Saturday, April 16, 2016

Mwashangaa Fatu kupigwa! Mwashangaa nini!?



Salaam nawasalimia! Najua wako baadhi yenu ambao mmepita kijiweni kwangu mara nyingi na kunikosa na hata wengine nasikia walishakula wali wa hitima. Si makosa yenu, ila miye salaam nawasalimia. Nasema sionekani kijiweni si kwa sababu sipo ila kwa sababu hamnioni. Labda pia sipendi mnione maana si siku hizi hata upele mwaita jipu na kila mmoja atafuta kuonekana tabibu na anaweza kutumbua! Nani kakwambia na miye jipu! Naapa mwanitafuta ubaya enyi wana na miye humo simo ila salaam tu miye nawasalimia. 

Ala! Kwani mi si nimekuwa nakuoneni tu tangu mlipomaliza ule mchezo wwenu kichaa jinsi ambavyo nyote mmehamia huku kwetu ‘bize’ mkimwagiana “majitaka” ilhali mwajua fika kwamba muda wa kuchafuana ushakwisha!?. Haya, endeleeni kumwagiana majitaka tu midhali si mtindi mkali, lakini nawaapia enyi wana msipokubaliana kutokukubaliana na mkasonga mbele hata kama kwa mwendo wa Kobe, huko mwendako nachelea mtaanza tumbuana wenyewe kwa wenyewe ila miye humo nahusikaje! Simo naapa. 

Leo miye nimekuja tu huku mjini kwenu mara moja  kumletea salaam za heri Mkulu wa kaya ya Wadanganyika walipakodi; ikiwa heri ni kunyamaa usinene yale wasiyopenda kuyasikia akina kaka mkubwa Muishiwa wa Mdanganyika wa Mlakodi, , salaam nakusalimia. 

Muishiwa sana Mkulu wa kaya yetu, miye ni yule nduguyo Chokoraa wa Muhangaikaji wa Mlalahoi wa Pangupakavu wa Kabwela wa Mdanganyika Mlipakodi, ambaye siku si nyingi wapambe wako walipita kijiweni kwangu na baragumu kunitaka nikusanyike kwenye uwanja wa ‘mkung’utano’; nishuhudie jinsi mlivyokuwa mkiucheza ule mchezo wenu maarufu kwa harufu, muupendao wewe na waishiwa wenzio, mchezo wa kuchafuana. 

Ha ha ha ha ha!!! Sikuwa nimevaa rangi rangi, na sauti ya kijiweni haitoki kwa mvaa suti kwa hiyo kama hukunitambua kwa masempele yangu niliyokuwa nimejifunika ili walau msiseme natembea uchi japo kusema kweli sikuwa nimevaa, basi itakuwa shida kweli kunikumbuka, ila salaam nakusalimia, shikamoo mkulu wa kaya. 

Sitaki nikukumbushe zamani maana najua wewe waifahamu vyema historia ya kaya yetu hii na jinsi ambavyo kaka mkubwa, Mkufunzi wa Mdanganyika wa Mlipakodi alivyotuasa na kutuacha, ila miye nimekuja tu hapa mtaani kwako nikuletee  salaam za wadogo zangu wale akina Mtafutaji na Mjasiria, na hata yule aliyepewa jina la babu wa babu yake na babu mzaa baba, Mlalahoi. 

Wala sina haja ya kukumbusha jinsi Mlalahoi alivyo mtundu na hata bibi yake yaani mama yenu mkubwa Mchakarikaji anasema amechoshwa na kelele na vurugu za huyu mtoto, ila hayo unayajua.

Juzi tu wakati nafunga safari kuja mjini, mlalahoi akaniijia na majani  mabichi mkononi, unaweza kudhani nilimdharau tu kwa vile ni mtoto anacheza, lakini mimi namfahamu vyema mlalahoi, akifanya jambo ujue anataka kusema jambo. Asivyo na adabu, ati nayo akayaweka kwenye kimfuko changu cha Rambo nilimoweka pia vidaso vyangu vya kubadilisha, hapo sasa nikakasirika, nikataka kumzaba kofi, lakini kabla hata sijanyanyua mkono akanitazama na kutabasamu kitoto, kisha akasema “Kaka, hiyo dawa hiyo, uende nayo huko mjini”.

 “Dawa ya nini wewe Mlalahoi, mbona weshi vituko we mtoto?” Nikamuuliza na hata mimi sasa nilitabasamu maana kumbe ule niliowaza kuwa uchafu, ilikuwa namna yake ya kunijali nisiugue niendako.
 “Dawa ya majipu kaka, huko mjini nasikia huo ugonjwa umeenea na hata kaka yetu Muishiwa sana mkulu wa kaya, siku hizi anatumbua majipu tu...”. Nikamtazama huyu mtoto, kisha nikaanza kujihoji ameyatoa wapi mawazo hayo kichanga huyu asiyejua chochote katika dunia hii ya “si hasa” za kuchafuana hata baada ya “uchafuzi mkuu”?

Nadhani mlalahoi aliouna wasiwasi wangu, akanishika mkono na kuniashiria nikae chini, nikaketi na kumsikiza, ndipo aliponiambia nikifika mjini nikusalimu na ati nikwambie ingawa ni kweli kwamba dawa yoyote ni chungu wakati wa kunywewa kwake, na kwamba dawa ya jipu kutumbuliwa, lakini tumeagana na nyonga katika mbio hizi!?.

Ndiyo, maana huku kwetu sasa wale watoto watukutu wa mzee Mhalifu wameanza tena zile tabia mbaya za kumpiga dada “Fatuma” na ati ukiuliza unaambiwa “hali ngumu sasa tukale wapi?”, na miye swali ambalo sijalipatia jibu hadi sasa ni ikiwa ‘kumpiga fatuma’ ndiyo suluhu ya njaa yao, ila miye salaam nakusalimia.
Nasema hili ongezeko la kile ambacho sungusungu wa kijiji wanakiita “uhalifu mdogo mdogo” siyo hasa jipu, bali ni dalili za kansa inayomea na kukua upesi, na naapa mwaniapisha ikiwa hamtafuti dawa yake, tumbueni majipu lakini kansa haitumbuliwi. 

Ati! Najua wako wanaosema kwani anajua nini bananga huyu, na wako wengine watatafuta kunitumbua na miye kwa kutumia ile sindano yao ya “swahiba klaimu”, lakini miye sivunji sheria bali ni salaam tu nawasalimia. 

Ala! Kwani mmepofuka lini msione kwamba ama ongezekeo hili la ‘vibakaji’ vinavyobaka hata chakula chetu tulichokitolea jasho na damu, ni dalili ama kwamba ile bana matumizi sasa inaanza kutufikia hata sisi tuliokuwa tukipiga kelele za ufisadi bila kujua kwamba hata kuishi mjini kwa ‘misheni tauni’ ni ufisadi, ama kwamba wahalifu papa hasa wauzao sembe wameamua kuanzisha mbinu ya kuhamisha ‘atensheni’ yenu mkimbizane na ‘vijitu vidogovidogo’ ili wao wasage na kuuza sembe lao kwa amani!? Ha ha ha ha ha ha!!! Nacheka mwanichekesha miye!

Nasema ya wauza sembe msiniulize maana miye si mla nyama, mchicha na tembele ndiyo mboga yangu, lakini sembe simo hata kidogo, na hapa salaam nawasalimia, ila fumbueni macho muikate kansa hii kabla haijaenea sana na kuwazidi kimo enyi wana maana mchelea mwana kulia hulia yeye.
Ala! Kwani hamjui kwamba kuna waliokuwa wakiishi mjini kwa misimu ya sikuu za kitaifa na sasa hawana la kufanya  ili wanunue ugali kwa mama ntilie!? Ama mwajifanya mmesahau kwamba walipoamua kutoendesha magari yao kwa vile mafuta yamekuwa aghali, na vipuri vimeacha kuharibika na hivyo gereji hazina kazi!?. Nasema simo humu namo!. Mwashangaa ati inakuwaje sasa mnasikia kilio, fatuma kapigwa mtaani kwenu!? Mwashangaa nini!?

Sisemi kati msibane matumizi na wala msitumbue majibu uchungu  maana dawa ya ugonjwa tiba, lakini nauliza tu ikiwa kuna mipango mbadala ya kukabiliana na madhara yatokanayo na hatua chanya hizi ama wote tufumbe macho tusali!? 

Ni mimi ndugu yenu Chokoraa wa Muhangaikaji wa Mlalahoi wa Pangupakavu wa Kabwela wa Mdanganyika Mlipakodi, salaam nawasalimia.

Thursday, March 12, 2015

KWANI HUU SI MWAKA WENU WA UCHAFUZI!? CHAFUANENI.



Salaam nawasalimia!

Hivi! kwanini wengi wenu mmekuwa “mnanidipu” kwenye kitochi changu na ati kwavile Chokoraa nina “gando” la kugandishwa nikiwapigia mnakimbilia kuniuliza mbona siku hizi sionekani!?. Ala! Mwataka nionekane wapi!? Kwenye vilinge vyenu vya ulevi wa “si hasa” majitaka!? Nani kasema nataka kulichafua kaniki langu na majitaka yenu?. Simo naapa. 

Ha ha ha ha ha!!! Chafuaneni maana huu hasa ndiyo wakati na mwaka wenu, mwaka wa Uchafuzi.  Na miye humo nahusikaje!? Simo. 

Nasema kama walivyokwishasema wale waliokuwa kabla yenu, Nguruwe kwake sifa kugagaa matopeni na mimi nakupongezeni kwa juhudi zenu za kuchafuana, na wala siwalaumu maana huu ndiyo muhula wake, muhula wa kuchafuana, ila miye salaam nawasalimia.
Nasema kuchafuana si jambo baya kwenu hasa kwa vile hiyo ishakuwa mila na “visturi” kwenu, ila wacheni basi kutuchezea mahepe na viini macho tena mchana kweupe siye wana wa Mdanganyika Mlipakodi, maana michezo yenu hii mwailipia kwa kodi za Wadanganyika hawa na miye nauliza mwataka kutudangaya mpaka lini!?. 

Ati! Kwani si nawasikia jinsi mlivyo na juhudi katika kututaka na sisi tushiriki kuchafuana kwenye uchafuzi wa  “ ka tiba” kapya ilhali hamjafanya maandalizi tosha ya kutufikisha mahututi siye kwa tabibu!?. Ha ha ha ha ha!!! Na miye nauliza, hivi ‘ka tiba’ haka kanatibu ule ugonjwa wenu uliomuua Maadili wa Mdanganyika  ama ugonjwa unaowaua kila kuitwapo leo wana wa  Mdanganyika wa Mlipakodi!?. Naapa hiki ni kiini macho kwa wazima kupata ‘ka tiba’ ilhali wagonjwa wa umaskini na “si hasa” maji taka wakiachwa wajifie kwa kadri wawezavyo ila simo. Tena simo kabisaaa, sihusiki. 

Haya, niyawache hayo miye ya ‘ka tiba’ kalikomuua badala ya kumtibu Umoja wa Mshikamano wa Mdanyika wa Mlipakodi, japo kusema kweli nakumbuka  bado jinsi tulivyotawanyika msibani bila hata kuanua matanga ati kwa vile sungusungu wa kijiji waliamuliwa wawanyamzishe wote waliokuwa wakilia sana, na ati watakaogoma kunyamaza basi wapigwe tu maana wanapenda kulia.
Nasema huu mwaka wenu tu hata mkatae enyi wana wa Mdanganyika Mlipakodi na japo mwenye macho haambiwi tazama, lakini kutazama si kuona na miye hapa salaam nawasalimia. Ala! Kwani si wenyewe mwajionea vituko vya uchafuzi huu, wakati mnapofukuzana kwenye banda lenu ati kwa vile mmeshindwa kuelewana wenyewe kwa wenyewe, ama kwa vile bwana mdogo ameshindwa kunyamaza akasemea kwenye kashimo kwamba mfalme ana masikio kama popo!?. Ha ha ha ha ha ha!!! Ama kweli si kila ukweli ni ukweli na si kila ulijualo yakupasa kulisema maana ati ulimi uliponza kichwa.  Simo naapa. 

Nauliza ikiwa kumwendesha Farasi kwa kupeni taabu mtaiweza nyie kasi ya Nyumbu ama na nyie mwachafuana tu kwa vile huu nao ni mwaka wa uchafuzi!?. Pole sana wewe mwembamba  lakini mzito kwa uzito wa Tembo. Nasema hili si kosa lako hata kidogo bali ni kosa la Wadanganyika sisi tuliosahau katazo la kumsifia Mgema na sasa umewatukana Mamba ilhali hujavuka mto, ona sasa hasira yao inavyokuchafua. Hata hivyo si mwaka wa uchafuzi!  Chafuaneni tu ila mimi humo simo katu!. 

Nasema mnisamehe ikiwa pamoja na ukweli kwamba ninaumwa, tena hoi bin taabani, bado nachelea kuchafuana kwenye uchafuzi wenu huu wa ‘ka tiba’, japo kusema kweli najihoji, mtafanzaje bila ‘ka tiba’ ilhali mwaka huu kale ka ugonjwa kenu ka kuchafuana kamewaanza tena!?. Ha ha ha ha ha ha!!! Nicheke Chokoraa miye maana kuchafuana ni kama kifafa, mwaujua msimu wake na dalili zake lakini ati mlikuwa na mambo mengi sana mkashindwa kuuandalia ‘ka tiba’ kwa wakati na sasa mwajaribu kuutibu kwa kasi ya zimamoto. Simo naapa. 

Haya, wacha nirudi zangu jalalani nikakusanye mapande ya Boflo kwa ajiri yangu na wadogo zangu na hata Yule mama yangu kikongwe Shida wa Matatizo wa Taabu Maisha Magumu. Naomba chonde chonde, mkiisha kupata ‘ka tiba’ ka ugonjwa huu wa kuchafuana, basi chafuaneni maana nani atakukatazeni ilhali huu ndo msimu wake hasa!  Ila chonde enyi wana msije mkauchafua hata mchezo wenyewe wa kuchafuana ikiwa mtaamua kujiingiza kichwa kichwa kwenye uchafuzi wa ‘ka tiba’ ati kwa vile msimu wa ugonjwa wa uchafuzi umefika, kwani kale ka tiba kalikokutibuni miaka yote kana nini hata mwatumia nguvu ya zimamoto kuzima barafu!!!!!?. 

Wasalaamu, ni mimi ndugu yenu Chokoraa wa Muhangaikaji wa Mlalahoi wa Pangupakavu wa Kabwela wa Mdanganyika wa Mlipakodi nawasalimia, shikamooni Wadanganyika.

Wednesday, October 15, 2014

Mwaujua Ugonjwa wetu enyi wana!?



Salaam nawasalimia. Nasema tofauti ya mjinga na mwerevu ni ipi ikiwa nilijualo hulijui na ulijualo silijui na ujinga ni kutojua jambo enyi wana salaam nawasalimia. Ha ha ha ha ha ha!!! Nicheke miye! Kwani si mlikuwa mwalalama ati mwataka makubaliano mapya nyie mwaita katiba ya kugawana kaya yenu? Haya, kiko wapi sasa enyi msiojua majira na nyakati hata mwalana na kuraruana mkigombea fito ilhali mwajenga nyumba ileile?. Naapa humu simo. 

Ona huyu naye ati niwachilie mbali viapo kwa vile viapo vyazuiwa na mila za kikoloni pasina kujua kiapo ni ukomo wa uwezo wa mwanaadamu, na mimi katika kukueleweni nimefika ukomo na naapa mwaniapisha enyi wana na miye humu simo. 

Shikamooni Wana wa Haraka Tu. Ndiyo, salaam nawasalimia kwa vile haraka zenu zakuponzeni mwapotea njia mchana kweupe kwa uvivu wa kuuliza na miye humo nahusikaje!?. Simo. 

Ala! Mwadhani ati kwa vile Chokoraa miye hushinda majalalani nikichakura nipate cha kuwalisha vitegemezi vyangu wana wa mama yangu Shida wa Matatizo wa Taabu wa Maisha magumu mke wa mzee wangu Muhangaikaji wa Mlalahoi wa Pangupakavu kilembwe wa Mdanyika Mlipakodi, basi siijui tofauti ya adhuhuri na jioni!? Mwanitania enyi wana na miye humo simo. 

Nasema wachilieni mbali uzandiki wenu ashakumu si matusi ila ikiwa kwenu kuuita uovu kwa jina lake matusi, basi miye salaam nawasalimia. Ndiyo, nakumbuka sana miaka ile ya kipindi kile cha Yule kitukuu wa Nchumali Ntoto wa Chilingi mwana wa Chipuputa mlivyokuwa mkiiandama ‘siri kali’ tena kwa kuivisha koti la chama cha upinde wa zamani, na kudai ati inakataa kuanza mchakato wa katiba na hivyo kuwahujumu wanyonge. Naapa wanyonge wa kaya hii wamekosa msemaji na miye humu nitoeni. Ala! Kwani mwadhani sioni jinsi ambayo kwa Mkwere huyu kukuruhusuni mfanye huo mchakato wenu mlivyowageuza ‘wana wa kaya’ kuwa ngao katika vita yenu ya panzi!?. Nasema msinitanie enyi wana maana miye si babu japo kusema kweli kwenu nyinyi pia si mjukuu na humu pia nitoeni. 

Nauliza maana kuuliza si ujinga, kwani ‘Waishiwa’ ninyi si ‘wana wa kaya’ ati kwa vile tu mko kwenye hilo genge lenu la wahuni wajuao kuvaa mavazi na tabasamu za kikoloni? Kama na nyie ni wana kaya, inakuwaje mwagombana na kila mmoja akidai anatetea maslahi ya Wana wa Mdanganyika wa Mlipakodi? Naapa mwatufanya mazuzu enyi wana na miye humu sitaki katu kuhusika maana simo, tena simo kabisaaaaa! 

Ati! Hivi mwadhani shekeli za baba yetu Mdanganyika wa Mlipakodi mnapoziswaga kama Ng’ombe waendao machinjioni kwa kisingizio cha kutuandalia  ka tiba kaliko bora bila kuufahamu vyema ugonjwa wetu, sisi nao ni wajinga tusioifahamu janja yenu!? Wacheni dharau enyi weledi wenye kwenda mbele ilhali macho yatazama mtokako na miye humu nahusikaje!? Simo.

Haya, mwabishana na kugombana kila mara ati muwe na siri ngapi za kuzitunza pasina kujiuliza hizo mlizokuwa nazo zimevujaje hata kutufikia sisi akina Chokoraa kama mwafahamu kutunza vyema hizo ‘siri zenu kali?’. Naapa ujinga hauna tafsiri na miye humu nitoeni.
Kwani nyie si ndiyo mliokuwa vinara wa kumnukuu Yule mzee mwana wa Mzalendo na hapa namsema Mkufunzi wa Mzalendo wa Mdanganyika, ki wapi sasa kile mlichokuwa mkituaminisha sisi wadharauliwa wenu kwamba “wale” wameasi misingi iliyotiwa na Mkufunzi na “ninyi” ndiyo manabii pekee mliobaki kuirejesha kaya yetu kwenye msingi?. Ha ha ha ha ha!!! Nasema penye pongezi zitolewe na mimi nakupongezeni maana mwauweza vyema mchezo wa ‘si hasa’ isipokuwa izi za mara hii ni zile za majitaka yasiyofaa kwa kunywewa ama kilimo cha umwagiliaji kama mjitapavyo na miye humu simo. Ala! Mlipoona misingi ya huyo mkufunzi mwenyewe inakinzana na tamaa za mioyo yenu, si nilikusikieni baadhi yenu mkimtusi hadharani kama wana wasio malezi wenye kutukana wazazi? Naapa laana mmelaaniwa enyi wana na miye humo simo. 

Nani kakudanganyeni Chokoraa miye na wadogo zangu ukoo wa Mdanganyika Mlipakodi ugonjwa wetu ni idadi ya ‘siri’ zenu!? Kwanza hatutaki hata kuzijua hizo siri zenyewe, ziongezeni ukali hata tusizikaribie kama mwataka, lakini hakikisheni kaya yetu inabaki moja kama alivyoiwacha mwana wa Mzalendo na msipotenda hayo, naapa hatutaiwachia historia kuwahukumu bali tutawahukumuni sisi wenyewe na  miye humo simo tena simo kabisaaaa, ila salaam nawasalimia. 

Ni mimi Mdharauliwa wenu, Chokoraa wa Muhangaikaji wa Mlalahoi wa Pangupakavu wa Kabwela wa Mdangayika wa Mlipakodi nawasalimia. Salaam Waishiwa.  

Friday, January 3, 2014

Mgeni Njoo Mwenyeji Akome.



Salaam nawasalimia. Najua mwaka wa jana umekwenda na najua wengi wenu bado mngali kwenye zile nyumba zenu zenye baridi ya kutengeneza huku mkijituma wengine kuijenga na wengine kuivunja kaya ya wadanganyika na ati bado mwashangaa kwanini jengo halikamiliki. Mwashangaa nini?. Nasema ikiwa walio wengi mnafanya kazi ya kubomoa ilhali wachache tena wenye nguvu chache wanafanya kazi ya kujenga si ajabu itawachukua miaka dahali walau kulifikisha jengo kwenye ‘renta’ ila humo miye simo bali salaam nawasalimia. Shikamoooni Wadanganyika. 

Nisemeje!?. Mwataka nirudie kuwakumbusha madhila yaliyotukuta kwa mwaka uliopita?. Katu. Nasema siendi safari ya maili kumi elfu kinyumenyume asomaye na afahamu ila mi salaam nawasalimia. Jana imepita na kesho si yetu lakini ikitumika vyema leo walau kesho yaweza kuwa na matumaini na miye hapa nawasalimia. Kwa mwaka huu naapa sitasema matukio bali mazoea na tabia zenu maana tabia hutengeneza utamaduni wa jamii na miye nakuulizeni enyi wana  wa Mdanganyika Mlipakodi nani aliyekundanganyeni kwamba kuna kaya nyingine mtakwenda baada ya Danganyika yenu hii?. Ala! Washangaa nini?. Kwani si miye nakuoneni mnavyoishi kama watalii tu hapa kwenye kaya yetu kila mmoja akijaribu kuwa kama wale waliowatawala babu zetu bila kujua kwamba twatofautiana siyo tu ngozi bali mtizamo na miye humu nitoeni.

Ha ha ha ha ha ha!!!! Nakumbuka Mkulu wa Kaya kabla ya ule “Uchafuzi Mkuu” wa mwaka uleeeee ulitukasirisha sisi Wadanganyika hata tukapiga kura na kumpa yeye aslimia zaidi ya thamanini ya ‘kula’ zetu huku tukisahau kwamba tuna zaidi ya asilimia tisini ya familia za kulishwa na ‘kula’ hizo za bwelele, alituahidi ajiira makumi mia na sasa leo twalalama na miye nauliza twalalama nini?. 

Mwaka wa jana Chokoraa wa Muhangaikaji wa Mlalahoi wa Pangupakavu wa Kabwela wa Mdanganyika Mlipakodi nimezunguka majalala yote tangu yale ya uswahilini kwetu kunakotupwa miiba ya dagaa hadi yale ya waishiwa kunakotupwa boflo na mapande ya nyama ati kwa vile yamekaa sana kwenye jokofu yakakosa radha, naapa mwakufuru enyi wana. Kwani mabucha hamkuyaona hadi mwanunua vyakula na kisha kuvitupa kwa kujifanya uzungu usio tija!?. Simo naapa. Kwani msipotupa Chokoraa miye nitakula nini? Lakini walau jifunzeni kumheshimu Mwenyezi aliyekupeni nyie kusaza siyo kwamba mtupe jalalani bali mtupe siye tusio hata na kidogo na miye humo nahusikaje?. Simo.
Nasema katika kuzurura kwangu nimejifunza jambo moja kuu na hapa salaamu nawasalimu wale sungu sungu wa mipaka yetu na wale manyapara wenye jukumu la kusimamia vibarua vya kaya yetu, shikamooni waishiwa. Nauliza, hivi waishiwa nyie mnafahamu  uzito na upana wa majukumu yenu au kwavile kama wasemavyo  wadogo zangu wale akina Mzembe na Mzururaji kwamba kaya imeuzwa basi na nyie mmeamua kuuza na utu wetu? Naapa humu miye nisihusishwe. 

Nasema kuanzia kule kwa akina Ngosha kwenye viwanda vya samaki hadi kwa akina Nchumali kwenye Korosho wadanganyika nyie hamna chenu  ati kisa mnatekeleza sera ya ‘Ukewenzaji’ na miye nauliza mbona ‘Ukewenzaji’ huu mwabakwa nyie na sisikii hata lalamiko?. Ha ha ha ha ha ha!!!!! Ninyamaze miye maana si ajabu mkaniuliza kanituma nani wakati miye ni salaam tu nawasalimia. 

Hivi wakati mlipoamua ‘kubinua na kufisha’ viwanda vyetu vyote tulivyorithi kutoka kwa wazee wetu Waishiwa nyie mliamua kubinua na kufisha hata ajira zetu?. Ha ha ha ha ha!!! Chokoraa miye nimepita na kukutana na wageni wakikaa kwenye majumba ya viyoyozi huku wakiwa hawajui hata kuandika idadi ya mali inayoingia na kutoka viwandani zaidi ya utaalamu wa kujua kuvaa na tabasamu za kikoloni na ujasiri wa macho wa kuwatazameni usoni mnaposhikana mikono kusalimiana na miye nauliza, hivi hakuna kati ya Wadanganyika wataalamu wa kufanya kazi hizi hadi mwatuletea wataalamu “feki” wenye kujua tu tabasamu na “hendisheki” ilhali utendaji wote wafanywa na akina “sabani” asomaye na afahamu?!!! Simo humu. 

Nani hakumbuki jinsi ambavyo kwenye migodi ya dhahabu kulikuwa na wageni waliokuwa wakiitwa “sekyurite sipeshialisiti” ati kwa vile wanatokea Unepali ilhali kwao walikuwa makplo na masajenti huku makapteni na maluteni wetu wastaafu wakisota mitaani kutafuta ugali wa kulisha watoto!? Naapa historia inajurudia na miye humu simo. 

Bado kidogo. Sijamaliza, naomba kuuliza wakati “wakewenzaji” hawa wanapoleta msururu wa “wataa haramu” hawa na kuwavusha kwenye stendi za mabasi ya hewani, wanawaeleza wataalamu wetu wa uhamiaji kwamba wanakuja ‘kuisaidia’ kaya yetu kwa lipi?. Au ndiyo yale yale ya kiazi kuitwa kwa lugha ya kitaalamu “potato”?!!!!. Naapa sihusiki.  Haya, endeleeni na michezo hii ya mbuni ya kuficha vichwa mchangani ili mkirudishe kizazi chetu kwenye ukoloni kule ambako babu zetu walipigana kufa na kupona kututoa sisi halafu na nyie mtakapolala na baba zenu mkiiendea njia ya watu wote mkumbukwe kama wasaliti wa juhudi za wazee wenu na miye humo nisihusishwe maana simo tena simo kabisaaaaa, sihusiki. 

Haya, na nyie mjiitao wakulu wa kazi na ajira wa kaya yetu, mmeshindwa nini kutengeneza torati ya kulinda ajira za wadanganyika wenzenu na kuzisimamia?. Ha ha ha ha ha ha!!!! Najua, najua mwaniona mjinga kwa vile wadogo wakisimamisha pembe wakubwa wapewa bahasha na mambo yanakwisha na miye humo nahusikaje? Lakini niseme miye nisijehukumiwa na kizazi kijacho kuwa mnafiki maana najua kama mungetaka kuyatenda yawapasayo yangetendeka lakini hiyari yashinda shuruti na miye humu nahusikaje?. Simo naapa. 

Haya, leo akina "Sabani" wamebaki kufukia hivyo "vidigirii" chini ya magodoro ya bibi zao huku wakipika chai na kufagia na kisha kwenda kufanya kazi za taaluma zao ili kuwafurahisha "mabosi" wasiojua hata kusoma na kuandika lakini wenye vibali halali tena vya kufanya kazi za taaluma kwenye kaya yetu na miye humu nahusikaje maana simo. Nauliza katika kutembea kwenu kote huko mwendako mmeshindwa kujifunza kwamba kaya za wenzetu hata kabla hujaenda wanakupima hata magonjwa wajiridhishe juu ya usalama wao na watu hao?. Nani aliyekurogeni enyi wana wa kushi?. Simo naapa. 

Ni mimi ndugu yenu Chokoraa wa Muhangaikaji wa Mlalahoi wa Pangupakavu wa Kabwela wa Mdanganyika Mlipakodi nawasalimia, Shikamooni Wadanganyika Walipakodi.

Wednesday, October 9, 2013

Wana Haraka tu!!!!!!!!

Salaam nawasalimia. Karibuni kwenye kilinge cha Chokoraa enyi Wadanganyika wana wa Mlipakodi mnisikize kaka yenu Chokoraa mwana wa Muhangaikaji, maana niyaonayo miye huku majalalani yatosha kunitia fahamu na kutaka salam kuwatumieni, Salaam wadanganyika. 

Ukiamka asubuhi huku tumbo lakusumbua, usikimbilie kupiga ramli ama kufakamia kikombe cha babu bali tafakari ulichokula jana yake na hiyo ndiyo busara enyi wana, salaam ndugu yenu Chokoraa wa Muhangaikaji wa Mlalahoi wa Pangupakavu wa Kabwela wa Mdanganyika Mlipakodi nawasalimia.
Ati!. Wakataa nini? Kwamba wewe si Mdanganyika ama si mwana wa Mlipakodi!?. Ha ha ha ha ha!!! Nicheke miye kitukuu wa Kabwela maana nijuavyo Wadanganyika nyie sasa mwahoji hata asili ya mzazi wa mzee Utaifa wa Uzalendo wa Uadilifu na miye humu nahusikaje!?. Ndiyo, kwani siku hizi si Wadanganyika wote wamekuwa ‘wana haraka tu’?.  

Nani alinidanganya nikadanganyika Chokoraa miye kwamba harakaharaka haina Baraka maana siku hizi ati mwauthamini zaidi msemo ule kwamba ngojangoja yaumiza matumbo pasina kutafakari kwamba ‘haraka tu’ zenu za kula hata visivyoliwa na wazee wenu kabla yenu, ndiyo sababu ya matumbo yenu kukusoketeni na wala si subira yenye kuvuta heri iliyo chanzo cha mgogoro wa matumbo yenu!?. Naapa humu miye msinhusishe maana simo. 

Siku hizi ati kila Mdanganyika ni ‘mwana haraka tu’ na miye nauliza, hizi haraka zenu zakupelekeni wapi enyi wana mbona mwanishangaza!. Nasema mapema ili yatokeapo msijenihusisha mchakuraji miye maana miye yangu majalala huku nikichakurachakura nione ikiwa nitapata kipande cha boflo nipooze njaa ya tumbo langu. 

Ama kweli kusoma kwingi si kujua mengi bali maisha ndiyo kipimo cha akili kama walivyosema wale waliokuwa kabla yangu miye mwana wa Muhangaikaji. Najiuliza hivi mbona kila siku kwaibuka ‘wana haraka tu’ na mbona wote waibuka kunifunda kudai haki na hakuna kati yenu awekezaye muda walau kiduchu kunifunza wajibu!?. Nani alikudanganyeni kwamba haki huja bila wajibu wenyi wana mbona mwapotea njia mchana kweupe kwa uzembe wa kuuliza?. 

Haki ya mtoto, haki ya mwanamke, haki ya kichaa, haki ya mlevi, haki…. na miye nakuulizeni haki zenye kuja bila wajibu mwayajua madhala yake nyie?. Ha ha ha ha ha!!! Oneni sasa mnavyolalama kwamba ati Yule mzee wa siku nyingi wa kaya yetu almaarufu Maadili ya Mdanganyika yu taabuni kama si taabani. Mwalalama nini ikiwa mmeshindwa kujua kwamba hamuwezi kuendelea kumlisha mzee huyu sumu iliyomuua Maadili ya Wageni na mkataraji ati kwa vile huyu na yule wafanana majina tu lakini si ndugu basi sumu itageuka kuwa dawa kwenu!?.  Simo nasema. 

Nasema ijapo mtasema wajuaje weye tofauti ya uchafu na chakula bora ama dawa na sumu kali ilhali wala majalalani na kulala mitaroni lakini nasema hekima si kama pesa kwamba ukiwa nayo yakutia kiburi na dharau na maneno ya mwenye hekima ni bora ijapokuwa hekima ya maskini haithaminiwi na hata maneno yake hayasikizwi na ndiposa nawasalimu, shikamooni Wadanganyika. 

Haya, nakumbuka wakati wa kukua kwa wadogo zangu wale akina Mzembe na Mzururaji na hata mimi kaka yao Chokoraa wa Muhangaikaji, fimbo ilikuwa ufunguo uliiondoa ujinga kichwani mwa mtoto lakini sasa mwasema ni haki ya mtoto kutopigwa bali ipigwe ngoma na miye nakuungeni mikono na miguu yote, lakini wacheni kulalama basi ikiwa heshima ya juzi na jana zina tofauti maana hiyo ni haki ya mwendawazimu peke yake. Ala! Kwani si haki ilipaswa kuja na wajibu!?. Nasema ikiwa mwanifunda tu juu ya haki yangu na kudhani wajibu wangu nitaufahamu ikiwa tu nitapewa haki yangu, jiandaeni basi kwa madhila ya kizazi cha nipe nipe maana ndivyo mtakavyo na miye humu nahusikaje!?.  
Ati! Wengine mnalalama ni kwanini kila mkirejea majumbani mwenu mwakuta ‘ndoo’ zimevunjika na sasa vijana hamzitaki hata ‘ndoo’ zenyewe badala yake mwanunua mabeseni ya karatasi ambayo mkiishaogea mwayatupa huko huko maliwatoni!?. Mwalalama nini!?. Kwani mlipoamua kutangaza haki na usawa kati ya jinsi zenu bila hata kufafanua yale yapasayo kuwa sawa na yale yasiyopasa na badala yake mmeifanya jamii yote kuwa na watu wenye maumbile ya Adamu na Hawa lakini wenye kufikiri kama Adamu tu mlidhani madhara yake nini!?. Nasema chakula cha fahamu ni maneno na mifano na kile wanachokisikia wanenu na kukuoneni nyie mkitenda ndicho watakachotenda na wao kwa juhudi kubwa kuliko watangulizi wao na miye humu mnitoe maana simo. 

Wacha nikomee hapa hadi tutakapokutana juma lijalo kwenye kijiwe hiki, wacha nijaribu kumeza vipande vya boflo hivi na maji ya chumvi ila salaam zangu zikufikieni enyi Wadanganyika.
Wasalaam, ni mimi ndugu yenu Chokoraa wa Muhangaikaji wa Mlalahoi wa Pangupakavu wa Kabwela wa Mdanganyika, nawasalimia. Shikamooni Wadanganyika.