Friday, June 28, 2013

"SHIKAMOO" MKULU WA GUNIA.



Shikamoo Mkulu wa Gunia. 

Shikamoo si salaam mwana wa Muhangaikaji  nilikataa tangu zama ila sasa, shikamoo mkulu wa gunia. Nasema shikamoo si kwa kukuamkua maana ningekuamkua ningesema salaam nakusalimia lakini nasema tena kwa sauti ya juu unisikie ijapo kusema kweli akina kaka Muishiwa wamenifungia juu ya dari ya nyumba tena kwenye paa la choo ili nisionekane mbele yako, ila naamini sauti yangu itakufikia ewe mkuu wa gunia hili tambala bovu tuishilo sisi wana wa Adamu, shikamoo mkulu wa gunia. 

Ha ha ha ha ha ha!!! Nimekumbuka zamani enzi zile wakati wazee wangu hasa mama yangu Shida wa Matatizo wa Taabu Malingumu alipokuwa akiniamsha lukwiri ili niende huko kwenye jando la kikoloni kufundwa ujinga wa kuidharau ‘ilimu’ ya babu na babu zangu kwa kuuita ushenzi ilhali tamaduni za mgeni zikiitwa uungwana, hilo si lengo la waraka huu, shikamoo mkulu wa gunia. 

Nakumbuka enzi hizo ikiwa Mkulu wa kaya ama wasaidizi wake walitembelea kijiji chetu, wote tuliambiwa tuoge, tuchane nywele zetu kwa mitindo ya kurithishwa na wakoloni wenyewe ati wakiita ‘kisasa’ bila kuheshimu ukweli kwamba hakuwezi kuwapo na sasa bila zamani na mjukuu ni matokeo ya babu, humu namo simo ila, shikamoo mkulu wa gunia. 

Tulijipanga mabarabarani na enzi hizo barabara zenyewe zilikuwa za vumbi tupu na ole wetu ikiwa ulikuwa msimu wa mvua na siye na shati zetu nyeupe kwa weupe wa mkorogo, letu lilikuwa tope na maji machafu wakati walinzi wa ‘mkulu wa kaya’ wakipita na magari yao na siye tukijitahidi kupunga mikono na kulazimisha tabasamu nasema enzi ni enzi na kumbe historia hujirudi, shikamoo mkulu wa gunia. 

Mkulu wa Gunia, mwana wa wana wa Hamu ndugu wa Shemu na Yafethi kwa mujibu wa misaafu iliyoletwa na wale uwatawalo leo, nimemua kupaza sauti kwanza nikukumbushe japo najua wajua ya kwamba shikamoo humaanisha niko chini ya miguu yako na hilo ndilo ninalotaka kukwambia leo, niko chini ya miguu yako na kusema kweli unanikanyaga. Sikulaumu. Wala! Hata kidogo. Nani kasema nakulaumu? Miye sikulaumu kwa vile kama walivyofanya babu zako ambao walipokuja wageni wenye pua ndefu na tabasamu za unafiki uonekanao kama urafiki, waliwakuta babu zetu wakiwazika machifu mikononi mwa walio hai na waliozikwa hao ati kumsindikiza chifu kwenye safari yake ya mwisho walikufa kwa ujasiri ati kwa vile walikuwa mashujaa na mimi ni shujaa mtukufu mkulu wa gunia. 

Mimi ni shujaa ila si shujaa wako bali shujaa wa kaka Muishiwa kwa vile tangu ulipotangaza kwamba waja huku kwetu mimi niko chini ya miguu yako na hata mkate wa wanangu niliokuwa nimeukumbatia kifuani kwangu nao sasa umesagika kwa kule tu mimi kuwa chini ya miguu yako. 

Ha ha ha ha ha ha!!! Usitake nikutajia jina la marehemu bibi yangu mzaa mama yangu wewe aliyeniambia mbwa mwitu na mbuzi hukaa kundi moja tena bila kuchokozana ama kuogopana Simba anapoingia kichakani na sasa kwa sehemu nasadiki.

Ati! Nasema uji wako kwenye ardhi ya wadanganyika walipa kodi umenikumbusha mambo mengi mojawapo ni mzee yule aliyekuwa mwenye kigoda cha kijiji chetu. Pamoja na kuwa mtu mkubwa sana wa enzi zake lakini hakuwa na shati hata moja lisilo na tobo mabegani na siku moja Mkufunzi alipotembelea darasa lake na kuamua kukagua usafi, yule mzee kwa vile alijua Mkufunzi angekagua mavazi alikuwa amevaa koti zuri juu ya shati lake ila kwa vile mkufunzi alipoamuru huyo mzee avue koti lake ndipo tukagundua kumbe mabega na mgogo vilikuwa wazi. Ha ha ha ha ha ha!!! Nicheke kama mazuri Chokoraa miye. 

 Najua!!! Najua, najua unashangaa kusikia Mkufunzi alitutembelea na kumvua yule mzee shati lake kwenye ukaguzi wa usafi wakati unajua mkufunzi huwa anakagua wanafunzi pekee ila ulichosahau ama kudharau ni kwamba wakati huo kaya yetu yote ilikuwa shule na mkufunzi alikuwa mmoja akituongoza kama Mussa na Israel hayo unayajua kwa hiyo , shikamoo mkulu wa gunia. 

Wacha nikumalizie kisa hicho halafu ninyamaze maana najua akina kaka Muishiwa kwa sasa wamenuna ati Chokoraa nampigia kele mgeni na ndiyo maana ati kwa vile miye siujui ‘ustaarabu’ wamenikataza kuja mjini. Mkufunzi baada ya kumvua koti yule mzee na kumkuta amevaa shati lililochanika akaamuru atandikwe viboko sita pale pale na mimi nikajihoji, kwanini kumtandika mtu aliyejaribu kujiheshimu mbele ya mgeni!? Mkufunzi akanisikia wakati najihoji inawezekana nilijisahau nikawa nazungumza kwa sauti, akaniita mbele. Weeeee! Hukuwapo maana ungecheke sana jinsi nilivyokuwa nikitetema.

 Nilijua leo na miye vyangu sita ninavipata lakini mzee yule Mkufunzi alikuwa heshi visa, ati akaanza kunifafanulia Chokoraa miye ni kwanini alimtandika mzee yule viboko sita. Akasema kwa kitendo cha mzee yule kuficha shati lake lililochanika, mkufunzi angeondoka kijijini ameridhika kwamba mambo yako barabara maana hata mwenye kigoda kava suti kumbe ndani malapulapu na hivyo asingetuma tena “kilimpilini” pale kijijini mwaka huo labda baada ya miaka sita na hivyo aliamua kumtandika kwa vile mwenyekigoda alimficha ukweli wa mambo. Ha ha ha ha ha ha!!! Natamani na wewe mkulu wa gunia ungekuwa na busara ya kujua kilichojificha nyuma ya jiji safi unalolipitia unapotokea kwenye stendi ya mwewe! Lakini waaaapi! Kwani watakwambia!?.

Hata wakikwambia kwani utawafanyaje zaidi ya kuwapongeza kwa juhudi ya kusafisha jiji? Nasema uchafu waliouondoa ni mimi na ndugu zangu akina Seremala, makenika, machine na yule Ntilie, mdogo wake na mama yao Mama Lishe, na miye nauliza, kwani sisi sasa ni takataka kwenye kaya yetu wenyewe ati kwa ajiri ya ujio wako? Naomba kujua unaoga maji ama maziwa!?. Ila bado zijajiinua wasijeniangushia vitu vilipukavyo, bado niko chini ya miguu yako mkulu wa gunia. 

Nasema kumbe ukweli na uwazi ni mchezo mgumu kuucheza na yawezekana wanaohofia na wanachokihofia miye nakijua. Ati! Sikia huyu naye! Ati wanahofia usalama wako? Nani kasema! Hawana mashaka na usalama wako maana kama wao wenyewe tu wako salama iweje wewe na maguvu yote uliyo nayo na ‘utukutu’ uliojifunika nao usiwe salama katika kaya ya amani na utulivu!? Na huyu, ati wanahofia maandamano na si hasa!? Hilo nalo si kweli maana hayo yaweza kutokea popote na vyovyote ila wadanganyika siye hatuna kawaida ya kuwafanzia fujo wangeni kuuana twauana wenyewe lakini mgeni yuko salama.

 Wanachohofia mimi nitakwambia ijapo najua ukiondoka nitakiona cha mtema kuni. Ndiyo, ukiwapo hawanigusi kwa vile, niko chini ya miguu yako. 

Wanaogopa usije ukawauliza zile shekel, noti na mifedha kedekede uliyowapa walete kuboresha maisha ya wadanganyika imefanya nini ikiwa miaka hamsini ati baada ya bendera bado wadanagnyika wanaishi chini ya nusu dola kwa siku!? Nani kasema wanaishi chini ya dola moja? Kwani dola moja si sawa na “si nyingi” zetu harufu mbili! Naapa wako wadanganyika miongoni mwetu ambao wanaamka na kuzitafuta “si nyingi” tamo mia na wasizipate hao wanaishije chini la dola moja!?.  Wanaogopa utawauliza kuhusu magari yao ya kifahari wanayoendesha ilhali mama Ntilie na Machinga hawajui watakula nini na hivyo wanapotuondoa akina siye mjini utakaoukutana nao ni “wao” na hivyo hutojua kundi la akina siye tuko wapi na kuondoka ukidhani na “sisi” ni kama “wao” kumbe pana tofauti kubwa. Natamani kuendelea kusema lakini naonga kama uzito wako unaongezeka na mimi pumzi zinapungua kwa sababu, niko chini ya miguu yako. 


Wasalaam, ni mimi Chokoraa wa Muhangaikaji wa Mlalahio wa Pangupakavu wa Kabwela wa Mdanganyika nakusalimia. Shikamoo Mkulu wa Gunia.

Thursday, May 23, 2013

Kaka Mkulu wa Kaya, Salaam Nakusalimia.



Kaka  Mkulu wa Kaya, salaam nakusalimia,
Nasema kuwa huru si rahisi kama ilivyo si rahisi kuwa rais na sasa Chokoraa nawasalimia. Kubadili majalala huku kuna siku nitaingia kwenye jalala la tindikali naapa kwa jina la bibi yangu mzaa mama yangu Shida wa Matatizo msinihusishe. Nasema msitake niseme kwa mtiririko maana yaliyonijaa kwenye koo ni mengi na njia ya ama kuyameza ama kuyatema ni ndogo na hivyo wacheni niyatapike liwalo na liwe maana ni bora moja kuliko sifuri na humu miye nahusikaje!?. 

Kwani nani kaiona ramani ya kaya yetu, ile ramani halisi ya Danganyika ya Wadanganyika tuliyoachiwa na wazee wetu kabla haijabadilishwa na hawa wenye kujitangazia uhuru kila uchao kisa “uhuru na haki za raia” na mimi nauliza ni nini uhuru na haki za rais na kwa hili mnitoe maana simo. 

Kaka mkulu wa kaya, nimetumwa na wadogo zangu akina Muuza Mayai na Karanga, na hata mama yangu mdogo Mama Ntilie kanituma nikusalimie.  Hawa wawili wanasema wanakumbuka kabla ya kufariki baba wa kaya yetu na kabla ya wewe kuteuliwa na kikao kilichopita cha ukoo kuwa Mkulu wa Kaya na kuongoza kundi la akina kaka Muishiwa wa Maadili na Kiongozi Mbadhilifu katika kuiwakilisha kaya yetu hii, tulikuwa sisi wote ni wamoja watoto wa mzee Mdanganyika Mlipakodi na mama yetu Bi Mzalendo.  

Ati wanasema baada ya kufariki baba yetu, kundi lenu likiongozwa na akina kaka Muishiwa walimpendekeza kaka yenu mkubwa Mtukutu kutuelekeza kule yalikofichwa maisha tarajari ya kaya yetu na ati baada ya siku chache kaka yetu huyu kujitangaza kuwa ‘Mtukufu’ watu wakaogopa lakini kwa vile ati kilikuwa kizazi kilicholelewa vyema na marehemu baba yetu kwa kutohoji yale yafwanywayo na wale wenye kuvaa lile joho lefu la baba na wenzake lenye rangi ya Kiongozi, basi wakakaa kimya. Hata hivyo yale yaliyotendeka ati yalitendeka na hata akina Mlalahoi wakaanza kujenga maghorofa kwa kuuza vitunguu swaumu nisikuchoshe na historia, salaam nakusalimia. 

Baadaye ndipo kijiti alipopewa kaka mkubwa Muishiwa. Wanasema ati huyu naye kwa sehemu alizingatia sehemu ya mafunzo ya marehemu mama yetu Mzalendo binti Mdanganyika ijapokuwa ni kweli kwamba yeye kijiko chake kilikuwa kikubwa maakulini ukizingatia na sisi wengine, lakini walau alijenga daraja na siyo ukuta, nasema nisikuchoshe ila salaam nakusalimia. 

Sasa kuna Yule dada yetu mkubwa ambaye hasa ndiye aliyenifanya nikuandikie waraka huu hasa kwa vile binafsi naweza nisipate nafasi ya kuonana na wewe mwaka huu, si kwa sababu sipendi ama ati kwa vile naogopa wale walinzi wako kama mjomba, lah! Bali kwa vile lile daraja kutoka huku kwetu kuja huko kwenu lina mushkeli kidogo hasa baada ya juzi tu wadanganyika kuchoshwa na kuamua kutenda watendavyo mradi iwe iwavyo, salaam nakusalimia. 

Nasema watu wakichoshwa ni heri ya punda mzee kubeba mzigo yeye na mwana kuliko mtu ama aliyeshiba mema au asiyekula kabisa maana wote huwa na wazimu kwa sababu tofauti na mimi humu sihusiki. 

Dada yetu mkubwa Mjasiriamali ameniagiza nikusalimie na kisha nikueleze kwamba kwake yeye ijapokuwa hapendi hata kidogo jinsi ati unavyotuhumiwa kwa mjomba na shangazi kuwa na sauti nzito kuliko wewe kwenye  kaya yetu, lakini walau alikuwa bado angali na imani na ile “Siri kali” labda kwa vile ilikuwa imefichwa na haikujulikana kwake na hivyo si kwamba aliiamini “Siri kali” bali aliamini kwamba kuna siku na yeye atakuwa sehemu ya wale wenye kuifahamu siri hiyo ifichwayo kwa udi na uvumba na hilo linanifanya salaam nakusalimia. 

Anasema baada ya hivi majuzi watu wasiojulikana kujitangazia mamlaka bila madaraka na kuufunga mji wa Mtwara tena pasina kupata upinzani wowote kutoka kwa walinzi wa “Siri kali”, dada yangu mjasiriamali amejiuliza maswali kadhaa ambayo machache yake amenitaka nikuulize na mimi sasa nakuuliza; Hivi ni kweli kwamba ile “Siri kali” yetu imevuja na sasa kila aliyeko nje anaona ndani kama aliyeko ndaniaonavyo nje!? Nasema usijesema miye sina adabu ninazo tena tele lakini najiuliza inawezekanaje kwamba genge la “wahuni” linafunga mji kiasi Chokoraa wa Muhangaikaji wa Mlalahoi wa Pangupakavu wa Kabwela wa Mdanganyika na hata dada yangu chakaramu Mjasiriamali hatuwezi kutoka ndani na kwenda kuokoteza mkate wa siku? .
Samahani unisamehe, si hoja yangu ya msingi ikiwa ni sahihi kwako kujenga njia ya panya na kupitisha gesi, oil ama mafuta hiyo kwangu si hoja. Nasema yafaa nini mimi kuhoji ikiwa hilo ni sahihi ama si sahihi ikiwa mimi Mdanganyika sina haki wala hadhi ya kuhoji usahihi ama tafsiri ya usahihi wenyewe?.

Kinachonikera mimi na dada yangu Mjasilia ni kwanini na hasa inawezekanaje kwamba ‘watu wasiojulikana’ wanaweza kufunga mji na biashara zake zote na hadi sasa wakawa bado “hawajajulikana”?.   

Ati! Utani wa kuniambia tena ati ni “kundi la wahuni” wanaohatarisha maisha ya wadanganyika wa Ntwara tafadhali tuuacheni maana wahuni hawa sasa wamepevuka mno kutoka daraja la kawaida la uhuni sasa wanaelekea kuwa ‘waahini’ na mimi humo sihusiki. Hivi inawezekanaje kwamba watu ‘wasiojulikana’ ama “wahuni” kama ambavyo baadhi yenu mtataka nisadiki, kwa kutumia ‘vikaratasi’tu  wameufunga mji na biashara zote kusimama?. 

Nasema kwa hili msinihusishe hata kidogo. Haya, ebu niwaze kichokoraa. Hivi wakati ‘tanchi’ la kwanza lilipopigwa, vipeperushi si vilikuwa vimeanza kusambazwa tangu jumatatu na tanchi lilipigwa ijumaa! Nani kasema unahitaji ‘kadigirii’ kujua kwamba hapo katikati kulikuwa na jumla ya siku tatu nzima na jumla ya saa sabini na mbili za kuwasaka na kuwatia ‘mtaroni’ agha! Samahani, kuwatia mbaroni ‘wahuni’ wanaoongoza vitendo hivi!? Hivi siku hizi wale ‘sungusungu’ wako wa kaya nao wamekuwa butu hawana meno kazi yao imebakia kututishia siye vitukuu wa mdanganyika lakini linapokuja suala la usalama wa kaya nao hawajui cha kufanya!? Kama ni kweli wanafanya kazi “araundi ze kloku” kama msemavyo ninyi, nini kilifanya hadi ‘tanchi’ la ijumaa 17 likatokea? 

Ha ha ha ha ha ha ha!!! Nicheke kama mazuri. Kwani hamkujua kwamba kwa kuruhusu watu hawa ‘wasiojulikana’ kuufunga mji siku moja mliwatumia salaam kwamba wanaweza kufunga mji wakati wowote watakao! Haya sasa wameanza kuufunga kila wanapotaka na mimi humu sasa nahusikaje?. 

Haya, hili sasa limekwishatokea. Lakini hivi ni kweli kwamba wale wanaohamasisha vurugu hizi wanatumia maneno matupu kama mnavyotaka niamini miye kitukuu wa Pangupakavu!? Naapa humu miye sihusiki. Nakataa kuhusika maana ikiwa ni uhafidhina wangu ama ni kweli waliyosema wale waliosema kale, basi “maneno matupu hayavunji mfupa” sasa nyie mwaniambiaje ati wanaoshawishi vurugu hizi wanasema maneno matupu yasiyo mashiko!? Sasa mbona mfupa unanjika!? Nitoeni nasema. 

Au mwataka niamini upinduzi  kwa kutumia ‘propara lenye maganda’ kwamba  wadogo zake na Nchumali wa Chipoku ni wachoyo wa ‘asili mali’ zilizoko kwenye ardhi yao ilhali wao wamefaidi za wenzao? Nasema na kwa hili mnitoe. Haya, basi tumieni wingi wa busara mlizojaaliwa na hata tukawaamini kuwavisha majoho mvaayo kujibu walau kwa kiwango cha uelewa wao ni kwanini viwanda vya sangara viko Mwanza, migodi ya Dhahabu iko Geita na Mara na viwanda vya Pamba na Kahawa viko mahala pa mazao hayo lakini vile vya kusindika Gesi vyajengwa huko kwingineko!? Sisemi hamna majibu ya swali hili, lakini yatoeni basi na kwa namna ya kueleweka hili na mimi nisishangae kama ninavyoendelea kushangaa. Bhaaaaa!! Mwanishangaza enyi wana.

Nasema mzaha mzaha hutumbua usaa, au kwa vile ninyi ni wa kisasa mwaamini mzaha mzaha huwafanya watu kucheka na hivyo kuongeza siku za kuishi!? Naapa ninyi ni kizazi cha wenye hekima na mtakapokufa ninyi basin a hekima nayo itakoma na humo nitoeni. 

Haya, nijuzeni na nyie wenye kufunga mji mwamkomoa nani!? Nasema hawa waliishauza nafsi zao na konzi la kifaranga halimuumizi Kicheche enyi wana. Kwani mnadhani ikiwa mmefunga bishara na kuharibu uchumi wenu kwa siku kadhaa ndipo mmeweza kuwakomesha hawa ‘wezi’ wenu? Naapa wao walikwishashiba halali na mlungula kilichowasalia wao ni heshima na uishiwa na labda kesho ya vizazi vyao ambayo wao wanakusudia kuipata iwe kwa kumaliza vizazi vyenu ama kuharibu kesho ya wanenu, basi tumieni busara badala ya mabavu ilhali mli hali dhoofu kwa kula kidogo na kutenda kazi sana. 

Wacha niyamaze miye maana nasikia kaya yetu hii mama mkwe akitembea uchi unaruhusiwa tu kuwaza kwamba mama mkwe yu utupu lakini ukisema hivyo dhambi. Ati! Kwani mnadhani kama kweli mngekuwa mnaitia mafuta bawaba enyi wenye nyumba, zingetoka wapi kele za mlango ijapokuwa kusema kweli haziwakoseshi usingizi!?. Simo nasema. 

Basi kaka yetu, mkulu wa kaya hii ya Wadanganyika walipa kodi. Wacha nikomee hapa nikatafute sehemu ya kuegesha kichwa changu maana lile pagala nililokuwa nikilala juzi na jana mmelibomolea mbali wakati wenye “siri kali” mlipokuwa mkipambana na “wahuni” katika kujaribu kulinda “siri kali” yenu isivuje pasina kujiuliza kinachoivujisha ni sakafu iliyoloa ama tundu kwenye chombo chenye kutunza “siri” yenyewe?. Ama kweli fahari wawili wapiganapo, ziumiazo nyasi na mara hii Chokoraa nimekuwa nyasi kavu kwenye uwanja wa vita vya fahari wa Faru na Sisimizi. Simo.

Salaam Mheshimiwa, ni mimi mdharauliwa wako Chokoraa wa Muhangaikaji wa Mlalahoi wa Pangupakavu wa Kabwela wa Mdanganyika nakusalimia.  

Monday, April 22, 2013

TUKANANENI WAKATI WADANGANYIKA TWALIWA.



Salaam nawasalimia.
Nasema tofauti kati ya jana na leo hutambulika na mwerevu kwa mjinga ni usumbufu na mimi sina haja hata kuieleza tofauti yenyewe maana muda na nafasi havinitoshi, hivyo naishia tu kuwasalimu, salaam nawasalimia.
Ingawa Chokoraa mwana wa Muhangaikaji wa Mlalahoi wa Pangupakavu wa Kabwela wa Mdanganyika nimekuwa mpenzi sana wa kale kamchezo ka kizazi hiki ka kuwa “bize”, kwa hili imenilazimu nikae chini ya ukuta wa pagala hasa baada ya kula kipande cha mkate niliiokota jana, niwatumieni salamu enyi ndugu zangu Wadanganyika walipa kodi. Ati! Wakataa nini kwamba wewe si Mdanganyika ama si Mlipa kodi!. 

Nasema juzi juzi binafsi nimeshuhudia akina kaka na dada ‘Muishiwa’ si tu wakibishana bali nimeshuhudia wakimwagiana mitusi na mara hii siyo tu ya nguoni bali hata ya msalani, mnisamehe.  Nasema ukubwa si miaka wala akili maana ikiwa utaamua kupima akili ya samaki kwa kumlazimisha kupanda mti, utaendelea kuwa mjinga kwa kudhani samaki hana akili na humu mnitoe.  Pia ukubwa si majukumu maana hata mtoto mchanga analo jukumu la kula na kulala na ikiwa atashindwa kulitekeleza vyema basi matabibu wataitwa ili waone kwanini ameshindwa jukumu lake, na humu najitoa. Ukubwa ni kutambua, kukubali na kuheshimu upana na mipaka ya majukumu yako tena kwa uadilifu mkubwa ingawa naapa si hizi uadilifu ni msamiati mpya kwenu nyie wana wa Mdanganyik mlio na umaarufu wa harufu na humu nitoeni. 

Ala! Ati mwataka sasa kwa vile na Chokoraa miye nimeghadhibika kwa kunichafulia shati langu jeusi kwa utomvu wenu wa nidhamu nimwage mitusi ili tufanane!? Sihusiki. 

Nauliza, kwani nyie wenye nguvu ya ukinzani kazi mliyopewa na Mdanganyika ni ipi? Nauliza ikiwa mlitumwa huko kilingeni ili mtumie uwezo wenu wa kukinzana ili mkinzane mpaka na yale yaliyo ya asili yetu kama busara na adabu!?. Nasema kwenye hili mi simo. Kwani hatuwezi kukinzana kwa hoja na hata tukaelewana bila kulazimika kutumia ubabe usio na faida? Si nimeshuhudia baadhi yenu mkitunisha misuli kujaribu kubaki kilingeni baada ya mwenyekigoda kutoa amri ya ‘auti’?.  Nani alidanganya nikadanganyika Chokoraa miye kwamba ati wenye nguvu ya ukinzani basi wanao pia uwezo madhubuti wa kuitumia nguvu hiyo kunitetea mimi na wadogo zangu wale wawili akina Mzembe na Mzururaji?. Si mmechomolewa mjengoni baada ya kupandishwa jazba kidogo na watu wakajipitishia ulaji wao bila hata haraka! Ha ha ha ha ha ha ha ha!!! Kama akili ni nywele basi kumbe ndiyo maana mwenye kigoda wenu naye kaamua kuzitia zake mafuta ya kizungu ili ziwe na mng’aro kwa waonao. Simo humu. Hivi kwani mlichokuwa mkijadili mle ndani ni maonevu mnayotendewa na ‘watwawala” ama mipango ya mapato na matumizi ya kodi ya Mdanganyika mlipa kodi!? Nasema mlipoamua kuendesha gari mkielekea usoni ilhali macho yako kwenye vioo pembe mlinunua shubiri kuitia mahala pa sukari na miye najitoa.

Ha ha ha ha ha ha ha!!! Nicheke kama mazuri mwana wa Kabwela miye. Ala! Kwani hamkujua nyie kwamba wakati jinsi ilipotumika kama kigezo pekee cha kuwachagulia mwenye kigoda, siyo tu makubaliano ya ajira kati yenu na mzee Mlipa Kodi yalivunjika, bali pia mlichumiwa vimbo ya akiba ili iwatieni adhabu pasina sababu wala adabu kwa wakati wake!? Naapa asiyeiona tofauti ya jana na leo kesho yake ina taabu na mimi simo. 

Haya, na nyie wenye kunitawala badala ya kuniongoza najiuliza nini kilikusukumeni na nyie kumwaga mitusi kedekede!?. Wenye ukinzani naweza kuwaelewa ikiwa wanaghadhibika na hata kutupa matusi ijapo kusema kweli sehemu kubwa ya kilichotamkwa ni kile ambacho zamani kiliitwa ‘maoni binafsi’ kwa vile ikiwa ninaamini kwamba ‘mdogo anamtawala mkubwa na nikasema hivyo’ kosa langu ni kuamkia salamu ya mchana ilhali ni asubihi hilo nalo ni ukosefu wa hekima, lakini walau nimekusalimia . Nasema naweza kuwaelewa kwa sababu yawezekana wanataka Mdanganyika mimi mwenye kukasirika nisipige mtu bali kura wakati ukifika wa hasira yangu niwapigie wao badala ya ninyi na hivyo wanchofanya ni kukutieni utomvu wa mashati yenu ‘matukufu’ kwa weupe wa mkorogo ili mchafuke, na mimi nauliza, ilikuwaje basi mkaamua kuyavua na kuyachovya wenyewe kwenye utomvu wa wakinzani wenu!? 

Hii michezo ya kukimbizana na kunguru aliyekwiba taulo lako ukiwa maliwatoni itakuponzeni naapa. Simo.
Hata hivyo si lengo langu kuwakosoeni bali kuwasalimia. Nasema mwisho wa yote binafsi nawasifu kwa ujuzi na weredi mkubwa mliionyesha kwa ama kutiana jazba na kutupana nje ya jengo huku mkiwa mmejipitishia bajeti za kutafuna kodi za wadanganyika bila tafakuri ya kina kwa vile wote mlikuwa kasi kurushiana mitusi na kuzinduka mshapitisha ulaji, na kwa kuwazidi akili Mbwa wa wadanganyika waliokabidhiwa jukumu la kulinda kodi zao hata mkazitafuna huku wao wakiwa bize kupandisha jazba. Ha ha ha ha ha ha ha!!!! Kweli, hamzumgumzi na mbwa na hata wenye mbwa hawana uwezo wa kuzungumza nayi.  Simo humu namo.

Salaama nawasalimia.

Saturday, January 19, 2013

BUNGE LIINGILIE KUPUSHA MGOGORO WA MTWARA




 Wananchi wakiondoka kwa amani kwenye mkutano uliofanyika juzi kwenye viwanja vya Bima ambapo mkutano wa leo umekwisha kwa vurugu..

Kwa sababu dunia imebadilika kiasi cha kuruhusu kila mtu kutoa maoni yake kwa urahisi na uhuru, na kwakuwa matumizi ya mitandao ya kijamii yametengeneza jukwaa pana zaidi kwetu sote kutumia nafasi na vipaji vyetu kuonyesha uwezo wetu, naamini ni kwa sababu hiyo baadhi ya wasomaji wangu japo kusema kweli ni wachache humu mtandaoni wananipa nafasi kubwa ya kusema kwao na hata wakakubali juu ya ninachokisema japo walio wengi wana sifa moja na mimi kwamba sisi ni watu wasio na nafasi huru  za kusema.

Ndiyo maana basi kwa hili nimeona vyema niseme kwa sababu wasomaji wangu hawa wanategemea niwe na cha kusema na kwa hilo Chokoraa nawaandikia. Siwaandikii hili wote mkubaliane na mimi lakini najaribu kwa kadri niwezavyo kupata uhuru wangu wa kusema.

Pamoja na kwamba nimekuwa Mtwara kwa karibu miezi sita sasa, leo nimepita katika mji wa Mtwara ukiwa katika kile ambacho kwangu binafsi kama Chokoraa kimenitisha. Nimeogopa. Nimetishwa na kuamka na kugundua kwamba kumbe Tanzania ile tuliyolala jana, inaweza kuamka ikiwa ni Tanzania nyingine ambayo watu wanaishi kwa hofu na mashaka kiasi hiki?

Mji wa Mtwara ulitanda askari Polisi waliokuwa wamejisheheneza vilivyo kwa ajiri ya kupambana na wananchi wa Mtwara waliokuwa  kwenye mkutano wa kupinga Gesi asilia kuondolewa Mtwara.

Inasemekana maandamano ya leo hayakukusidiwa kuwa maandamano ya fujo bali lengo lilikuwa kufanya mkutano mkubwa ambapo wananchi kutoka wilaya zote za  mikoa ya Lindi na Mtwara wangekutanika kwenye uwanja wa mashujaa ikiwa ni mwendelezo wa kuishinikiza serikali kutokuondoa gesi ghafi Mtwara.

Wakati maandalizi ya mkutano yakiendelea mara umeme ukakatika kwenye eno la mkutano na baadhi ya wananchi wakahisi hiyo ni hujuma kutaka mkutano usiendelee kama ulivyopangwa kwa vile vipaza sauti zisingefanya kazi bila umeme na ndipo kimbembe kilipoanza.  

Wananchi waliteremka mabarabarani na kuanza vurugu na fujo huku wakielekea zilipo ofisi za Tanesco na polisi wakaingia kuwadhibiti, kilichofuata ni milipuko ya mabomu, kurushwa mawe, magogo ya miti kupangwa barabarani na kufunga kabisa mji wa Mtwara. Barabara kuu ya Mtwara ilifungwa kabisa ambapo hakuna gari liliweza kupita barabara hiyo na hata makutano ya barabara eneo la Bima yalifungwa kwa magogo.

Maduka yalifungwa na mji mzima ulikuwa umepooza mnamo wa majira ya saa saba hadi tisa za jioni nilipojichomoa mjini na kuamua kujiridia kibandani kwangu kujificha na yatokanayo.

Si lengo langu kusema juu ya nini msimamo wangu binafsi juu ya hili kwenye makala hii  lakini niseme nilichokiona leo kimenitisha sana. Si kwa sababu nyingine yoyote bali kwa kuwa leo kwa mara ya kwanza (najua wako ambao wameshudia hili mara nyingi) nimeshuhudia barabara zikiwa zimefungwa kwa magogo ya miti, polisi wakiwama na siraha mikononi kukabiliana na wananchi waliokuwa na mawe na fimbo mikononi.

Kauli za waandamanaji wakifananisha mji huu na Libya ni jambo lingine lililonitisha. Wananchi wenye morali walisikika wazi wazi wakisema “Kama Libya…..damu itamwagika sana….” Na wengine kutishia askari Polisi wanaoishi uraiani kuhamishia familia zao kituoni.

Si lengo langu kusema juu ya nini msimamo wangu binafsi juu ya hili kwenye makala hii  lakini niseme nilichokiona leo kimenitisha sana. Si kwa sababu nyingine yoyote bali kwa kuwa leo kwa mara ya kwanza (najua wako ambao wameshudia hili mara nyingi) nimeshuhudia barabara zikiwa zimefungwa kwa magogo ya miti, polisi wakiwama na siraha mikononi kukabiliana na wananchi waliokuwa na mawe na fimbo mikononi.

Kilichonitisha zaidi ni pale ambapo mpaka sasa serikali imekaa kimya bila kutoa majibu yoyote kwa hoja za wananchi hawa na badala yake imeishia kudharau vuguvugu hili huku hali hiyo ikihatarisha usalama wa wananchi na amani ya nchi kwa ujumla.

Mkuu wa Mkoa wa Mtwara ndiye kiongozi mkubwa kabisa mkoani humu ambaye kauli yake kwa wananchi imeibua kero na manung’uniko hata miongoni mwa maafisa wa serikali yenyewe pale alipowaita wananchi hawa ‘wapuuzi’ na wasiosoma.

Nasema kwa hili serikali itoe majibu yanayoeleweka kwa wananchi wake ama bunge lichukue hatua ya kuitana haraka na kuzungumza kuhusu jambo hili ama mgogoro mkubwa utakaobadili historia ya nchi unaweza kutokana na ukimya huu. Ikiwa bunge limekuwa likiunda tume kuchungunza mambo kama pesa zilizofichwa nje ambazo bado kitendawili chake hakikajulikana ikiwa ni kweli au si kweli, basi ni wakati bunge lichukue hatua kwa hili.

Wananchi bado wana imani na bunge lao japokuwa hawana imani na serikali na ni wakati wabunge ambao ndiyo waajiriwa wa wananchi kuisimamia serikali, waamke na kufanya kazi waliyotumwa na wananchi wao.

Kazi hii wala wasiachiwe wabunge wa Mtwara peke yao. Nasema hivi kwa sababu inaonekana wazi kwamba kazi hii imewashinda kwa sababu maneno haya hayakufikia hapa kwa kuzaliwa leo asubuhi na kufikia hali hii bali yamekuwako kwa wanajamii muda mrefu na ikiwa ama wabunge hawakujua kwa sababu hawana ukaribu na wananchi wao ama walijua na kudharau kwamba ni maneno ya hovyo, basi wameshindwa kuwa na uwezo wa kuaminiwa tena na wananchi kumaliza suala hili na hivyo ni wakati Bunge kama taasisi ijiingize kwenye hili.

Wananchi wanachotaka ni kusikilizwa na kupewa majibu kwa hoja zao na kwa kuwa wamepoteza imani na majibu yanayotolewa na serikali, ni wakati kwa ajiri ya amani ya nchi, taasisi ya Bunge ijiingize kwenye jambo hili kuepusha umwagaji damu mkubwa.

Nilipotazama kwamba wengi wa waandamanaji ni vijana wadogo ambao hata hawajawa na familia bado, nikajifunza kwamba hili litakuwa jambo gumu sana kulimaliza kwa ubabe kwa sababu kimsingi vijana hawa hawana cha kupoteza kwa kufanya wafanyao.

Wednesday, January 16, 2013

WADANGANYIKA: "GESI KWANZA, VYAMA BAADAYE". NAHUSIKAJE HUMU MIYE!!!?

Simo. Katika kile kinachoonekana kuwa hasira za Wadanganyika wa mkoa huu wa akina Njomba Nchumari, ntoto wa Chipoku kukataa suala la mtambo wa kurudufu Gesi kujengwa wilayani Kibaha Mkoani Pwani badala ya Mtwara, leo mkutano Mkubwa ulifanyika kwenye viwanja vya Bima na kuhudhuriwa na maelefu ya Wadanganyika walipa kodi na Chokoraa wa Muhangaikaji nilikuwapo kushuhudia hali ilivyokuwa japo simo, tena simo kabisaaaa. Ala!
"Kwa wale wote wanaotaka kumtumia salamu 'Mkulu wa kaya' kwamba wananchi wa Mtwara hawakatai gesi kutoka Mtwara bali wanakataa gesi kutoka ikiwa ghafi inueni mikono juu......". Matokeo yake ndiyo yaliyozaa picha hii. Nimo kwani humu?
 Hivi ndivyo wananchi walivyoonyesha hisia zao kwa 'Mkulu wa kaya' na Chokoraa nauliza; "Mkulu wa kaya unawasikia hawa?" ikiwa utaamua kuwapuuza mi sihusiki tena simo kabisaaaaaa.
Wadanganyika waliweka chini tofauti zao za dini, vyama na hata makabila na hapa kulikuwa na lugha moja tu, "Gesi kwanza, vyama baadaye". Simo naapa.
 Mwenyekiti wa Vijana wa Chama cha Wananchi (CUF) taifa Bw. Ahmad Katani alikuwa mmoja wa wazungumzaji kwenye mkutano huu na moja ya kauli zilizowakuna wasikilizaji wake ni hii "Hata akija mwenyekiti wa CUF taifa Prof. Ibrahim Lipumba na kusema Gesi iondoke, mtimueni.....". Nauliza humu Chokoraa nimo?.
 Hapa Bw. Katani akizungumza na Meza kuu.
"Mimi nimejitolea, naamini hata nikifa kwa kupigania maslahi na maendeleo ya watu nitaiona pepo pasipo shaka yoyote".
 Ilikuwa jioni muda wa watu kutoka makazini na hapa wanaonekana maafisa wa benki ya CRDB tawi la Mtwara wakijadiliana jambo pembezoni mwa uwanja wa mkutano. Simo humu namo.
 Pembezoni mwa barabara kuu eneo la Bima, wananchi wakisikiliza kilichokuwa kikiendelea kwenye mkutano wa CUF "Gesi kwanza vyama baadaye" Nahusikaje humu miye.
Mmoja wa wadau wa chokoraa blog naye alipitia hapa kusikia kisemwacho na wale wasemao na mimi sihusiki humu namo. Simo.
 Ha ha ha ha ha!!! Gheshi ra Porisi, ririkuwepo kuhakikisha usarama wa raia na mari sao". Simo humu.
 Mwenyekiti Ahmad akisisitiza jambo.
 Sehemu ya wananchi waliohudhuria.
Salamu za Pongezi zimetumwa kwa Jeshi la Polisi mkoani Mtwara kwa kutotumia mabavu kwenye mikutano hii ya wananchi na Chokoraa natuma pongezi zangu kwa Kamanda wa Polisi Mkoa Bi. Marry Nzuki. "Hongera Kamanda.