Ati mwashangaa!! Ndiyo, wakati mwaka 2011 unapofikia mwishoni, Chokoraa wa Muhangaikaji wa Pangu pakavu, wa Mlalahoi, wa Kabwela, wa Mdangayika nimepata faida moja kubwa na mwaka huu na hiyo ni kutambua haki yangu ya kupewa taito.
Nasema wewe unayenuna na kukasirika ni kwa sababu hupendi tu nikwambie ukweli kwamba ikiwa unatafuta kufanya tathmini ya mwaka kwa kutumia kigezo cha shekeli ulizonazo kwenye ‘kilindo’ , basi umepotea njia. Ndiyo. Pamoja na kwamba pesa sabuni ya roho na penye udhia penyeza rupia, lakini kwenye hii dunia gunia yetu ya sasa, unahitaji pia kuwa kwenye ‘lokeisheni’ sahihi ili kuliona tundu la wewe kupenyeza lupia hapo penye udhia ili upate matokeo na kwa kuigundua siri hii nadai kutunukiwa heshima ya uprofesa wa kitaa. Ngoja kwanza! Bado nakamilisha ‘risachi’ kabla sijaanza kuitumia mbinu hii kwa ajiri ya kujiletea maendeleo, ila nimeamua nikumegee walau kidogo ili usisumbuke kujiuliza ni kwanini waishiwa kila mara wanaonekana kupanda juu ilhali wadharauliwa tukibaki chini siku zote, humu namo simo.
Ikiwa utaamua kubishana na Profesa (mtarajiwa) Chokoraa kwenye hili nasema simo. Ebu tazama pembeni yako uone. Wangapi umekua nao, umeishi nao na hata kufanya nao kazi na unao uhakika wa ‘asili elfu’ miamoja kwamba ‘kredenshozi’ zao na hata utendaji wao hauna hadhi wala sababu ya ‘kutunukiwa’ shahada ya udaktari ati wa falsafa wa heshima na kutengeneza kundi la mbumbumbu wenye majina yanayoanza na ‘Dk’ utadhani kuitwa ‘Dk’ kunabadili DNA na kumfanya mtu kuwa “royo klasi” kwa usiku mmoja tu, humu namo simo.
Huwezi kuamini kiasi na umbali wanaokwenda hawa jamaa kupata walau hiyo ‘taito’ ya utabibu, naapa utakasirika nikikueleza na ndiyo maana nashona domo langu nisibwabwaje kwa hasara ya kichwa changu na vitegemezi vyangu na hata yule kikongwe mke wa marehemu Muhangikaji, mkamwanae Mlalahoi, mama yangu Shida wa Matatizo.
Ngoja kwanza niendelee kukupa walau topic moja zaidi kwenye hili somo langu la “Kitaaolojia” ili nikiondoka darasani usibaki na maswali ni kwanini nataka ‘taito’ ya Prof. Chokoraa wa Muhangaikaji wa Kabwela wa Mlalahoi. Ala! Ati washangaa mimi kuitwa Profesa! Washangaa nini ebu nikuulize kama alivyouliza papaa mawani mwaka ule iliponyesha mvua nyingi na watu wakalima na kuvuna sana upande mmoja lakini kwa ubovu wa miundo mbinu na migomo ya yule nyoka wenu wa chuma, wakati upande mwingine misosi ikiozea kwenye maghala, upande wa pili wanadamu wakidodoka kwa kutokwa uhai kisa njaa na bado ati mwatunukiana shahada za udaktari wa falsafa, naapa simo.
Ala! Kwani nani hajui kwamba wako baadhi yenu mliolazimika ‘kupolitiki’ ili kupata nafasi za kutunukiwa hizo tunu zilizotengwa kwa ajiri ya wana wa adamu waliojaariwa kuvumilia shida za shule na kukabiliana na magumu ya watu wao hata kupata hadhi ya kutunukiwa shahada zenye shada la maua kwa utumishi uliotukuka!!? Naapa simo humu.
Tena nasema mnitoe miye Chokoraa wa Muhangaikaji wa Mlalahoi wa Pangu pakavu wa Kabwela wa Mdanyanyika. Nani kasema nataka kuhusika kwenye hili! Sasa hivi kila mmoja anataka kuitwa tabibu yaani “dokta’ hata kama anajua nafsini na moyoni kwamba hadi na heshima ya dokta ni mzigo wa mwiba ambao kuubeba kwake kutamuumiza lakini yu tayari kufa kikoloni na tai shingoni, nitoeni humu enyi wana.
Nasema, hizi ‘taito’ siku hizi zimegeuka kuwa ‘frontia’ ya mapambano kwenu wana za gunia hili bovu la dunia na athari zake zimekuja hadi huku kwenu wadanganyika na mimi simo. Kwani si mwanzo mlianza na “Uheshimiwa”!? Kila mmoja kwa juhudi na mbinu alizozijua yeye alipambana kwa kadri awezavyo ili kuwa muheshimiwa na mara mlipofika hapo mkagundua kwamba kumbe hata hapa hakuna jipya hasa kama mafanikio ya nje hayalingani na mafanikio ya ndani na hivyo “yu goti beta” mkaamua kutafuta kiwango kingine cha heshima mradi tu niwaheshimu mimi Mdangayika nisiwaze hata siku moja kuwa kama ninyi na ninaamini wala hamna mpango wa kurudi kujiita tena ndugu maana mnafahamu kwamba mimi na ninyi si ndugu tena, humu namo simo.
Sasa mmeamua kuwa matabibu. Ha ha ha ha ha Nicheke ninenepe Chokoraa miye. Ati, kila mmoja wenu sasa akiishafika tu kwenye kiwango cha heshima kwenye jamii anadai utabibu wa falsafa!!.
Mwanikera enyi wana wacha niseme ukweli wa moyo ikiwa baada ya hapa sitasema tena walau mjue kwamba Mdanyika miye nakereka na huu upuuzi wenu. Ona hata wale waliopaswa kuchunga kondoo wa Mungu nao wamekuwa walevi. Ndiyo, wamekuwa walevi tena wa ulevi mbaya wa kinywaji kiitwacho uheshimiwa ambacho kikiisha kukuzoea huacha kukulevya na ndipo mnapotaka sasa mpate nyongeza ya ‘alikohili’ ya ‘Udakitari wa Falsafa” nasema simo.
Kichefuchefu chanipata miye kila nisomapo majina yenu kwenye vyombo vya habari kila mara mkijitahidi kujiita madaktari ilihali nawajua wengi wenu nyie elimu zenu za ngumbalu na hata hayo mliyofanikisha si ninyi bali Mungu na ninayo hakika hakuwatuma muanze ‘kupolitiki’ ili kupata shahada za udaktari wa heshima, si hayo mgewaachia wana wa si hasa!!? Nasema humu simo.
Utakuta mmeandikwa kwa herufi kubwa na wino uliokoza ‘Reverendi, Dokta Chokoraa wa Muhangaikaji” hivi huu ureverendi tu hauwatoshi mpaka na udaktari naapa ikiwa itakuja “taito alikoho” nyingine mtakuwa wa kwanza kukimbilia.
Kwani kuchunga kondoo si ilipaswa kuwa kazi ya wito ambayo wale waliotangulia kabla yenu waliikata hadi Mungu (kwa vile yeye hashindwi na jambo) alipowalazimisha kufanya atakavyo yeye? Mbona nyie mwakimbilia kujipa majina makubwa hata kama mwajua mioyoni kwamba hamyastahili? Nasema kwenye hili hata kama mtasema nawakosea adabu, Chokoraa simo.
Mmezidiwa hata na ‘Mzanaki’ ambaye pamoja na kwamba alikuwa mmoja wa wadanganyika wa kwanza kabisa kupata shahada ya uzamivu na hata hiyo ya udakitari bado kwa unyenyekevu aliendelea kutaka aitwe “Mwalimu” hadi mwisho wa uhai wake, ati ninyi mliopaswa kuwa mabingwa wa unyenyekevu mnalilia majina ya utabibu. Nakataa kuhusishwa humu.
Nimechoka kusema, naamini wanafunzi mmesikia na kuelewa na kama kuna maswali basi tukutane kwenye kipindi kijacho kwenye somo letu hili la “Kitaaolojia” na Profesa wenu Chokoraa wa Muhangaikaji, wa Mlalahoi, wa Pangu pakavu, wa Kabwela, wa Mdanganyika.
Simo humu.