Thursday, March 12, 2015

KWANI HUU SI MWAKA WENU WA UCHAFUZI!? CHAFUANENI.



Salaam nawasalimia!

Hivi! kwanini wengi wenu mmekuwa “mnanidipu” kwenye kitochi changu na ati kwavile Chokoraa nina “gando” la kugandishwa nikiwapigia mnakimbilia kuniuliza mbona siku hizi sionekani!?. Ala! Mwataka nionekane wapi!? Kwenye vilinge vyenu vya ulevi wa “si hasa” majitaka!? Nani kasema nataka kulichafua kaniki langu na majitaka yenu?. Simo naapa. 

Ha ha ha ha ha!!! Chafuaneni maana huu hasa ndiyo wakati na mwaka wenu, mwaka wa Uchafuzi.  Na miye humo nahusikaje!? Simo. 

Nasema kama walivyokwishasema wale waliokuwa kabla yenu, Nguruwe kwake sifa kugagaa matopeni na mimi nakupongezeni kwa juhudi zenu za kuchafuana, na wala siwalaumu maana huu ndiyo muhula wake, muhula wa kuchafuana, ila miye salaam nawasalimia.
Nasema kuchafuana si jambo baya kwenu hasa kwa vile hiyo ishakuwa mila na “visturi” kwenu, ila wacheni basi kutuchezea mahepe na viini macho tena mchana kweupe siye wana wa Mdanganyika Mlipakodi, maana michezo yenu hii mwailipia kwa kodi za Wadanganyika hawa na miye nauliza mwataka kutudangaya mpaka lini!?. 

Ati! Kwani si nawasikia jinsi mlivyo na juhudi katika kututaka na sisi tushiriki kuchafuana kwenye uchafuzi wa  “ ka tiba” kapya ilhali hamjafanya maandalizi tosha ya kutufikisha mahututi siye kwa tabibu!?. Ha ha ha ha ha!!! Na miye nauliza, hivi ‘ka tiba’ haka kanatibu ule ugonjwa wenu uliomuua Maadili wa Mdanganyika  ama ugonjwa unaowaua kila kuitwapo leo wana wa  Mdanganyika wa Mlipakodi!?. Naapa hiki ni kiini macho kwa wazima kupata ‘ka tiba’ ilhali wagonjwa wa umaskini na “si hasa” maji taka wakiachwa wajifie kwa kadri wawezavyo ila simo. Tena simo kabisaaa, sihusiki. 

Haya, niyawache hayo miye ya ‘ka tiba’ kalikomuua badala ya kumtibu Umoja wa Mshikamano wa Mdanyika wa Mlipakodi, japo kusema kweli nakumbuka  bado jinsi tulivyotawanyika msibani bila hata kuanua matanga ati kwa vile sungusungu wa kijiji waliamuliwa wawanyamzishe wote waliokuwa wakilia sana, na ati watakaogoma kunyamaza basi wapigwe tu maana wanapenda kulia.
Nasema huu mwaka wenu tu hata mkatae enyi wana wa Mdanganyika Mlipakodi na japo mwenye macho haambiwi tazama, lakini kutazama si kuona na miye hapa salaam nawasalimia. Ala! Kwani si wenyewe mwajionea vituko vya uchafuzi huu, wakati mnapofukuzana kwenye banda lenu ati kwa vile mmeshindwa kuelewana wenyewe kwa wenyewe, ama kwa vile bwana mdogo ameshindwa kunyamaza akasemea kwenye kashimo kwamba mfalme ana masikio kama popo!?. Ha ha ha ha ha ha!!! Ama kweli si kila ukweli ni ukweli na si kila ulijualo yakupasa kulisema maana ati ulimi uliponza kichwa.  Simo naapa. 

Nauliza ikiwa kumwendesha Farasi kwa kupeni taabu mtaiweza nyie kasi ya Nyumbu ama na nyie mwachafuana tu kwa vile huu nao ni mwaka wa uchafuzi!?. Pole sana wewe mwembamba  lakini mzito kwa uzito wa Tembo. Nasema hili si kosa lako hata kidogo bali ni kosa la Wadanganyika sisi tuliosahau katazo la kumsifia Mgema na sasa umewatukana Mamba ilhali hujavuka mto, ona sasa hasira yao inavyokuchafua. Hata hivyo si mwaka wa uchafuzi!  Chafuaneni tu ila mimi humo simo katu!. 

Nasema mnisamehe ikiwa pamoja na ukweli kwamba ninaumwa, tena hoi bin taabani, bado nachelea kuchafuana kwenye uchafuzi wenu huu wa ‘ka tiba’, japo kusema kweli najihoji, mtafanzaje bila ‘ka tiba’ ilhali mwaka huu kale ka ugonjwa kenu ka kuchafuana kamewaanza tena!?. Ha ha ha ha ha ha!!! Nicheke Chokoraa miye maana kuchafuana ni kama kifafa, mwaujua msimu wake na dalili zake lakini ati mlikuwa na mambo mengi sana mkashindwa kuuandalia ‘ka tiba’ kwa wakati na sasa mwajaribu kuutibu kwa kasi ya zimamoto. Simo naapa. 

Haya, wacha nirudi zangu jalalani nikakusanye mapande ya Boflo kwa ajiri yangu na wadogo zangu na hata Yule mama yangu kikongwe Shida wa Matatizo wa Taabu Maisha Magumu. Naomba chonde chonde, mkiisha kupata ‘ka tiba’ ka ugonjwa huu wa kuchafuana, basi chafuaneni maana nani atakukatazeni ilhali huu ndo msimu wake hasa!  Ila chonde enyi wana msije mkauchafua hata mchezo wenyewe wa kuchafuana ikiwa mtaamua kujiingiza kichwa kichwa kwenye uchafuzi wa ‘ka tiba’ ati kwa vile msimu wa ugonjwa wa uchafuzi umefika, kwani kale ka tiba kalikokutibuni miaka yote kana nini hata mwatumia nguvu ya zimamoto kuzima barafu!!!!!?. 

Wasalaamu, ni mimi ndugu yenu Chokoraa wa Muhangaikaji wa Mlalahoi wa Pangupakavu wa Kabwela wa Mdanganyika wa Mlipakodi nawasalimia, shikamooni Wadanganyika.

1 comment:

  1. naona umejiandaa na mwaka wa kuchafukwa tumbo kutokana na uchafuzi mkuu

    ReplyDelete