sahihi kusema dini ni siasa kama siasa ilivyo dini. Ni ukweli wa kihistoria kwamba kumekuwapo na tawala nyingi duniani kwa karne na miongo mingi zenye kujiendesha kwa kufuata mfumo wa kidini yaani ‘serikali za kitheokrasia’. Katika serikali hizi, huaminika kwamba Mungu (kwa tafsiri ya watu ama jamii inayoongozwa na mfumo huu) ndiye mwenye kuongoza taifa na kwamba kiongozi mkuu wa nchi ni mteule mwenye mahusiano ya hali ya juu na ya kipekee na mungu huyo na hata maelekezo yake kuhusu jinsi ya kutatua migogoro na matataizo ya jamii yake huaminika kuwa yanatoka kwa Mungu. Mifano iko mingi lakini mfano wa jinsi Mussa alivyowaongoza waisraeli kutoka mikononi mwa Farao ama Firauni kama ajulikanavyo na baadhi ya misahafu, unaweza kutuonyesha vyema jinsi dini ilivyo na siasa ndani yake.
Lakini pia Siasa na Dini vyote hufanana kwa kuzingatia kwamba vyote huishi na kufaulu kwa kutumia nguvu ya ushawishi. Neno siasa linatafsiriwa na msomi wa kiarabu iliyo lugha yenye kuchagia maneno mengi kwenye Kiswahili kuliko lugha nyingine yoyote, Shaikh 'Alee Hassan Al-Halabee ya kwamba “ Ni kuhami na linda masuala ya umma”, neno Politics ambalo hutumiwa kumaanisha siasa kwa kiingereza linatafsiriwa kuwa ni ‘uwezo wa kuhamasisha jamii ya watu ama mtu mmoja katika kufikia malengo ya kiutawala”. Hivyo basi ni sahihi kusema kwamba dini na siasa haviwezi kutenganishwa na maisha ya kila siku ya mwanadamu kwa vile tunafanya vyote viwili kwa wakati mmoja tunapotenda majukumu yetu ya kila siku. 

Hayo hapo juu hata hivyo hayafanyi hoja ya waziri mkuu kuwataka viongozi wa dini wajitafakari wenyewe badala ya kuilaumu serikali kuwa na mashiko sana ila mantiki yake kwamba wala rushwa ni waumini wa dini hizi ndiyo hoja ya msingi. 

Viongozi wa dini ndiyo watu wenye dhamana ya kuamua muelekeo wa kidini wa watu wetu, na si hilo tu lakini kama alivyowahi pia kusema Rais wa awamu ya tatu Mh. Benjamini Mkapa kwamba maneno ya viongozi wa dini yanaaminika kuwa maneno ya Mungu miongoni mwa waumini, ni kweli kwamba sisi wengine kwa ujumla wetu tumewaachia viongozi wa dini watuongoze kuhusu masuala mazima ya kidini na bila kuwaingilia na hivyo ikiwa dini leo inageuka kuwa tatizo zito kiasi cha kutishia utaifa wetu, basi wa kulaumiwa wakiwa wa kwanza ni viongozi wa dini. 

Ndiyo, tunawalaumu wanausalama kunapokuwapo na uzagaaji wa siraha za moto na kuhatarisha usalama wa watu na hata usalama wa taifa si kwa kuwaonea bali kwa sababu kwa mwanachi wa kawaida hapa Tanzania hawezi kutofautisha hata milio ya risasi tu kutoka bunduki moja hadi nyingine kwa vile hiyo ni tasinia iliyo na wenye  taaluma, ujuzi na ufahamu nayo ambayo jamii nzima imewaamini na kuwapa jukumu siyo tu la kumiliki na kutumia siraha hizo kwa niaba yetu, bali kuhakikisha usalama wa siraha zenyewe, sasa kwanini mnataka tusiwalaumu wale waliopewa jukumu la kusimamia na kuhakiki usahihi wa mafundisho yatolewayo kwetu wakati jamii  inapohitaji miongozo ya kiimani?. 

Kuwaweka kando viongozi wa dini na kuilaumu serikali kwenye suala la udini ni sawa na kuibiwa mali kwenye ghala na kumweka kando mtunza ghala na kumlaumu muhasibu ati kwa vile tu majukumu yao yanaingiliana bila kuzingatia kwamba mtunza ghala alikabidhiwa majukumu maalumu kutunza ghala hilo hata kama muhasibu anahusika kusimamia matumizi ya rasilimali za shirika. 

Sisemi serikali haina sehemu katika madhila haya yanayoikumba jamii yetu leo, lakini nasema ikiwa kwa namna yoyote wanasiasa wametumia dini kujipatia matakwa yao ya kisiasa na hivyo kuyumbisha mfumo mzima wa jamii kwa kutojulikana mipaka kati ya dini na siasa, si kosa la wanasiasa bali la wanazuoni wetu ambao kwa makusudi ama kwa uzembe wameshindwa kusimamia misingi ya kiimani kuhusu uwajibikaji binafsi wa waumini wao kwa Mungu wao, waumini ambao ndiyo wanasiasa wanaolaumiwa.

Nasema ikiwa kiongozi anawalaumu wale anaowaongoza kwa kushindwa kutekeleza yale waliyopaswa kuyatekeleza, kiongozi huyu ameshindwa kuongoza hana budi kukaa kando awaanchie wengine waongoze.
Yanayojitokeza leo kwenye majumba ya ibaada ni matokeo ya viongozi wa dini kujichanganya wenyewe na kushindwa kusimamia misingi ya utakatifu na heshima kwa Mungu waliyepaswa kumtumikia. Nani haoni vile ambavyo leo mimbari zimegeuka majukwaa ya kisiasa tena yakitumiwa na wanasiasa ambao wana tuhuma nzito kwenye jamii zao wakiwa wamejichafua kwenye ulingo wa siasa na kukimbilia kujiosha kwenye majumba ya dini!? 

Najua wako ambao mtasema si kazi ya viongozi wa dini kuwatenga wakosefu bali kuwapokea na kuwasaidia lakini nasema Mungu mwenyewe hatoi msamaha kwa wasiotubu na hata manabii na mitume walilifundisha hili na hakuna kati yao aliyesema unaweza kumsamehe mkosefu kimya kimya tu bali “akitubu msamehe” na mimi najiuliza hivi watuhumiwa hawa ambao  wamekataa hata kujibu tuhuma zao (japo kusema kweli si tuhuma za kisheria bali za kijamii) na kujisafisha mbele ya jamii na badala yake kukimbilia mbele ya viongozi wa dini ili wawasafishe, watazuiwa na nini kesho wapatapo nafasi kuvurunda tena na kuwataka muwasafishe kama mwanzo?.

Niseme kama alivyowahi kusema Yesu “…chumvi ikipoteza radha yake yafaa nini….” Na mimi najiuliza viongozi wa dini wanaofanya michezo hii wanajua madhara ya kukumbatia watu wenye tuhuma bila kuwawajibisha ma madhara yake?. Najiuliza itakuwaje ama mtamlaumu nani ikiwa tutafika mahala ambapo watu hasa vijana tutakataa kuja kwenye majumba yenu ya ibada kwa vile kumbe huko nako ni kunajisi kama ilivyo kwenye siasa na badala yake kuamua kubaki nje kwa vile ndani na nje kote kunanyesha na hivyo ni bora kulowa huku ukitembea maana mwisho utakuwa umesogea hatua kuliko kuloa ukiwa mahala pamoja?.
Viongozi hawa wa dini ndiyo wanaoshadidia mafundisho yenye kusababisha mitafaruku mikubwa kwenye jamii yetu na si ajabu kwamba leo vijana wa kitanzania ni wazalendo zaidi kwa dini zao kuliko walivyo wazalendo kwa jamii yao. Si ajabu vijana wengi wa kitanzania wanaamini jamii yao ni wale wenye imani ya kidini sawa na wao na wale wenye imani tofauti si sehemu ya jamii yao na hivyo hakuna ndani ya akili za vijana hawa ile iliyojulikana miongoni mwetu kwa miaka mingi kama jamii ya Kitanzania.

Pita kwenye mahubiri na mihadhara mingi utawasikia viongozi wa dini wakiwahubiri vijana wao juu ya umuhimu wa kujitazama kwa “wao” kwa maana ya dini zao badala ya kutumia mwanya wa kuwafundisha imani ya dini ili kuitumia kutatua matatizo yao na jamii zao. Yako mabaraza mengi ya kidini nchi hii na yote yamengukia kwenye mkumbo ule ule. Si mabara ya maaskofu wala masheihk yanayochukua hatua kuwakemea wajinga wachache, natumia neno wajinga na si wapumbavu, wanaojaribu kueneza chuki miongoni mwetu na ndiyo maana kukawa na wachungaji wenye kutumia vituo vyao vya redio kutukana na kupandisha jazba waumini wa dini nyingine hadi serikali ilipoamua kuvifungia. Nauliza wakati wote wahubiri hawa wanahubiri sumu hizi ndani ya jamii yetu, mabaraza ya kidini ya dini hizi yalikuwa yakifanya kazi gani!? Kwani jukumu la mabaraza haya ni nini kama si pamoja na kuhakikisha kwamba mafunzo ya dini hizi hayapotoshwi?. 

Kwani wale waliojiita masheikh waliokuwa wakiendesha mihadhara yenye kuchochea chuki na kusambaza CD za chuki hizo walikuwa kwa namna yoyote hawawajibiki kwa mabaraza ya kidini? Mbona viongozi wa mabaraza hayo wasikemee upuuzi huo hadi damu zimemwagika ndipo ati polisi inawatafuta na wao kukimbilia nje ya nchi?. Najiuliza je, viongozi wa kidini wanafurahishwa na  mafundisho haya yenye kuibomoa jamii yetu? Kwa faida ya nani!?

Ni unafiki. Ni unafiki leo viongozi wa dini kusimama na bila aibu kuilaumu serikali kwamba ndiyo inayochochea udini wakati dini ni tasnia pekee ambayo kwa miaka mingi haikuingiliwa na serikali ndani ya nchi hii hadi pale wenyewe wanaposhindwa kuendesha mambo yao na kusababisha vurugu. Ni ajabu kwamba hata inapofikia hapo bado serikali inapoingilia utawasikia viongozi hawa hawa wakilalamika kwamba serikali inaingilia uhuru wa kuabudu wakati wameshindwa kuutumia uhuru na kuufanya kuwa uendawazimu. Maana uhuru usio mipaka ni uendawazimu. 

Wakati viongozi wa dini wanapojitafutia umaarufu kwenye vyombo vya habari kwa kuzungumzia masuala yasiyowahusu kana kwamba wao ndiyo wasemaji wa taasisi za umma ama kujitokeza kwenye vyombo vya habari kuzitaka taasisi za umma kujibu hoja zao na bado wakaendelea kudai wasiingiliwe uhuru wao wa kuabudu, binafsi ninaona kama wameiondoa ibada kwenye milango ya mahekalu na masinagogi na kuipeleka kwenye malango ya ikulu jambo ambalo ni kinyume na katiba na ni kuingilia uhuru wa taasisi nyingine.
Wako ambao hadi leo wanalalamikia kauli za kiongozi mmoja wa dini ya kikristo kufuatia vurugu za Mwembechai mnamo February 13, 1998 ambapo baada ya vurugu hizo, kiongozi mmoja wa dini alijitokeza mbele ya waandishi wa habari akisema “jeshi la polisi halikutumia nguvu kubwa bila sababu na kwamba ilikuwa sahihi kutumia siraha za moto kwa sababu raia(akiwataja kwa dini yao) nao walikuwa na mawe na kwamba mawe nayo yanaweza kuua….”. Ni kauli za jinsi hii na zifanazo ambazo zimechangia kuchochea migogoro ya kidini kufikia hapa ilipo leo kwa sababu kiongozi huyu hakupaswa kwa namna yoyote kusema aliyosema hata kama yeye aliamini ni sahihi na hata kama kwa mujibu wa katiba anao uhuru wa kutoa maoni yake, lakini alipaswa kuzingatia nafasi yake na kutafakari madhara ya yeye kutoa maoni hayo maana hekima ni uwezo wa kusema neno sahihi, mahala sahihi kwa wakati sahihi na kwa namna sahihi. Ikiwa utanisalimu salamu ya asubuhi wakati wa machweo, utakuwa umefanya kitu sahihi kwamba umenisalimia, ila utakuwa umekosa hekima kwa kunisalimu salamu ya asubuhi wakati wa jioni. 

Ni wakati sasa viongozi wa dini wajichunguze na warudi nyuma kufanya mambo kadhaa waliyoyaacha. Viongozi hawa waache kukubali kuwa daraja la wanasiasa na wahakikishe kwamba wanawaunga mkono wanasiasa katika mambo ya maendeleo lakini pia wapime upepo na kutazama sifa ya mwanasiasa katika jamii na ni lazima wahakikishe kwamba wanasiasa wanajua kwamba ikiwa watajichafua kwenye utendaji wao, dini hazitakuwa mahala pa kujisafishia. 

Viongozi wa dini wakemee watu wanaoibuka kila leo na kufundisha mambo yaliyo kinyume na upendo na amani na hata mshikamano wa watu wa jamii yao badala ya kuingia kwenye makundi ama kuoneana aibu ati kwa vile huyo anayekosea ni wa mlengo wa dini yangu na hivyo siwezi kumkosoa hadharani. Ni lazima viongozi wa dini wanaopotoka kutoka kwenye misingi ya kidini na kuvunja hata sheria za nchi kwa mahubiri ama mafunsidho yao wakemewe na viongozi wenzao wa dini na ikibidi hadharani ili dini zirudi kuwa mahala ambapo mizaha ya hatari haiwezi kuruhusiwa kamwe. 

Ni lazima tuache kuwashabikia watu wenye kufanya vitendo vya kipuuzi na kuumiza binadamu wenzao ati kwa kisingizio cha dini lakini pia tusiwakalie kimya na kisha kusimama tukijiosha kwamba hao ni “wahuni” maana wanachofanya hakikubaliki na dini, ni lazima tuseme hadharani mapema kwamba hawa wanachofanya hakikubaliki na tuwapinge badala ya ama kuwavisha mavazi ya heshima ama kuwakalia kimya hadi serikali inapoonyesha kukasirika ndipo ati na sisi tunaibuka na kauli za kujiosha. 

Viongozi wa dini walinde heshima ya mimbari na pia wasimame ndani ya mipaka yao badala ya kujitwalia mamlaka ya kusema kuhusu kila kitu maana miluzi mingi humpoteza mbwa na ni busara kunyamaza kuliko kusema ikiwa kusema kwenyewe ni kwenye kuchochea moto unaochoma nyumba tayari. Ikiwa bado viongozi wa dini mnataka kujiingiza kwenye siasa na kisha kuwalaumu wanasiasa mi nadhani ni wakati sasa mfike mahala muone haya kwa haya yanayotokea. 

Ni mimi ndugu yenu Chokoraa wa Muhangaikaji wa Mlalahoi wa Pangupakavu wa Kabwela wa Mdanganyika, nawasalimia.