Wednesday, October 15, 2014

Mwaujua Ugonjwa wetu enyi wana!?



Salaam nawasalimia. Nasema tofauti ya mjinga na mwerevu ni ipi ikiwa nilijualo hulijui na ulijualo silijui na ujinga ni kutojua jambo enyi wana salaam nawasalimia. Ha ha ha ha ha ha!!! Nicheke miye! Kwani si mlikuwa mwalalama ati mwataka makubaliano mapya nyie mwaita katiba ya kugawana kaya yenu? Haya, kiko wapi sasa enyi msiojua majira na nyakati hata mwalana na kuraruana mkigombea fito ilhali mwajenga nyumba ileile?. Naapa humu simo. 

Ona huyu naye ati niwachilie mbali viapo kwa vile viapo vyazuiwa na mila za kikoloni pasina kujua kiapo ni ukomo wa uwezo wa mwanaadamu, na mimi katika kukueleweni nimefika ukomo na naapa mwaniapisha enyi wana na miye humu simo. 

Shikamooni Wana wa Haraka Tu. Ndiyo, salaam nawasalimia kwa vile haraka zenu zakuponzeni mwapotea njia mchana kweupe kwa uvivu wa kuuliza na miye humo nahusikaje!?. Simo. 

Ala! Mwadhani ati kwa vile Chokoraa miye hushinda majalalani nikichakura nipate cha kuwalisha vitegemezi vyangu wana wa mama yangu Shida wa Matatizo wa Taabu wa Maisha magumu mke wa mzee wangu Muhangaikaji wa Mlalahoi wa Pangupakavu kilembwe wa Mdanyika Mlipakodi, basi siijui tofauti ya adhuhuri na jioni!? Mwanitania enyi wana na miye humo simo. 

Nasema wachilieni mbali uzandiki wenu ashakumu si matusi ila ikiwa kwenu kuuita uovu kwa jina lake matusi, basi miye salaam nawasalimia. Ndiyo, nakumbuka sana miaka ile ya kipindi kile cha Yule kitukuu wa Nchumali Ntoto wa Chilingi mwana wa Chipuputa mlivyokuwa mkiiandama ‘siri kali’ tena kwa kuivisha koti la chama cha upinde wa zamani, na kudai ati inakataa kuanza mchakato wa katiba na hivyo kuwahujumu wanyonge. Naapa wanyonge wa kaya hii wamekosa msemaji na miye humu nitoeni. Ala! Kwani mwadhani sioni jinsi ambayo kwa Mkwere huyu kukuruhusuni mfanye huo mchakato wenu mlivyowageuza ‘wana wa kaya’ kuwa ngao katika vita yenu ya panzi!?. Nasema msinitanie enyi wana maana miye si babu japo kusema kweli kwenu nyinyi pia si mjukuu na humu pia nitoeni. 

Nauliza maana kuuliza si ujinga, kwani ‘Waishiwa’ ninyi si ‘wana wa kaya’ ati kwa vile tu mko kwenye hilo genge lenu la wahuni wajuao kuvaa mavazi na tabasamu za kikoloni? Kama na nyie ni wana kaya, inakuwaje mwagombana na kila mmoja akidai anatetea maslahi ya Wana wa Mdanganyika wa Mlipakodi? Naapa mwatufanya mazuzu enyi wana na miye humu sitaki katu kuhusika maana simo, tena simo kabisaaaaa! 

Ati! Hivi mwadhani shekeli za baba yetu Mdanganyika wa Mlipakodi mnapoziswaga kama Ng’ombe waendao machinjioni kwa kisingizio cha kutuandalia  ka tiba kaliko bora bila kuufahamu vyema ugonjwa wetu, sisi nao ni wajinga tusioifahamu janja yenu!? Wacheni dharau enyi weledi wenye kwenda mbele ilhali macho yatazama mtokako na miye humu nahusikaje!? Simo.

Haya, mwabishana na kugombana kila mara ati muwe na siri ngapi za kuzitunza pasina kujiuliza hizo mlizokuwa nazo zimevujaje hata kutufikia sisi akina Chokoraa kama mwafahamu kutunza vyema hizo ‘siri zenu kali?’. Naapa ujinga hauna tafsiri na miye humu nitoeni.
Kwani nyie si ndiyo mliokuwa vinara wa kumnukuu Yule mzee mwana wa Mzalendo na hapa namsema Mkufunzi wa Mzalendo wa Mdanganyika, ki wapi sasa kile mlichokuwa mkituaminisha sisi wadharauliwa wenu kwamba “wale” wameasi misingi iliyotiwa na Mkufunzi na “ninyi” ndiyo manabii pekee mliobaki kuirejesha kaya yetu kwenye msingi?. Ha ha ha ha ha!!! Nasema penye pongezi zitolewe na mimi nakupongezeni maana mwauweza vyema mchezo wa ‘si hasa’ isipokuwa izi za mara hii ni zile za majitaka yasiyofaa kwa kunywewa ama kilimo cha umwagiliaji kama mjitapavyo na miye humu simo. Ala! Mlipoona misingi ya huyo mkufunzi mwenyewe inakinzana na tamaa za mioyo yenu, si nilikusikieni baadhi yenu mkimtusi hadharani kama wana wasio malezi wenye kutukana wazazi? Naapa laana mmelaaniwa enyi wana na miye humo simo. 

Nani kakudanganyeni Chokoraa miye na wadogo zangu ukoo wa Mdanganyika Mlipakodi ugonjwa wetu ni idadi ya ‘siri’ zenu!? Kwanza hatutaki hata kuzijua hizo siri zenyewe, ziongezeni ukali hata tusizikaribie kama mwataka, lakini hakikisheni kaya yetu inabaki moja kama alivyoiwacha mwana wa Mzalendo na msipotenda hayo, naapa hatutaiwachia historia kuwahukumu bali tutawahukumuni sisi wenyewe na  miye humo simo tena simo kabisaaaa, ila salaam nawasalimia. 

Ni mimi Mdharauliwa wenu, Chokoraa wa Muhangaikaji wa Mlalahoi wa Pangupakavu wa Kabwela wa Mdangayika wa Mlipakodi nawasalimia. Salaam Waishiwa.  

Friday, January 3, 2014

Mgeni Njoo Mwenyeji Akome.



Salaam nawasalimia. Najua mwaka wa jana umekwenda na najua wengi wenu bado mngali kwenye zile nyumba zenu zenye baridi ya kutengeneza huku mkijituma wengine kuijenga na wengine kuivunja kaya ya wadanganyika na ati bado mwashangaa kwanini jengo halikamiliki. Mwashangaa nini?. Nasema ikiwa walio wengi mnafanya kazi ya kubomoa ilhali wachache tena wenye nguvu chache wanafanya kazi ya kujenga si ajabu itawachukua miaka dahali walau kulifikisha jengo kwenye ‘renta’ ila humo miye simo bali salaam nawasalimia. Shikamoooni Wadanganyika. 

Nisemeje!?. Mwataka nirudie kuwakumbusha madhila yaliyotukuta kwa mwaka uliopita?. Katu. Nasema siendi safari ya maili kumi elfu kinyumenyume asomaye na afahamu ila mi salaam nawasalimia. Jana imepita na kesho si yetu lakini ikitumika vyema leo walau kesho yaweza kuwa na matumaini na miye hapa nawasalimia. Kwa mwaka huu naapa sitasema matukio bali mazoea na tabia zenu maana tabia hutengeneza utamaduni wa jamii na miye nakuulizeni enyi wana  wa Mdanganyika Mlipakodi nani aliyekundanganyeni kwamba kuna kaya nyingine mtakwenda baada ya Danganyika yenu hii?. Ala! Washangaa nini?. Kwani si miye nakuoneni mnavyoishi kama watalii tu hapa kwenye kaya yetu kila mmoja akijaribu kuwa kama wale waliowatawala babu zetu bila kujua kwamba twatofautiana siyo tu ngozi bali mtizamo na miye humu nitoeni.

Ha ha ha ha ha ha!!!! Nakumbuka Mkulu wa Kaya kabla ya ule “Uchafuzi Mkuu” wa mwaka uleeeee ulitukasirisha sisi Wadanganyika hata tukapiga kura na kumpa yeye aslimia zaidi ya thamanini ya ‘kula’ zetu huku tukisahau kwamba tuna zaidi ya asilimia tisini ya familia za kulishwa na ‘kula’ hizo za bwelele, alituahidi ajiira makumi mia na sasa leo twalalama na miye nauliza twalalama nini?. 

Mwaka wa jana Chokoraa wa Muhangaikaji wa Mlalahoi wa Pangupakavu wa Kabwela wa Mdanganyika Mlipakodi nimezunguka majalala yote tangu yale ya uswahilini kwetu kunakotupwa miiba ya dagaa hadi yale ya waishiwa kunakotupwa boflo na mapande ya nyama ati kwa vile yamekaa sana kwenye jokofu yakakosa radha, naapa mwakufuru enyi wana. Kwani mabucha hamkuyaona hadi mwanunua vyakula na kisha kuvitupa kwa kujifanya uzungu usio tija!?. Simo naapa. Kwani msipotupa Chokoraa miye nitakula nini? Lakini walau jifunzeni kumheshimu Mwenyezi aliyekupeni nyie kusaza siyo kwamba mtupe jalalani bali mtupe siye tusio hata na kidogo na miye humo nahusikaje?. Simo.
Nasema katika kuzurura kwangu nimejifunza jambo moja kuu na hapa salaamu nawasalimu wale sungu sungu wa mipaka yetu na wale manyapara wenye jukumu la kusimamia vibarua vya kaya yetu, shikamooni waishiwa. Nauliza, hivi waishiwa nyie mnafahamu  uzito na upana wa majukumu yenu au kwavile kama wasemavyo  wadogo zangu wale akina Mzembe na Mzururaji kwamba kaya imeuzwa basi na nyie mmeamua kuuza na utu wetu? Naapa humu miye nisihusishwe. 

Nasema kuanzia kule kwa akina Ngosha kwenye viwanda vya samaki hadi kwa akina Nchumali kwenye Korosho wadanganyika nyie hamna chenu  ati kisa mnatekeleza sera ya ‘Ukewenzaji’ na miye nauliza mbona ‘Ukewenzaji’ huu mwabakwa nyie na sisikii hata lalamiko?. Ha ha ha ha ha ha!!!!! Ninyamaze miye maana si ajabu mkaniuliza kanituma nani wakati miye ni salaam tu nawasalimia. 

Hivi wakati mlipoamua ‘kubinua na kufisha’ viwanda vyetu vyote tulivyorithi kutoka kwa wazee wetu Waishiwa nyie mliamua kubinua na kufisha hata ajira zetu?. Ha ha ha ha ha!!! Chokoraa miye nimepita na kukutana na wageni wakikaa kwenye majumba ya viyoyozi huku wakiwa hawajui hata kuandika idadi ya mali inayoingia na kutoka viwandani zaidi ya utaalamu wa kujua kuvaa na tabasamu za kikoloni na ujasiri wa macho wa kuwatazameni usoni mnaposhikana mikono kusalimiana na miye nauliza, hivi hakuna kati ya Wadanganyika wataalamu wa kufanya kazi hizi hadi mwatuletea wataalamu “feki” wenye kujua tu tabasamu na “hendisheki” ilhali utendaji wote wafanywa na akina “sabani” asomaye na afahamu?!!! Simo humu. 

Nani hakumbuki jinsi ambavyo kwenye migodi ya dhahabu kulikuwa na wageni waliokuwa wakiitwa “sekyurite sipeshialisiti” ati kwa vile wanatokea Unepali ilhali kwao walikuwa makplo na masajenti huku makapteni na maluteni wetu wastaafu wakisota mitaani kutafuta ugali wa kulisha watoto!? Naapa historia inajurudia na miye humu simo. 

Bado kidogo. Sijamaliza, naomba kuuliza wakati “wakewenzaji” hawa wanapoleta msururu wa “wataa haramu” hawa na kuwavusha kwenye stendi za mabasi ya hewani, wanawaeleza wataalamu wetu wa uhamiaji kwamba wanakuja ‘kuisaidia’ kaya yetu kwa lipi?. Au ndiyo yale yale ya kiazi kuitwa kwa lugha ya kitaalamu “potato”?!!!!. Naapa sihusiki.  Haya, endeleeni na michezo hii ya mbuni ya kuficha vichwa mchangani ili mkirudishe kizazi chetu kwenye ukoloni kule ambako babu zetu walipigana kufa na kupona kututoa sisi halafu na nyie mtakapolala na baba zenu mkiiendea njia ya watu wote mkumbukwe kama wasaliti wa juhudi za wazee wenu na miye humo nisihusishwe maana simo tena simo kabisaaaaa, sihusiki. 

Haya, na nyie mjiitao wakulu wa kazi na ajira wa kaya yetu, mmeshindwa nini kutengeneza torati ya kulinda ajira za wadanganyika wenzenu na kuzisimamia?. Ha ha ha ha ha ha!!!! Najua, najua mwaniona mjinga kwa vile wadogo wakisimamisha pembe wakubwa wapewa bahasha na mambo yanakwisha na miye humo nahusikaje? Lakini niseme miye nisijehukumiwa na kizazi kijacho kuwa mnafiki maana najua kama mungetaka kuyatenda yawapasayo yangetendeka lakini hiyari yashinda shuruti na miye humu nahusikaje?. Simo naapa. 

Haya, leo akina "Sabani" wamebaki kufukia hivyo "vidigirii" chini ya magodoro ya bibi zao huku wakipika chai na kufagia na kisha kwenda kufanya kazi za taaluma zao ili kuwafurahisha "mabosi" wasiojua hata kusoma na kuandika lakini wenye vibali halali tena vya kufanya kazi za taaluma kwenye kaya yetu na miye humu nahusikaje maana simo. Nauliza katika kutembea kwenu kote huko mwendako mmeshindwa kujifunza kwamba kaya za wenzetu hata kabla hujaenda wanakupima hata magonjwa wajiridhishe juu ya usalama wao na watu hao?. Nani aliyekurogeni enyi wana wa kushi?. Simo naapa. 

Ni mimi ndugu yenu Chokoraa wa Muhangaikaji wa Mlalahoi wa Pangupakavu wa Kabwela wa Mdanganyika Mlipakodi nawasalimia, Shikamooni Wadanganyika Walipakodi.

Wednesday, October 9, 2013

Wana Haraka tu!!!!!!!!

Salaam nawasalimia. Karibuni kwenye kilinge cha Chokoraa enyi Wadanganyika wana wa Mlipakodi mnisikize kaka yenu Chokoraa mwana wa Muhangaikaji, maana niyaonayo miye huku majalalani yatosha kunitia fahamu na kutaka salam kuwatumieni, Salaam wadanganyika. 

Ukiamka asubuhi huku tumbo lakusumbua, usikimbilie kupiga ramli ama kufakamia kikombe cha babu bali tafakari ulichokula jana yake na hiyo ndiyo busara enyi wana, salaam ndugu yenu Chokoraa wa Muhangaikaji wa Mlalahoi wa Pangupakavu wa Kabwela wa Mdanganyika Mlipakodi nawasalimia.
Ati!. Wakataa nini? Kwamba wewe si Mdanganyika ama si mwana wa Mlipakodi!?. Ha ha ha ha ha!!! Nicheke miye kitukuu wa Kabwela maana nijuavyo Wadanganyika nyie sasa mwahoji hata asili ya mzazi wa mzee Utaifa wa Uzalendo wa Uadilifu na miye humu nahusikaje!?. Ndiyo, kwani siku hizi si Wadanganyika wote wamekuwa ‘wana haraka tu’?.  

Nani alinidanganya nikadanganyika Chokoraa miye kwamba harakaharaka haina Baraka maana siku hizi ati mwauthamini zaidi msemo ule kwamba ngojangoja yaumiza matumbo pasina kutafakari kwamba ‘haraka tu’ zenu za kula hata visivyoliwa na wazee wenu kabla yenu, ndiyo sababu ya matumbo yenu kukusoketeni na wala si subira yenye kuvuta heri iliyo chanzo cha mgogoro wa matumbo yenu!?. Naapa humu miye msinhusishe maana simo. 

Siku hizi ati kila Mdanganyika ni ‘mwana haraka tu’ na miye nauliza, hizi haraka zenu zakupelekeni wapi enyi wana mbona mwanishangaza!. Nasema mapema ili yatokeapo msijenihusisha mchakuraji miye maana miye yangu majalala huku nikichakurachakura nione ikiwa nitapata kipande cha boflo nipooze njaa ya tumbo langu. 

Ama kweli kusoma kwingi si kujua mengi bali maisha ndiyo kipimo cha akili kama walivyosema wale waliokuwa kabla yangu miye mwana wa Muhangaikaji. Najiuliza hivi mbona kila siku kwaibuka ‘wana haraka tu’ na mbona wote waibuka kunifunda kudai haki na hakuna kati yenu awekezaye muda walau kiduchu kunifunza wajibu!?. Nani alikudanganyeni kwamba haki huja bila wajibu wenyi wana mbona mwapotea njia mchana kweupe kwa uzembe wa kuuliza?. 

Haki ya mtoto, haki ya mwanamke, haki ya kichaa, haki ya mlevi, haki…. na miye nakuulizeni haki zenye kuja bila wajibu mwayajua madhala yake nyie?. Ha ha ha ha ha!!! Oneni sasa mnavyolalama kwamba ati Yule mzee wa siku nyingi wa kaya yetu almaarufu Maadili ya Mdanganyika yu taabuni kama si taabani. Mwalalama nini ikiwa mmeshindwa kujua kwamba hamuwezi kuendelea kumlisha mzee huyu sumu iliyomuua Maadili ya Wageni na mkataraji ati kwa vile huyu na yule wafanana majina tu lakini si ndugu basi sumu itageuka kuwa dawa kwenu!?.  Simo nasema. 

Nasema ijapo mtasema wajuaje weye tofauti ya uchafu na chakula bora ama dawa na sumu kali ilhali wala majalalani na kulala mitaroni lakini nasema hekima si kama pesa kwamba ukiwa nayo yakutia kiburi na dharau na maneno ya mwenye hekima ni bora ijapokuwa hekima ya maskini haithaminiwi na hata maneno yake hayasikizwi na ndiposa nawasalimu, shikamooni Wadanganyika. 

Haya, nakumbuka wakati wa kukua kwa wadogo zangu wale akina Mzembe na Mzururaji na hata mimi kaka yao Chokoraa wa Muhangaikaji, fimbo ilikuwa ufunguo uliiondoa ujinga kichwani mwa mtoto lakini sasa mwasema ni haki ya mtoto kutopigwa bali ipigwe ngoma na miye nakuungeni mikono na miguu yote, lakini wacheni kulalama basi ikiwa heshima ya juzi na jana zina tofauti maana hiyo ni haki ya mwendawazimu peke yake. Ala! Kwani si haki ilipaswa kuja na wajibu!?. Nasema ikiwa mwanifunda tu juu ya haki yangu na kudhani wajibu wangu nitaufahamu ikiwa tu nitapewa haki yangu, jiandaeni basi kwa madhila ya kizazi cha nipe nipe maana ndivyo mtakavyo na miye humu nahusikaje!?.  
Ati! Wengine mnalalama ni kwanini kila mkirejea majumbani mwenu mwakuta ‘ndoo’ zimevunjika na sasa vijana hamzitaki hata ‘ndoo’ zenyewe badala yake mwanunua mabeseni ya karatasi ambayo mkiishaogea mwayatupa huko huko maliwatoni!?. Mwalalama nini!?. Kwani mlipoamua kutangaza haki na usawa kati ya jinsi zenu bila hata kufafanua yale yapasayo kuwa sawa na yale yasiyopasa na badala yake mmeifanya jamii yote kuwa na watu wenye maumbile ya Adamu na Hawa lakini wenye kufikiri kama Adamu tu mlidhani madhara yake nini!?. Nasema chakula cha fahamu ni maneno na mifano na kile wanachokisikia wanenu na kukuoneni nyie mkitenda ndicho watakachotenda na wao kwa juhudi kubwa kuliko watangulizi wao na miye humu mnitoe maana simo. 

Wacha nikomee hapa hadi tutakapokutana juma lijalo kwenye kijiwe hiki, wacha nijaribu kumeza vipande vya boflo hivi na maji ya chumvi ila salaam zangu zikufikieni enyi Wadanganyika.
Wasalaam, ni mimi ndugu yenu Chokoraa wa Muhangaikaji wa Mlalahoi wa Pangupakavu wa Kabwela wa Mdanganyika, nawasalimia. Shikamooni Wadanganyika.

Tuesday, September 3, 2013

Salaam Mkulu wa Sungu Sungu.



Nimepata ujumbe  unasema nijihadhari na haya ‘matakataka’ yangu niyamwagayo  kwenye milango ya majumba ya ‘waishiwa’ maana ati yanatoa harufu mbaya yenye kuwakela waishipo kwenye mahekalu yao hayo ambayo ati nayo wameyapata si kwa halali. Nimekusikia ndugu yangu  na ndiyo maana sijathubutu kwa karibu majuma kadhaa sasa kupita mitaani kwao ila leo nimelazimika kuja kumsalimu mkulu wa sungusungu wa kijiji, mkulu salaam nakusalimia, shikamoo mkulu wa sungusungu. 

Wanasema ati wewe umetumia muda wako mwingi tangu ulipotoka pale kwenye jando la kijiji lililoko Mlimani, ukiwa nje ya kaya yetu  hii ati tena ukifanya kazi na wale wenye rangi nyeupe na kutudanganya siye kwa tabasamu na hivyo mkulu wa kaya alipokuteua wewe kuwa mshika “manati za ndhungu” mkuu wa kitengo hiki cha sungu sungu, Wadanganyika walipakodi walikuwa na matumaini makubwa na wewe lakini ati kwa kadri siku zilivyokwenda sasa Wadanganyika hawa hawa wanawaogopa vijana wako kiasi wewe hawakuogopi bali wanakuabudu na humo miye simo maana nimekuja tu kukusalimu, shikamoo mkulu wa sungusungu. 

Ndiyo nasema na wewe mtoto wa mtu Mwema ambaye kwa wema wake alikutuma wewe kwenye jando la kijiji ili ukiisha kuyapata mafunzo ya jando  uje tena hapa kwenye kaya yetu utusaidie sisi watoto wa mzee Mdanganyika Mlipa kodi na ati vile visenti vilivyokupeleka wewe jandoni vilikopwa kwa baba yetu mzee Mdanganyika  wa Mlipa kodi na ndiyo maana miye nakusalimu, shikamoo mkulu wa sungusungu. 

Ngoja! Nielewe na uniamini  ewe mwana maana sina dhihaka hata kidogo nisemapo “niko chini ya miguu yako” kwa vile ni kweli unanikanyaga na wala siwezi hata kujaribu kujiinua maana ni bora unikanyage wewe kuliko nidunguliwe na ‘manati’ za vitegemezi vyako na humo miye unitoe maana simo. 

Kinachonitisha miye si kule kujua kwamba hata salaam hizi zaweza ama kupelekea miye kudunguliwa na manati za ndhungu zilizo mikononi mwa vitegemezi vyako ati kwa vile miye “nimewakosea adabu” sungusungu wa kaya yetu, lakini nasikia ati huko uliko wewe mkulu wa sungusungu mumeanzisha mchezo wa kuoshana maji moto mkibabuana sura kama mwataka kutengeneza staftahi kwa sura za wenzenu na miye humo msinihusishe maana simo. 

Wacha niliseme hili walau niondoe funda lililonikaba kooni maana uhai naupenda na uzima kuliko maradhi lakini uhuru wa kweli huja kwa fikra sahihi na hizo huja kwa lugha sahihi na miye humu sasa nahusikaje?. Aala! Usinitanie. Nasema mzaha wako utatumbua usaha we mwana sikiliza Chokoraa nikueleze yaliyo ya kweli maana unajua yaliyokuwa kwa wale waliokuwa kwenye kiti chako kabla yako na jinsi ambavyo leo hawana heshima isipokuwa nyumbani kwao na hivyo limetanguka lile lililonenwa na manabii kuwa nabii hana heshima kwao, ama hawakuwa manabii na hivyo haliwahusu hilo la nabii kukosa heshima kwao. 

Nani hajui kwamba zilikuwa enzi katika kaya yetu hii hii ambazo watu ati alitumwa tu binti ‘fatuma’ akavunja malango ya watu na wafuasi wakanyang’anya mali na uhai!? 

Hayo sasa yamepita na sasa mwamwagiana ‘mtindi mkali’ na humu miye sasa nahusikaje!?. Simo naapa. Nasema Wadanganyika sasa wamehama makwao wanaishi nyumba za jirani yao Yule mzee mwenye sura mbaya Hofu wa Uoga ati kwa vile kuishi kwao uwaogofya sana hadi wamezoea kuishi “na” kama si kuishi “kwa” Hofu na ndiyo maana miye salaam nakusalimia. 

Nasema ingawa umewapunguzia mzigo wadogo zangu wale wawili Mzembe na Mzururaji wenye  umaarufu wa harufu na hata majina yao siyasikii yakitajwa sana kama ilivyokuwa kwa watangulizi wako, lakini ati kaka yangu Machinga wa Muhangaikaji siku hizi ndiye amechukua zamu ya kusumbuliwa, na ati wadanganyika wanadai imekuwa sawa alivyosema Mkufunzi enzi za uhai wake kwamba ati ‘siri kali’ ikiishakuwa imetoboka inavuja basi hubakia kukimbizana na vijitu vidogo mabarabarani, kwa vile akina kaka mkubwa Mstahiki wa Mtukuka huwa ati wewe na vijana wako mwaogopa kuwagusa kwa vile watakataa “kuja” ila miye humo simo. 

Nasema mimi jina langu halisi ni Chokoraa wa Muhangaikaji naomba msinifananishe na wale vijana wawili wa mzee Si Hasa akina Mchochezi na Mropokaji ingawa tumekua pamoja ila mwenzao  majalala yamenifunda kuwa na adabu ndiposa mkulu miye nakusalimia, shikamoo mkulu wa sungusungu. Sisemi, ndiyo, sisemi kwamba akina mzembe na mzururaji na hata kaka yangu Machinga wa Muhangaikaji wanaruhusiwa kukosa adabu ati kwa vile akina kaka Mstahiki na hata Yule kaka yetu mkubwa Muishiwa wa Mbadhilifu wanaukosea adabu msaafu na mafunzo ya kaya yetu, lakini nasema imekuwaje hata imekuwa kwamba nyie wenye kuijua siri ya mzazi wa Amani bi Haki binti Wajibu na nyie mmekuwa ndumilakuwili mkiufuata msemo wa waswahili kwamba haja kubwa ya ng'ombe mbolea ya bata uchafu!?. 

Haya, nasikia sasa si salama hadi kwenye viota vyenu wenyewe na miye nasema hivi na nyie mlishiriki kula pesa ya sanda ya marehemu Uadilifu hata mkasababisha mzee yule kuzikwa pasipo sanda!?. Ha ha ha ha ha ha ! Nicheke miye maana ikiwa na nyie mlio na taa haramu ya kumulika ili wengine tuone mwatembea gizani kwa uzembe wa kuitia kandiri mafuta, itakuwaje basi yule mama yangu bi kikongwe Shida wa Matatizo wa Taabu wa Muhangaikaji!?. 

Naona kama muda unaniishia nachelea nisikute paka na mbwa wamemaliza vile vilivyotupwa jana jalalani ndiyo maana nakuomba uniruhusu tena juma lijalo nije nikuletee ujumbe nilioagizwa na dada na kaka zangu watoto wa Mdanganyika. Ndiyo, nitakuja tena kwa ajiri ya kukuletea salaam baada ya kuuguza vidonda vya mkong’oto niliopokea kutoka kwa vijana wako nilipojaribu kuukaribia mlango wa afisi yako ili nikusalimu. Mmoja wa vijana wako aliponiona ati akaniita jina si langu eti “we kibaka, watafuta nini karibu na Muishiwa Mkulu wa Sungusungu?”, ile kujaribu kujieleza kwamba miye ni Chokoraa wa Muhangaikaji na si Kibaka, kidundo nilichoambulia ukichanganya na uzito wa ujumbe nilio nao kutoka huko kwetu, ndiyo maana sauti yanitetema nizungumzapo ingawa nina hakika salaam zitafika, salaam nakusalimia. 

Ni mimi mdharauliwa wako, Chokoraa wa Muhangaikaji wa Mlalahoi wa Pangupakavu wa Kabwela wa Mdanganyika wa Mlipakodi nakusalimia, shikamoo mkulu wa Sungusungu.

Thursday, August 22, 2013

Pole kwa Msiba Muishiwa Mkulu wa Kaya.



Salaam nakusalimia. Hizi ni Salamu kwako wewe, ndiyo wewe mkulu wa kaya ya Wadanganyika walipa kodi kutoka kwangu Chokoraa wa Muhangaikaji wa Mlalahoi wa Pangupakavu wa Kabwela wa Mdanganyika nakusalimu, Shikamoo Mheshimiwa. 

Nasema tena kama nilivyowahi kusema hapo kabla kwamba shikamoo si salaam bali mazao ya ukoloni mkongwe lakini wacha niitumie kwako kwa vile hasa ni ukweli usiopingika kwamba niko chini ya miguu yako, shikamoo Muishiwa, aha! Samahani, shikamoo Mheshimiwa. 

Nataka , nimesema nataka wala siombi maana Chokoraa miye sifungwi na ‘proto kali’ ninapotaka kuzungumza na mkulu wa kaya yangu kwa vile yaliyonijaa moyoni ni mazito maana yanatishia heshima ya Mdharauliwa miye kwako wewe Mheshimiwa sana mkulu wa kaya yangu na hapa salaam nakusalimia. 

Hivi! Kwani heshima ni kitu cha bure kama wasemavyo waswahili wa Danganyika yetu!? Si kweli. Naapa ni uongo kuniambia ati heshima ni kitu cha bure maana nijuavyo miye mwana wa Muhangaikaji heshima hulipiwa gharama kubwa ya juhudi, utu, kujituma, kutenda mema na kutumia nafasi na vipawa ulivyojaaliwa na mwenyezi  na pia kuaminiwa na wadanganyika wenzako kwamba waweza kusema na hata kutenda kwa niaba yao na hapa salaam nakusalimia. 

Wala! Wala usinichukulie miye mwana wa Mdanganyika kuwa mmoja wa waungaji mkono wako mbumbumbu ambao hawawezi katu kukwambia ukweli pale unapovurunda katika kutenda yale tuliyoyakasimu kwako kutenda lakini pia si mnafiki miye kitukuu wa Mlalahoi wa kutokusifia unapotenda zaidi ya nilivyotaraji. Nimesema unapotenda zaidi siyo unapotenda kwa kiwango tarajari na humu sasa najitoa maana simo. Nasema kwangu kama unayo masikio ya popo basi yafunike maana ikiwa nitayaona nitasema hadharani kwamba mfalme ana masikio kama popo. 

Hilo si lengo la waraka wangu leo hata hivyo hizo zilikuwa salaam tu na kusalimia mkulu wa kaya ya Wadanganyika Walipa Kodi. Leo ninataka kukueleza kuhusu Heshima ya Mheshimiwa wewe ambaye Mdharauliwa miye ili nikufikie na kukusalimu ni lazima kwanza nitambae mwendo mrefu nikijiangusha chini kila baada ya hatua kadhaa ati kwa vile heshima siku hizi ni shikamoo, basi shikamoo Mheshimiwa.
Nasema ni juzi tu hapa Yule Mnyarwanda alikutupia matusi ya nguoni kwa kumshauri jinsi ya kuishi vyema nyumbani kwake ati kwa kisingizio cha kwamba unaingilia mambo yake ya ndani ilhali kila anapogombana na mkewe wewe ndiye unawapa wanae malazi na chakula. Nadhani huyu ameifanya hii kuwa mbinu ya wewe kumlelea wanae na hii si hoja yangu lakini ni sehemu ya salamu, shikamoo Mheshimiwa. 

Kilichonifanya nikuandikie leo ni kukupa pole kwa msiba, msiba mzito wa walinzi wa kaya yetu hii ya wadanganyika walipa kodi nasema kwa hili wakati ninapoandika Chokoraa machozi yanilengalenga. Silii kwa sababu ya msiba wenyewe maana twafwa sote tu kama upepo upitao na kwenda zake na siku zetu si nyingi juu ya dunia gunia letu hili lakini kinachonisikitisha ni mazingira yenyewe ya vifo vyao.
Najiuliza ni wapi ulipochorwa ule mstari mwekundu unaoweka tofauti kati ya amani na vita na ikiwa kwa hili mstari huu haujavukwa maana mbele naona giza, ila bado nakusalimu, shikamoo mheshimiwa.
Hivi hawa wanaopigana na kuuana kila kuitwapo leo “watwawala” wao si wameamua kwa makusudi kuwateketeza vijana wao walio matumaini ya jamii yao kwa maslahi binafsi hadi pale walipokuja kushtuka maji yashazidi unga na wakaomba kuwapo kwa msaada kutoka kwa jirani?. Ndiyo, na sisi tukawatumia wajumbe wa amani na nani alisema ni mjumbe hauawi!? Naapa aliyenena hili ama alitudanganya au tulijidanganya wenyewe kwa kumsadiki maana wajumbe wa amani wameuawa kwenye uwanja wa vita na mimi nasema huu ni upuuzi. 

Ndiyo. Ni upuuzi kumtuma mwalimu darasani bila chaki wala kitabu ama mkulima shambani bila jembe au hata Chokoraa jalalani bila mfumo wa Rambo asomaye na afahamu na sasa ndugu zetu hawa wamekwenda. 

Ndugu zetu hawa wamekwenda tena walio wengi wamekwenda na ndoto zao, na matumaini yao ya kesho yamezimika na hata wale waliobaki nyumbani ambao matumaini yao yalifungwa kwa hawa basi hawa waliokwenda wamekwenda nayo na itawachukua waliobaki miaka kama si dahali kujenga matumaini mapya na kama ilivyo kovu alisafishwi kwa sabuni likaisha, hawa wamekwenda. 

Kinachonifanya nikuandikie siyo tu kukupa pole bali kukutaka ujivike wewe viatu vya wale waliobaki nyuma ya hawa waliokwenda na ambao siku za usoni pia watakwenda kama ambavyo pia mimi na wewe tutakwenda hiyo njia ya watu wote lakini kwa sasa tuvae viatu vya walio hai maana waliokwenda wamekwenda na hakuna njia ya kurudia huko waendako watu wote. 

Najua, najua utataka kutumia tena busara kwenye hili na hapa mwana wa Muhangaikaji naomba nijitoe maana simo. Ala! Kwani si nimeona tangu umekalia kitu hicho jinsi ambavyo matumizi ya busara yamezaa hasara nyingi kuliko faida ama wataka nikukumbushe kidogo!?. Haya, ebu kumbuka wale walioanza kuhubiri upuuzi wa kipuuzi na kutugawa kwa misingi ya dini, kwani habari hizi hazikufika mezani kwako kwa wakati na ukaamua kutumia busara kukabiliana nao!? Ona sasa tulipofika ambapo hata majalalani Machokoraa twaulizana dini kabla ya kupeana kipande cha boflo na wali uliolala ukatupwa asubuhi. Humu namo simo. 

Tazama, tazama jinsi ambavyo wale waliotuhumiwa kwa ufisadi mkubwa na wakathibitika ulivyotumia busara ya kuwataka warudishe walichoiba badala ya kufichua mwizi na kumwadhibu kwa kadri ya miiko na vijiko vya kaya yetu na mwisho wa siku ni hao hao waliotangaza ati wewe ni dhaifu na hasira zikawapanda wale walio na ngazi za kupandisha hasira hizo miye nikajitoa kama ambavyo hata sasa najitoa. 

Ona jinsi ambavyo ati baada ya fedha kedekede za wadanganyika kutumika kununua Rada na hawa wadanganyika tukatakiwa kula nyasi kama Mbuzi kwa ajiri hiyo bado wanyama wetu walipakiwa kwenye dege tena la kijeshi na kurushwa nje ya kaya yetu na hata sasa bado imetumika busara. Sitaki kusemea wale walioua waandishi na wengine wengi na madhila ya kila leo yawapatayo wadanganyika ilhali wewe mkulu wa kaya ukiwa unaendelea kutumia busara. 

Leo sicheki, nasema sicheki kwa vile nina huzuni na hasira maana nakumbuka kuna wakati wako walioomba ati uwe mkali walau kiduchu tu ili heshima ya uheshimiwa ilindwe lakini naamini hata hao nao ulitumia busara kutowasikiliza kama ambavyo unatumia busara kuwaachilia wale waliokuwa kituoni na wenye wajibu wa kulinda raia na mali zao wanapovamiwa na kuibiwa na hata sasa bado busara ingali inatumika na ndiyo maana najitoa. 

Nakuandikia nikuombe kwa hili muishiwa, aha! Nisamehe, mheshimiwa sana mkulu wa kaya ya Danganyika ya Wadanganyika walipa kodi usitumie busara hata kidogo. Nasema si sahihi kuwa sahihi mara zote maana hilo humaanisha kwamba ustaarabu kwa mpumbavu huonekana kuwa uoga na ndiyo maana hata wale tuliowale na kuwalisha leo wanatutukana na wewe unatumia busara ilhali matusi yao hayaishii kwako tu maana shati ulilovaa kipande chake nimevaa mimi na wadogo zangu wengine watoto wa baba yetu Mdanganyika na hivyo utomvu wao wa nidhamu watuchafua wote japo kusema kweli wewe wachafuka sana maana uko hukoooo mbele yetu. 

Kwani hatuwajui wakuu wa hawa wauaji waliowaua vijana wetu? Wako wapi akina Sikamona na wenzie ama waliishia tu kwenye mawazo ya akina Mtobwa na hivyo Danganyika yetu haina tena mashujaa wa Salaamu toka kuzimu ili wawapelekee salamu wajinga hawa kwa ujinga wao wa kuwaua wajumbe wetu wa amani ilhali wanajua fika mjumbe hauawi!?. 

Nasema ni wakati sasa vijana wetu wavuke mipaka wakawatafute wahalifu hawa na kuwaleta hapa kwenye kaya yetu ili tuwakalishe kwenye ule mbuyu mkubwa na kuwazodoa kwa mawe na maembe mfu na ujumbe ufike kwa jirani kwamba kila atakayemgusa Mdanganyika pasipo kuzingatia taratibu atazodolewa. 

Nasema sisi kwa sisi tugombane na kuumizana maana mwanao ukimpiga mwenyewe unajua kiwango cha adhabu lakini anapopigwa na jirani huna budi kujua sababu vinginevyo umeshindwa kuwa baba na kumfunda mwanao kuwalinda wanawe baada yake na humu miye simo ila salaamu nakusalimia.
Nasikia umemtumia salaam mkulu mwenzio wa kaya ya jirani afanye “haraka” kumtafuta nyoka aliyeuma vijana wetu maana yumo humo ndani mwake na kwamba ikiwa atashindwa kumpata “haraka” basi utawatuma vijana wako kumkamata mwenyewe huyo nyoka na Chokoraa nauliza tafsiri yako ya “haraka” mara hii inamaanisha nini !!?. 

Ni mimi Mdharauliwa wako, Chokoraa wa Muhangaikaji wa Mlalahoi wa Pangupakavu wa Kabwela wa Mdanganyika  Mlipakodi nakusalimia. Shikamoo Mheshimiwa.