Wednesday, October 15, 2014

Mwaujua Ugonjwa wetu enyi wana!?



Salaam nawasalimia. Nasema tofauti ya mjinga na mwerevu ni ipi ikiwa nilijualo hulijui na ulijualo silijui na ujinga ni kutojua jambo enyi wana salaam nawasalimia. Ha ha ha ha ha ha!!! Nicheke miye! Kwani si mlikuwa mwalalama ati mwataka makubaliano mapya nyie mwaita katiba ya kugawana kaya yenu? Haya, kiko wapi sasa enyi msiojua majira na nyakati hata mwalana na kuraruana mkigombea fito ilhali mwajenga nyumba ileile?. Naapa humu simo. 

Ona huyu naye ati niwachilie mbali viapo kwa vile viapo vyazuiwa na mila za kikoloni pasina kujua kiapo ni ukomo wa uwezo wa mwanaadamu, na mimi katika kukueleweni nimefika ukomo na naapa mwaniapisha enyi wana na miye humu simo. 

Shikamooni Wana wa Haraka Tu. Ndiyo, salaam nawasalimia kwa vile haraka zenu zakuponzeni mwapotea njia mchana kweupe kwa uvivu wa kuuliza na miye humo nahusikaje!?. Simo. 

Ala! Mwadhani ati kwa vile Chokoraa miye hushinda majalalani nikichakura nipate cha kuwalisha vitegemezi vyangu wana wa mama yangu Shida wa Matatizo wa Taabu wa Maisha magumu mke wa mzee wangu Muhangaikaji wa Mlalahoi wa Pangupakavu kilembwe wa Mdanyika Mlipakodi, basi siijui tofauti ya adhuhuri na jioni!? Mwanitania enyi wana na miye humo simo. 

Nasema wachilieni mbali uzandiki wenu ashakumu si matusi ila ikiwa kwenu kuuita uovu kwa jina lake matusi, basi miye salaam nawasalimia. Ndiyo, nakumbuka sana miaka ile ya kipindi kile cha Yule kitukuu wa Nchumali Ntoto wa Chilingi mwana wa Chipuputa mlivyokuwa mkiiandama ‘siri kali’ tena kwa kuivisha koti la chama cha upinde wa zamani, na kudai ati inakataa kuanza mchakato wa katiba na hivyo kuwahujumu wanyonge. Naapa wanyonge wa kaya hii wamekosa msemaji na miye humu nitoeni. Ala! Kwani mwadhani sioni jinsi ambayo kwa Mkwere huyu kukuruhusuni mfanye huo mchakato wenu mlivyowageuza ‘wana wa kaya’ kuwa ngao katika vita yenu ya panzi!?. Nasema msinitanie enyi wana maana miye si babu japo kusema kweli kwenu nyinyi pia si mjukuu na humu pia nitoeni. 

Nauliza maana kuuliza si ujinga, kwani ‘Waishiwa’ ninyi si ‘wana wa kaya’ ati kwa vile tu mko kwenye hilo genge lenu la wahuni wajuao kuvaa mavazi na tabasamu za kikoloni? Kama na nyie ni wana kaya, inakuwaje mwagombana na kila mmoja akidai anatetea maslahi ya Wana wa Mdanganyika wa Mlipakodi? Naapa mwatufanya mazuzu enyi wana na miye humu sitaki katu kuhusika maana simo, tena simo kabisaaaaa! 

Ati! Hivi mwadhani shekeli za baba yetu Mdanganyika wa Mlipakodi mnapoziswaga kama Ng’ombe waendao machinjioni kwa kisingizio cha kutuandalia  ka tiba kaliko bora bila kuufahamu vyema ugonjwa wetu, sisi nao ni wajinga tusioifahamu janja yenu!? Wacheni dharau enyi weledi wenye kwenda mbele ilhali macho yatazama mtokako na miye humu nahusikaje!? Simo.

Haya, mwabishana na kugombana kila mara ati muwe na siri ngapi za kuzitunza pasina kujiuliza hizo mlizokuwa nazo zimevujaje hata kutufikia sisi akina Chokoraa kama mwafahamu kutunza vyema hizo ‘siri zenu kali?’. Naapa ujinga hauna tafsiri na miye humu nitoeni.
Kwani nyie si ndiyo mliokuwa vinara wa kumnukuu Yule mzee mwana wa Mzalendo na hapa namsema Mkufunzi wa Mzalendo wa Mdanganyika, ki wapi sasa kile mlichokuwa mkituaminisha sisi wadharauliwa wenu kwamba “wale” wameasi misingi iliyotiwa na Mkufunzi na “ninyi” ndiyo manabii pekee mliobaki kuirejesha kaya yetu kwenye msingi?. Ha ha ha ha ha!!! Nasema penye pongezi zitolewe na mimi nakupongezeni maana mwauweza vyema mchezo wa ‘si hasa’ isipokuwa izi za mara hii ni zile za majitaka yasiyofaa kwa kunywewa ama kilimo cha umwagiliaji kama mjitapavyo na miye humu simo. Ala! Mlipoona misingi ya huyo mkufunzi mwenyewe inakinzana na tamaa za mioyo yenu, si nilikusikieni baadhi yenu mkimtusi hadharani kama wana wasio malezi wenye kutukana wazazi? Naapa laana mmelaaniwa enyi wana na miye humo simo. 

Nani kakudanganyeni Chokoraa miye na wadogo zangu ukoo wa Mdanganyika Mlipakodi ugonjwa wetu ni idadi ya ‘siri’ zenu!? Kwanza hatutaki hata kuzijua hizo siri zenyewe, ziongezeni ukali hata tusizikaribie kama mwataka, lakini hakikisheni kaya yetu inabaki moja kama alivyoiwacha mwana wa Mzalendo na msipotenda hayo, naapa hatutaiwachia historia kuwahukumu bali tutawahukumuni sisi wenyewe na  miye humo simo tena simo kabisaaaa, ila salaam nawasalimia. 

Ni mimi Mdharauliwa wenu, Chokoraa wa Muhangaikaji wa Mlalahoi wa Pangupakavu wa Kabwela wa Mdangayika wa Mlipakodi nawasalimia. Salaam Waishiwa.  

No comments:

Post a Comment