Najua! Naam, bado nakumbuka ahadi niliyokuahidi kwamba nitakueleza zaidi kuhusu yule jamaa maarufu wa harufu hapa mjini kwa jina la Maisha Magumu, lakini ngoja kwanza nimalizie kila kisa cha Chokoraa wa Muhaingaikaji wa Mlalaohi wa Pangupakavu wa Kabwela wa Mdanganyika kufikishwa kwenye kituo kikuu cha walinzi wa ‘muishi miwa’ saaaaana Dola.
Bila shaka unakumbuka nilipokomea kwenye kukuhadithia tukio zima na jinsi ambavyo nilitandikwa kibuti cha mgongo na kuishia kunyamaza kimya ili kuokoa uhai wangu, lakini nakuapia ndugu yangu bado nigali na hasira kwa kitendo kile japo kadhia nzima imepita sasa. Aala! Yaani kufikishwa tu kituoni tena si mahala pa usalama bali kashfa matusi na vipigo? Naapa humu miye simo. Ati kila anayefikishwa kwenye “sentro” basi ni mhalifu hata kama hajaonana na pilato na hawa walinzi wanaanza kumpa majina kwa kadri watakavyo mara wakuite Mhalifu wa Mkosaji, mara wakuite Kibaka wa Mwizi, mara Jambazi wa Sugu na mengine mengi, naapa kwenye yote hayo hakuna hata jina langu.
Nilitamani nikuite ndugu yangu Udadisi ili uwaambie hawa jamaa kwamba mimi naitwa Chokoraa wa Mdanganyika lakini nikahofia kukuingiza na wewe kwenye msambwe na kadhia ya kupachikwa majina ya ajabu ajabu huku ukitandikwa kwa kadri watakavyo wanaotaka katika kutaka kwao na humu simo.
Basi ndugu yangu, baada ya kuulizwa maswali kadha wa kadha ya kuudhi nikasukumizwa ‘lokapu’ bila hata kujua kosa langu na kama nilivyokuahadithia hapo awali, nikaamua kukaa kimya kwa vile nilijua tu kwamba kesho yake wababe hawa wangenipeleka tu kwa pilato na huko ningesema bila hofu wala mashaka kwa sababu huko hawaruhusiwi kunifanyia ubabe wao huu.
Yaliyonikuta humo ndani hata sitaku kukuhadithia ndugu yangu Udadizi na nakuonya kwa sababu ya jina lako usije ukajaribu kuingia huko kwa ajiri ya kujua kunani maana naapa hakufai. Kesho ilifika hata hivyo, asubuhi na mapema nikaamshwa na kukabidhia tena “kobazi” zangu niziitazo viatu na sehemu ya vikaratasi vyangu vilivyokuwa mfukoni na ambavyo nilinyang’anywa wakati nikitiwa ‘lokapu’, noti yangu ya shekeli kadha wa kadhaa iliyokuwa mpya niliikuta imebadilishwa na moja iliyokuwa chakavu karibu na kuchanika, lakini walau kuzeeka kwa noti hakuondoa thamani ya fedha humu namo simo, nikaitia mfukoni na kupakiwa kwenye gari na watu wengine niliowakuta ‘lokapu’ jana yake.
Kilichonishangaza hadi nakaribia kuanguka na kuzimia si kufika kwa pilato na kugundua jinsi ambavyo wababe hawa wa muishi miwa sana Dola walivyogeuka kuwa wapole na waungwana ghafla, hapana, hilo nililitaraji lakini nilishangazwa na mashtaka niliyosomewa mbele ya Pilato wa Mwamuzi.
Nakwambia ilikuwa kama mchezo wa kuigiza, mshitaki akajipanga vizuri na kurekebisha ‘ulimi wa mbwa’ shingoni mwake na kisha akajikohoza kidogo kuweka sauti sawa, kisha kwa sauti yenye mikwaruzo kidogo, na nadhani mikwaruzo hii ni kwa sababu ya kunywa sana mvinyo ila humo namo simo, akasema;
“Chokoraa wa Mdanganyika, unashitakiwa mbele ya ‘kilinge’ hiki cha ‘muheshimiwa’ Pilato kwa kosa la Uzembe na Uzururaji, kwamba siku ya juzi mnamo saa tatu na dakika kidogo za usiku ulikutwa ukitenda kosa la Uzembe na Uzururaji kwenye mitaa ya kaya yetu hii kinyume na kifungu cha sheria…..” sikupata hata nafasi ya kumsikiliza hili amalize nikaamua kumkatisha’
“...Kwanza mimi Jina langu halisi ni Profesa Chokoraa wa Muhangaikaji wa Mlalahoi wa Pangupakavu wa Kabwela wa Mdanganyika, halafu umenishitaki kwenye ‘kilinge’ hiki kwa makosa ya wadogo zangu wawili yaani Kulwa na Doto maana wamezaliwa mapacha kwa mama yetu Shida wa Matatizo na ndiye aliyemwita Kulwa Uzembe na Doto akamwita Uzururaji, na hivyo nafikiri ama ukawatafute waje wajibu makosa yao ama unipe mimi muda nitawaleta hata nyumbani kwako ukitaka”.
Nakwambia “kilinge” chote kilikaa kimya kwa muda maana nilizungumza kwa jazba na kujihamini sana. Aala! Yaani kwanza ati nashitakiwa kwa makosa ya watu wengine! Huu sasa si uonevu? Yaani Uzembe na Uzururaji wafanye makosa halafu nishitakiwe mimi Chokoraa kwa lipi hasa!? Halafu hayo makosa yenyewe waliyoyafanya mimi hata siyafahamu, nitajibuje sasa kuhusu makosa yao ambayo hata sikuwapo wakati wakiyatenda kama kweli waliyatenda na siyafahamu? Naapa huu sasa ni uonevu.
Namshukuru mwenyezi kwamba Pilato naye ni mtoto wa Muungwana na bila shaka unakumbuka jinsi yule mzee naye alivyowalea watoto wake na kuwafunza kuwa na huruma na kutenda haki, baada ya kusikiliza maneno yoote ya mlalamikaji, akalifutilia mbali shitaka lenyewe kwa vile ati aliliona halina msingi. Mimi nasema halikuwa hata na ngazi, madiirisha, milango wala paa.
Basi bwana, nikaondoka mahakamani na kujaribu kupita dukani mgahawani ili walau nijipatie chochote kitu kwa ajiri ya kula maana njaa ilikuwa ikiniuma, lakini kutahamaki hata ile noti yangu mbovumbovu ilishakwapuliwa haikuwamo mfukoni. Nikaona sina jinsi, nikaamua kujikongoja kidogo kidogo hadi kwa yule rafiki yake na marehemu baba yetu mzee Mkulima ili walau nipate embe nitulize njaa wakati nikiangalia uelekeo na ndipo nikapitia posta na kukuta barua yako.
Bila shaka sasa umefahamu chanzo cha ugomvi kati yangu na wadogo zangu hawa wawili Uzembe na Uzururaji. Nitakapokuandikia tena nitakueleza ni kwa nini nimekasirikia zaidi Uzembe uliko uzururaji ile kwa sasa nahitaji kwenda hospitali kumtazama mtoto wa Uzembe yule mdogo aitwaye Ulalamishi maana nasikia ni mgonjwa, damu nzito kuliko maji nakwambia.
Ati! Hujui kama Uzembe ana mtoto? Kweli wewe sasa unazeeka vibaya rafiki yangu. Haya nitakuhadithia yahusuyo huyo mtoto kwenye waraka wangu utakaofuata ila kwa sasa nikusalimie tu.
Wasalaamu, nduguyo Chokoraa wa Muhangaikaji wa Mlalahoi wa Pangupakavu wa Kabwela wa Mdanganyika, nakusalimia.
Wednesday, June 27, 2012
Saturday, June 9, 2012
Rafiki yangu kipenzi Udadisi Chautundu
Nimepata barua yako rafiki yangu kipenzi tuliyekua pamoja na kucheza pamoja “kidaso” yaani naona hata aibu kukuita rafiki maana wewe ni ndugu yangu. Umenilaumu kweli kwenye barua yako kwamba ndugu yako nimekusahau na hata jina lako huna hakika kama ningali nikilikumbuka, lakini nakuhakikishia hata ningeamshwa usingizini ghafla na kutakiwa nimtaje rafiki yangu wa karibu, ningekutaja wewe kwanza kaka yangu Udadisi Chautundu. Hata hivyo ni siku nyingi kweli tangu tulipoonana na nimegundua baada ya kusoma barua yako, kwamba kuna mambo mengi uliyoyasahau kuhusu mimi na kuna mengi pia yametokea ambayo hujayajua na inawezekana kama ungekuja mjini kunitafuta basi bila shaka ungenikosa.
Nakupongeza hata hivyo ulivyoamua kubaki kijijini. Ndiyo, nakupongeza kwa sababu huku mjini kuna watu wana roho mbaya sana kiasi ningekuwa sina tetesi kuhusu wazazi wao, basi nisingesita kukwambia hawa si binadamu na hawakuzaliwa lakini kwa bahati kuna tetesi nyingi kuhusu wazazi wao. Kuna huyu Maisha Magumu. Huyu jamaa unapoingia tu mjini ndiye wa kwanza unayekutana naye na nakwambia huyu jamaa ni maarufu humu mjini kuliko hata ‘mkulu wa kaya’ yetu na kila siku umaarufu wake unaongezeka.
Ha ha ha ha!! Unaona sasa, umeanza kumfananisha huyu jamaa na yule mzee pale kijijini ambaye wewe rafikiri yangu Udadisi ulinifanya kila siku nifikirie maana ya jina lake bila majibu mpaka nilipokuja huku mjini. Si yule mzee alikuwa na koti lefu jeusi na kofia ambayo japo hatukujua aliifua saa ngapi lakini haikuwa ikionekana chafu kila alipoivaa!! Usijifanye umemsahau bwana, mzee Malingumu wa Maliyatabu.
Huyu maisha magumu wala hana uhusiano na hao wawili. Yeye huyu hajulikani vizuri hasa nasaba yake maana wako wanaosema anatoka kwenye ukoo wa yule mzee mwenye kitambi mheshimiwa Kiongozi Mrafi na eti ni mtoto wa mke mkubwa wa huyu mzee Bi Rushwa wa Mlungula.
Wangine wanasema hapana, Mheshimiwa Kiongozi Mrafi anasaidia tu kumlea huyu mtoto kwa sababu wakati anamuoa mke wake Bi Rishwa wa Mlungula, Bi Rushwa alikuja na huyu mtoto kutoka kwenye ndoa yake ya kwanza kwa yule mzee kiburi sana hapa mjini Bw. Ubadhirifu wa Maliyauma. Vyovyote iwavyo, huyu jamaa amejifunza vyema kwa mama yake maana tabia zake mnh! Nitakueleza siku nyingine, leo nataka tu kujibu barua yako.
Kwanza nikuhakikishie kwamba sijakusahau ndugu yangu na unapoona sikuandikii hata barua, ni kwa sababu ndugu yako siku hizi naishi kwenye kitongoji kimoja hapa mjini ambacho ni maarufu kwa kuwa na shughuli nyingi wenyewe wanaita “bize”. Basi mwenzako nashinda bize tangu asubihi hadi jioni na kila uzingizi ukinizidia ‘naangusha gari’ hapo hapo ninapokuwa na nikaimka naendeleza libeneke. Lakini pia yule mdogo wangu Uzembe naye anachangia hii hali ya mimi kutokukuandikia barua, lakini usijari kwa sababu sasa hivi mimi na uzembe tuna ugomvi tena mkubwa, basi nadhani kwa muda mrefu kidogo ataniacha peke yangu na hivyo nitapata nafasi ya kukuandikia kila mara.
Unashangaa tuna ugmvo gani!!? Si ndo hayo sasa ninayokwambia ndugu yangu kwamba siku hizi kuna mambo mengi yamenitokea na wewe huyajui!! Hata! Wala sikulaumu. Najua unanipenda sana na ungependa kujua kila kinachonipata swahiba wako Chokoraa wa Muhangaikaji, lakini mara nyingine huwa nalazimika kukuficha mengine maana najua yatakuumiza hasa kwa vile wewe ulivyo Mdadisi kama jina lako, najua utaumia sana moyo ndiyo maana huwa mengine namezea.
Haya basi, kwa vile umelazimisha, wacha nikwambia tuna ugomvi gani na Uzembe halafu hayo mengine nitakuandikia waraka ujao. Ilikuwa usiku kamaa saa tatu na nusu hivi na tulikuwa watatu tunatokea kwenye soko la “bize” kurejea ‘gheto’ kwa ajiri ya kupumzisha mbavu zetu. Basi bwana, mara ghafla tukakutana na watumishi wa ‘siri kali’ wenye jukumu la kulinda amani. Mimi soga zilikuwa zimenikolea mwenyewe hata sikuwaona hadi walipokuwa wameshatufikia karibu, kutahamaki, Uzembe na Uzururaji wakatimua mbio na kuniwacha peke yangu. Kwanza sikufahamu kwa nini walikimbia, lakini kama unijuavyo ndugu yako Chokoraa huwa sina hofu na walinzi wa mheshimiwa Dola.
Nikasimama kwa ujasiri kabisa tena kwa kujiamini si ninajua sina matatizo mimi na mwenyekiti wetu Mheshimiwa Dola! Wapi!! Nakwambia yaani hawa walinzi hata kabla hatujasilimiana nikasikia mmoja ambaye nadhani alikuwa kubwa wao akisema kwa sauti ya ukali na ya kushutumu “Hivi hili si ndiyo linaitwa Chokoraa litoto na yule mzee marehemu Mhangaikaji?”. Akajibiwa “Ndiyo” hata sikujua ni nani aliyejibu maana tayari alishaanza kunitandika makofi huku akinipa amri mfululizo “kaa chini kachini…mikono juu.. una nini mfukoni we Chokoraaa?... huna majani mfukoni kweli wewe….?”.
Sikujua hata nijibu swali lipi kwanza na sikujua hata kosa langu, mara nikawasikia wakizungumza maneno fulani kwenye vilongalonga vyao na lugha yenyewe hata sikuifahamu ila nahisi kitakuwa ni kigagagigikoko maana sikuambulia hata sentensi moja, mara gari hilo likaja limejisheheneza walinzi wengine na hata mmoja wao akiwa amebeba ‘manati ya ndhungu’. Niliogopa nilipoiona hiyo manati wewe!!! Asikudanganye mtu ndugu yangu, manati ya ndhungu inatisha ikiwa kwenye mikono ya watu wenye hasira kama hawa walinzi wa dola. Basi bwana, nikapakiwa kwenye gari tena kwa kusukumizwa kama mzigo hadi kwenye kituo kikuu cha hawa walinzi, hapa napo nikapokelewa na maneno kadhaa ya kejeli “Mmelitoa wapi hili Chokoraa!!?” mmoja wao akauliza huku akinikwida na kunizungusha nyuma ya meza kuuubwa ajabu! Mwingine akadakia, “kwani ni Chokoraa au Jambazi kabisa hili?”.
Ala! Sasa hasira zangu zikanipanda na povu likaanza kunitoka mdomoni. Yaani wananifananisha na yule adui yangu mkubwa ambaye ndiye aliyemuua baba yangu marehemu Muhangaikaji? Nimekuwa nikimtafuta huyu jamaa na hata walinzi wa Dola waliniahidi kwamba wangemtia mbaroni sasa ni mwaka sijui wa ngapi hajapatikana na nasikia anaishi mjini humu humu tena rafiki zake wengine wanajulikana na ati ndiyo sababu ameshindikana kukamatika, leo hawa wananifananisha naye! Haiwezekani.
Nikafumbua kinywa hivyo hivyo na mapovu mdomoni. “Mimi siyo jambazi, mimi ni Chokoraa wa Muhangaikaji. Hata mimi namtafuta huyu Jambazi kwa sababu alimuua baba yangu miaka kadhaa iliyopita…” hata sikumaliza, sori ya kiatu ikatua mgongoni na kunituliza chini, nikaona ili kuokoa uhai wangu bora nikae kimya hadi nitakapofika kuonana na liwali kesho maana hawa jamaa hata hawatakki kunisikiliza. Itaendelea
Tuesday, May 1, 2012
Ama kweli hamna adabu enyi wana.
Najua! Najua umekuwa muda sasa tangu nimepitia kijiweni hapa
walau kukusalimia na si kwamba nilikusahau, ila nilikuwa kwenye ule mchezo wa
sasa ambao kila mtu ni lazima acheze tangu mdogo hata mkubwa, maskini ama
tajiri, msomi kama wewe ama mbumbumbu kama Chokoraa, nao ni mchezo wa kuwa “bize’.
Naapa simo. Si kwamba simo kwenye mchezo wenyewe, isipokuwa kwa vile wako ambao
wako ‘bize’ kila siku na wapata chochote kitu ilhali wengine wako ‘bize’
waambulia umaarufu wa harufu, humu namo simo.
Ha ha ha ha ha ha!! Nicheke miye Chokoraa wa Muhangaikaji wa
Mlalahoi wa Pangu pakavu wa Kabwela wa Mdanganyika si kana kwamba nina furaha,
lakini nani kasema hii “gunia” yetu ni kama ile ya babu yangu Pangu pakavu
ambapo walioweza kupata habari, wachilia mbali walioweza kutoa habari walikuwa
wachache sana na wenye daraja fulani katika jamii!!? Washangaa nini! Nakumbuka
miaka hiyo kulikuwa na vyombo vichache sana vya habari na vyote vilikuwa kwenye
‘siri kali’ vikitumiwa tu na ‘watwawala’ kuwapelekea amri ‘watwaliwa’ na hata
sheria ikaweka kwamba ili iwe sheria ni lazima kwanza itangazwe kwenye gazeti
la ‘siri kali’. Ha ha ha ha ha ha!!! Leo watu wasema na sisi kupitia ‘ubunifu
wa Buibui’ na mwana wa Muhangaikaji nasikika kupitia kamchezo hako ka mdudu Buibui
na bado wataka ati nisicheke! Simo humu.
Haya, wacha basi nikupe pole kwa msiba maana siku hizi kwa
ajiri ya wadanganyika woote kuhama mitaani na vijijini kwao wakishinda “bize”
na kurudi jioni ama usiku mwingi, basi utamaduni wetu umebadilika na hata
misiba haihudhuriwi kama ilivyokuwa zama na ndiyo maana hata Chokoraa sikuwa
nimepata nafasi ya kukupa pole ya misiba. He! Ona huyu ati hajui kwamba kwenye ‘inji’
hii tumepata misiba mikubwa kadhaa na ya kitaifa kwa sababu ati naye alikuwa ‘bize’
kiasi cha kushindwa kusoma ‘udaku’ na kutazama kasanduku ka picha ama
kusikiliza ile radio ya mwenyekigoda wa kijiji chao, hata alipoingia kwenye
makaazi ya Buibui yaani ‘mtandaoni’ hakupata nafasi ya kusoma ‘niuzi’ zaidi ya
kupata ‘esi emu esi’ kadhaa kwa BBM na kuishia kulala ili adamke mapema na
kukimbilia ‘bize’, naapa utamaduni wa binadamu unafirisika kila kukicha na humu
simo.
Nasema mnitoe kwenye huu mufirisi wa ustaarabu wenu enyi
wadanganyika maana mtu asite utamaduni ni mfungwa wa kifungo cha nyumbani walau
hivyo ndivyo nijuavyo Chokoraa wa Muhangaikaji wa Mlalahoi na kwa hili naapa
tutashindana sana lakini simo. Hivi si ulikuwa utamaduni wenu enyi wadanganyika
wa kuheshimu watangulizi wenu iwe ni wazazi nyumbani ama viongozi kwenye hizo ‘siri’
zenu ‘kali ‘ na hata mlikuwa na ‘proto kali’ ya kutokunywa kahawa kama
mwenyekigoda hajafika? Nasema huo unaoonekana kama upuuzi kwenu ninyi masharo
wa sasa ndiyo ulikuwa misingi ya uzalendo wa watu wa inji hii na hata kujitolea kufa kwa ajiri ya ‘udanganyika’
wao kwa sababu walau walijua ‘legasi’ yao ingebaki. Sasa naapa kila mmoja
anataka kuwa “msanii” na nimtumie pole ‘mzee wa ukweli usio wazi’ kwa juhudi
zake za kutaka ati kuifanya ‘danganyika’ yake isiitwe tena ‘bongo’ kwa vile ati
‘usanii’ ulizidi. Nani anataka kuwa ‘hiro ov ze nesheni’ (naonyesha msisitizo)
kwa kutumikia inji hii ilhali anaweza kuacha ‘ligasi’ kwa watoto wake kwa kuwa
muuza sura luningani nasema mnitoe. Ati wakulu wote wa kaya wakajikusanya na kujirundika
kwenye msiba wa ‘msanii’ na kuishushia heshima ya ‘kiifitaki’ misiba ya mashujaa
wa inji hii hadi wale walioliongoza ‘geshi la waheshiwa tangu zamani’ naapa
humu simo. Nasema kwa hili Chokoraa nitasema na kurudia kwamba adabu si
shikamoo na uungwana ni vitendo, kizazi hiki kimekosa adabu kwa watangulizi
wake na namuomba jalali awajaalie mzeeke ili muone jinsi inavyoumiza kwa kizazi
kinachofuata baada yenu ‘kuikanya legasi’ yenu chini ya nyao za miguu, siyo
nawalaani nawaombea maisha mema na ya neema ila kwenye hili la dharau mimi
simo, tena simo kabisaaa.
Nasema kama mgekubali kuwa wanafunzi mgejifunza maana
waalimu wako wengi waliotenda vyema kabla yenu ili muone na kujifunza kwao
lakini nani kasema adabu inauzwa ama hukwanguliwa kama vocha!? Naapa simo. Ala!
Kwani wakati ‘mzee wa kuruhusu’ alipoamua ‘kushtuka’ (naogopa kusema kizanaki
msijesema natumia vibaya lugha ya taifa) na kujiweka pembeni ‘kuepusha
msongamano’ ilimnyima nini kuwa ‘mkulu wa kaya’ wakati ulipowadia!? Au ni kwa
sababu ninyi sasa mmeendela sana na mnaamini “riziki kama ipo ichukue kama
haipo ilazimishe” na hivyo mwaona kung’atuka ni aibu?.
Labda ni kweli kwamba hamna heshima kwa ‘wazee’ wenu tena
enyi wana wa danganyika maana nani hakusikia wakati mlipowatazama usoni wazee
wenu na kuwahoji sababu ya wao kutotumia hayo mawazo mazuri wanayokupeni
kipindi cha ‘wakati wao’ mkisahau kwamba wakati ukuta?. Naapa mna zaidi ya
kiburi enyi wana. Nasema kama ilivyokwisha kusemwa kwamba sokoni hupatikana
vyote yaani chakula na uchafu na cha pili si aghali kupatikana kwake japo
matumizi yake ni adimu na ninyi mmejifunza kwa watangulizi wenu lakini kama
waenda sokoni mmechukua uchafu mkaacha chakula ashakumu si matusi, humu simo.
Ala! Kwani si mmeamua kwa makusudi kujifunza kwa wale waliojitokeza hadharani
mbele ya visanduku vyetu vya picha, tena tunavyoviwasha kwa umeme tunaoulipia
sisi wakitwambia wala si kutuomba kwamba tugeuke mbuzi na ng’ombe tule nyasi
lakini wao wanunue “mwewe” kwa ajiri ya ‘mkulu wa kaya?”. Nasema mmejifunza kwa
hao na mmefaulu na humu mimi nakataa kuhusika, simo tena simo kabisa.
Ni hivi juzi tu, mlikulana na kuparurana makucha huko kwenye
jumba la maamuzi na kutaka hata kuvuana nguo na wala hii si mara ya kwanza ama
ya pili walau kwa siku za karibuni, lakini tofauti na mwanzo wakati watu
walipojipachika majina kama “Bangusiro’ na mengineyo, ninyi mmekataa kuwa ‘mbuzi
wa sadaka’ na badala yake mmekuwa ‘ngangari’ kwenye kuendeleza ‘yale yote
ambayo kwa moyo na nia thabiti mmekuwa mkiitendea inji hii’ na kwa hili
nakupongezeni ila mi mnitoe maana simo. Naam, mioyo na nia zenu ni thabiti katika
kutenda lakini mnatenda kama waenda sokoni maana pana faida gani kuendelea
kuonyesha njia mbele ya mtu ambaye hayuko tayari kukufuata? Naapa nilidanganyika. Ndiyo, ni uzembe wangu
kwamba nilidanganywa nikadanganyika kwamba kiongozi wa domo daraja la kwanza
ama domo class A huzingatia misingi ya ‘domo class A’ yaani utawala wa watu
kupitia watu kwa ajiri ya watu, kumbe sivyo na humu simo tena simo kabisa.
Nakataa kuwamo kwa sababu kama watu (kupitia mawakala wao) wamekataa kwamba
fulani na fulani hatutaki muendelee kutangulia huko mbele, si adabu basi kwamba
mjitenge na kuwaacha watu wachague watu wengine wa kuongoza njia ya watu kwa
ajiri ya watu ama ninyi mnayo tafsiri nyingine ya ‘domo krasi ei’?
Sitaki kuongea sana wacha haya machache yatoshe kwa leo na
niwape pole wadanganyika walipa kodi kwa misiba mikubwa ya kitaifa
iliyowakuteni ikiwamo kuondokewa na wazee wetu, waliojitolea kufa na kupona,
waliorudisha fedha za serikali kwa sababu waliamini kwamba wamelipwa zaidi ya
walivyotumia na hatuwezi kwa na mfano bora zaidi wa uwajibikaji na uzalendo
kama huu. Nasema jifunzeni kwa hawa kama bado mmebakiza sehemu ya kuingiza
mafunzo mapya kwenye fahamu zenu lakini ikiwa tayari mmekwishakuwa mbwa wazee
wasiofunzwa mbinu mpya, sina jingine la kuwaambieni isipokuwa kuwasalimiwa.
Wasalaaam, ni mimi ndugu yenu Chokoraa wa Muhangaikaji wa
Mlalahoi wa Pangu pakavu wa Kabwela wa Mdanganyika, nawasalimia.
Wednesday, March 7, 2012
Ati! Una "mawazo"!? Kwani ulitakaje?.
Salaam,
Leo siandiki ati kwa sababu nahitaji msomaji, na wala sina kile kiherehere cha kujaribu kujithibitishia kwamba naweza kuandika. Lah! Ninaandika kwa sababu ya kuandika tu hasa kwa vile kuandika kama kusema huyatoa yale yaliyoko moyoni yaani huyafanya mawazo kuwa maneno na ustaarabu wote wa binadamu umejengwa juu ya mambo mawili makubwa, mawazo yaliyotendwa ambayo kifupi huitwa matendo, na mawazo yaliyosemwa ambayo kifupi huitwa maneno na neno hili maneno hutumika mara nyingine kuelezea mawazo yaliyoandikwa kama haya ya kwangu ambayo mara nyingi huitwa maandiko.
Tofauti iliyoko hata hivyo kati ya maandiko, maneno na matendo ni muda wa kudumu na kukumbukwa kwa hizi njia zote tatu za kuwasilisha mawazo. Matendo, hudumu muda mrefu na huonwa na wengi, hata hivyo kwa kadri kizazi kimoja kinavyoondoka na kuruhusu kizazi kingine, basi yale yaliyokuwa matendo makubwa na yenye nguvu na maana kwa kizazi kimoja hubadilika kuwa tu msingi wa matendo bora zaidi, lakini hayaleti tena ule msisimko wa awali.
Fikiria kwa mfano juu ya wazo la mvumbuzi wa simu. Wakati alipowaza kwamba binadamu wangeweza kuwa na njia bora ya kuwasiliana kwa mazungumzo wajapokuwa umbali fulani ikiwa tu watakuwa na chombo chenye uwezo wa kusafirisha mazungumzo yao kutoka upande mmoja hadi mwingine na kurudi, bila shaka kama angerudi leo kwenye dunia yetu hii na kuona jinsi ambavyo sasa teknolojia ya mawasiliano imekuwa hata kizazi chetu hiki kinaamini kwamba kinaishi katika ulimwengu wa teknolojia ya habari na mawasiliano, asingeshangazwa kuona wazo lake la msingi kuwa likiishi hadi sasa, bali angeshangazwa na ukweli kwamba matendo yake yaani chomo alichotengeneza hakitumiki kabisa leo. Mifumo na vyombo vitumikavyo leo kwenye mawasiliano kama tuyajuavyo leo, ni matokeo ya uboreshaji wa mawazo ya yule aliyewaza kwanza juu ya mfumo huo na kuyatia mawazo yake katika vitendo. Ni jambo linaloshawishi kuamini kwamba hakuwa akiwaza mawasiliano kwa mifumo na viwango tulivyo navyo sasa. Na hivyo kazi yake kwa maana ya vile alivyoyatendea kazi mawazo yake vile alivyoyawaza imesahahulika na leo wako wengine wanaoutukuzwa kwa uvumbuzi bora wa mifumo na vyombo vya mawasiliano kuliko Alexander Bell ambaye mtambo wake aliotengeneza yaweza kuwa kwamba hauko leo hata kwenye majumba ya makumbusho . Kinachosemwa hapa ni kwamba matendo japo huwa makubwa na huacha nyuma yake mchango usiopingika, lakini usahauliwa upesi zaidi katika mifumo yote hii mitatuu ya uwasilishaji wa mawazo.
Maneno ya hekima huwa kama msumari uliogongomewa sana katika mioyo ya wale wasikiao, lakini maneno husahaulika haraka zaidi na utuzanji wake hata kwenye ulimwengu ulioendelea kama huu wa kwetu wa sayansi na teknolojia bado ni mgumu sana ukilinganisha na maandiko. Inawezekana pia kwamba maneno hupata zaidi maana yake kutoka kwenye sauti na nota wakati wa kutamka na hivyo japo ni rahisi kusema fulani kasema hivi ama vile, lakini si rahisi kuwasilisha kwa jinsi alivyosema yeye wakati aliposema kwa vile sauti yake ni yake na mvumo wa sauti hiyo wakati akisema neno hilo ulikuwa wa maana sana ili kulipa neno lenyewe maana.
Ndiposa binaadam tangu kale amefahamu umuhimu wa kuandika na sehemu kubwa ya historia ya binadamu iliyotunzwa hata sasa imetunzwa kwa kuandika japo si kuandika kule tukujuako leo. Wamayani kwa mfano, ndiyo jamii yenye historia tajiri kuliko nyingi na ambayo yaonekana kuwa na mchango mkubwa kwenye mambo mengi yatumikayo na binaadamu wa leo, na sehemu kubwa ya maandiko yao yameendelea kutafsiriwa kizazi hadi kizadi yakitufunulia kile walichokijua wakati huo na walichokitegemea kwenye ulimwengu ujao baada yao.
Imani zote za dini duniani, zimejengwa pia kwenye maandiko yaliyoandikwa na wale waliokuwako kabla ya baba zetu na hata sisi na yatakuwako baada yetu na watoto wetu japo imani na uchaji wake hutofautiana toka kizazi hadi kizazi.
Kwa kutambua maana, heshima na nafasi ya kuandika ndiyo maana leo naandika.
Naandika mawazo kwa vile kila binadamu huwaza, naam, hata wale ambao wanadhani hawana muda wala haja ya kusoma, kusikia ama kufahamu mawazo ya wengine, nao huwaza na wanalo hitaji la kufahamiwa na hata kuheshimiwa mawazo yao na ingewasaidia kujua kwamba wako watu wengine wawazao kama wao au hata kinyume chao juu ya mambo kadha wa kadha katika ubinadamu wao.
Kama umesoma mpaka hapa, maana yake umekubali kwamba na wewe huwaza na kwamba unalo hitajio la kujua mawazo ya wengine hata kama hukubaliani nayo na ama unayaona kuwa ni upuuzi lakini bado unajua kwamba ni mawazo.
Labda sasa umebaki ukihitaji kujua ni mawazo juu ya nini? Hili jibu lake ni rahisi tu. Ni mawazo juu ya mawazo kwa sababu maisha yote na ustaarabu wote wa binadamu ni mawazo yaani matendo ni mawazo yaliyotendwa, maneno ni mawazo yaliyosemwa na hata maadiko ni mawazo yaliyoandikwa na hivyo huwezi kumtenga binadamu na mawazo.
Hivyo leo nimeamua wakati nilipoamua kuandika, hilo lilikuwa ni wazo lililotokana na wazo juu ya muda na hivyo nitakushirikisha mawazo yangu kuhusu muda.
Miasha ya binadamu yanaonekana kupata tafsiri yake kwa kutumia muda walau hayo ndiyo mawazo yangu. Wakati tunapozungumzia umri wa mtu, kitu ama taasisi, tunazungumzia muda ambao mtu, kitu ama taasisi husika imekuwapo.
Pia muda ni moja ya vitu adimu lakini visivyohitaji fedha kuwa navyo na ndiyo maana watu wote dunia kote wamepewa muda kwa kiasi sawa. Binadamu na awe upande wowote wa dunia, rangi yoyote ya ngozi yake na hata jinsi yoyote ya maumbile yake, anazo saa kumi na mbili za mchana na saa kumi na mbili za usiku. Katika saa hizi, binadamu hupata nafasi ya kuwaza na kusema ama kutenda mawazo yake.
Wakati binadamu anapofanya shughuli yoyote, anachofanya ni ama kutumia muda wake kutekeleza mawazo yake ama ya wengine. Ukweli unabaki kuwa kwamba binadamu anatumia muda kutekeleza mawazo iwe ni kwa kutenda ama kusema.
Kwa hiyo, kama maisha ya binadamu yangekuwa chakula ama kinywaji, basi tungesema kinywaji hiki kinahitaji mchanganyiko bora wa vitu viwili tu, navyo ni mawazo na muda na kwamba uchanganyaji wa muda na mawazo ndivyo huamua ikiwa maisha ya binadamu huyu yatakuwa mazuri ama mabaya.
Uko msemo miongoni mwetu uliosemwa na wale waliokuwa kabla yetu usema “Hekima ni uwezo wa kutenda ama kusema neno sahihi, mahala sahihi, kwa watu ama mtu sahihi, kwa wakati sahihi, na lugha sahihi”. Ni mawazo yangu kwamba usahihi woote unaweza kuharibiwa tu ikiwa tutapatia maeneo mengine ya kauli hiyo tukakosea usahihi wa muda.
Kwa hiyo kwa maelezo hayo tumeona kwamba mawazo na muda huwekwa pamoja kuleta ama madhara au faida kwa binadamu.
Ni mawazo yangu kwamba muda ni sawa na fedha iwekwayo kwenye akaunti ya benki. Ebu fikiri hivi, kwamba kila siku asubuhi, fulani hukuwekea fedha kiasi cha shilingi themanini na sita elfu na mia nne, na kukwambia utumie fedha hizo kwa kila siku na kwamba ikiwa utabakisha, kiasi utakachobakisha hakitaweza kuingizwa kwenye akaunti yako kesho, bali kesho utapewa kiwango kile kile cha fedha.
Hii ingemaanisha kwamba ungetumia shilingi elfu tatu na mia sita kwa saa moja na kile ambacho ungenunua kwa fedha hizo ni juu yako. Ndivyo na muda. Unazo sekunde 3600 kwa kila saa moja na unachofanyia sekunde zote hizo ni juu yako. Kwa mfano, muda unaotumia kusoma makala haya, utakuwa umetumika kabisa na kuptea milele na ikiwa hutapata faida yoyote kwa kusoma makala haya, basi utakuwa umepata hasara ya muda wote uliotumia kuisoma.
Wakati nikiwaza haya na jinsi muda ulivyo wa muhimu katika matumizi yake, nikaona nikuandikie ili nikueleze ujibidishe kutumia muda wako kuwaza na kutekeleza mawazo yako. Mimi nimewaza kuandika makala haya na nimekuandikia.
Wasalaam,
Chokoraa wa Muhangaikaji wa Mlalahoi wa Pangu pakavu wa Kabwela wa Mdanganyika.
Saturday, February 4, 2012
NAWEKA MOJA CHEMBA.
Chokoraa wa Muhangaikaji wa Kabwela wa Mlalahoi nilipoamua kuwa natembea nimeshikilia "manati ya ndhungu", kuna waliodhani sasa nimeanza kuingia kwenye kutafuta shekeli kwa matumizi ya mabavu, humu nakataa simo. Simo kwa sababu matumizi ya mabavu kwa kutumia hii manati ni hatua nisiyoitaka kabisa, lakini leo nimekuja kijijini hapa kutangaza rasmi kwamba naweka moja chemba. Ndiyo, naweka moja chemba kwa sababu naona sasa ama kuna watu kwa maskudi kabsaaa wanamchezea kichwa mkulu wa kaya na kwa hivyo wanatuchezea vichwa wanakaya wote ama mkulu wa kaya mwenyewe hajali matatizo ya wadanganyika walipa kodi wake na humu naapa sihusiki. Ala! Hivi mwataka ati niendelee kuelekeza mtutu wa hii manati chini ilhali "waishiwa" wanyonya damu ya wadanganyika (mbu) na watema sumu hatari (nge) wamekutana kwa karibu siku saba sasa na hawataki kuzungumzia hali ya afya ya vitegemezi vyangu ilhali wao ndiyo walikuwa tegemeo langu la mwisho kwenye ulimwengu huu wa kupiga domo class 'A'. Nakataa simo. Hivi mnachotaka kuniambia Chokoraa miye mwana wa Kabwela ni kwamba ile timu nzima ya 'ivitaki' pale kwenye "chikale" haijui kwamba wadanganyika tumekuwa kwa juma zima tukimsubiria mkulu wa kaya aseme kitu kuhusu hawa akina "kalumanzila" wa kaya yetu waliogoma kuzama porini kuchimba mizizi na kutoa michemsho kwa matumbo ya watoto!!?. Ati anakuja na nyie mwampeleka moja kwa nne kwenye kufungua majumba ya hela!? Hela gani mtaweka humo ikiwa wadanganyika nguvu kazi ya kaya yetu wanakufa kwa vile hakuna "mshana" unaotolewa huko kilingeni?? Nitoeni humu. Simo, tena simo, simo, simo kabisaaaaaaaaaaaaa.
Naapa mwaka huu mtakiona cha moto wadanganyika walipa kodi nyie maana mmekuwa nyasi kwenye uwanda wa mapambano ya mafahali wa Nyati na Faru na humu simo. Bhaaaa!! Yaani ati kwa vile ninyi mwatibiwa nje ya mipaka ya kaya yetu hii mkituacha wadanganyika tukitaabika, basi mwatuona pia hatuna akili wala uwezo wa kupambanua mambo! Ama kweli ukitaka kumuua mbwa ua kwanza pua zake, nanyi mmeshindwa kunusa harufu ya hasira na chuki za wadanganyika na kwa hili simo.
Nasema, wadanganyeni wengine wooote lakini si mimi mwana wa Muhangaikaji maana mimi ninayo macho, tena makubwa kama ya bundi naona vyema usiku kuliko mchana na hivyo hamnidanganyi enyi mchekao nasi mchana ilhali usiku mwatuua gizani na kuhudhuria mazishi mchana mkivalia sura za uongo na kweli muonekane wahuzunika nasi, nasema simo.
Ha ha ha ha ha, nacheka miye kitukuu wa Kabwela kwa sababu nawajua ninyi hata kutokea mbali maana macho yangu ya ndani yanaona hata mjapo ninyima kuona kwa macho ya nje mtendapo mtendayo kwa siri na hila, lakini nikiuona mwisho, naujua mwanzo wake na kwa hili nasema mnitoe!. Ala! Kwani si ni nyie wenyewe wana wa ‘ifitaki’ mliokuwa hapo mwanzo mkimweka mkulu wa kaya mbele ya luninga zetu huku mkimfanya kuongelea mambo ambayo yalipaswa kuongelewa na liwali wala si mkulu wa kaya na kutufanya wenye akili kushangaa kwa nini mwamvunjia heshima namna hii!!? Yuko wapi sasa kuzungumzia madhira yenye kuwagusa wadanganyika, madhira ambayo neno lake tu, roho za wadanganyika arobaini milioni na ushee zingepona, nasema kwa hili mimi nakuwa wa kwanza kusema “Amina”.
Ndiyo nasema amina maana musa alitangulia kuwajua enyi wana na akaandika akigiaza walaaniwe wampotezao mgeni njia na watu wote waseme amina na mimi kwenye hili ni wa kwanza “Amina”.
Najua mtasema nabwabwaja mambo nisiyoyajua lakini haya ninayoyajua ninayajua na ninayasema kwa usahihi ili mwenye masikio asikie, mmempoteza njia aliyepaswa kuongoza njia na humu simo. Nasema simo kwa vile wote twasafiri na tuendako wote twapajua, basi kelele na manung’uniko haya sit u ni mazao ya ‘ domo ghasia’ kama msemavyo ili msadikiwe na wazandiki wenye kuwapa vipande vya chupa ilhali wakiondoka na almasi yenu, bali ni hisia za wazi kwamba wadanganyika waliokuwa siku zote wakijua kwamba ni wadanganyika na kujivunia kudanganyika, sasa wamechoka na wanataka uhakika na kwenye hili nasema mnitoe.
Mnitoe, tena simo kabisa. Naam, kwa sababu najua mnajua ya kwamba hamna majibu ya maswali yaulizwayo na sasa mnataka tunyamaze tusiulize si kwa vile tunauliza upuuzi bali kwa vile hamkujua kwamba wakati unakuja tutawauliza kwa habari ya talanta ya “kula” mlizopewa na wenye kukasirika na kupiga ‘kura’ ili wapate kula kuambulia kuliwa, humu namo simo.
Ala! Hivi nyie ndugu wawili wa mdanyika yaani Mbu na Nge mmeanza lini tabia hii!!? Ha ha ha ha ha ha ha ha, nacheka miye maana najua wadanganyika walidanganyika walipodhani kwamba wakiwaweka ninyi pamoja yaani mbu kwa sababu ya sauti yako nzuri ya kubembeleza huku ukinyonya damu na kuwacha virusi, basi ungenyonya kwa wanyonyaji na kuacha virusi kwao ili ulete faida kwa wadanganyika, sasa najua kwamba walidanganyika, na ninaapa simo. Walidanyika walipodhani Mbu na Nge wakiwekwa pamoja wataleta uwezo wao wa kunyonya damu na kutema sumu hili kuleta nafuu kwa niaba ya wadanganyika walipa kodi kumbe hawakujua kwamba kwenye kijiji cha waishiwa kuna kaugonjwa ka ‘metamofisisi’ kanakowabadili wadanganyika wanaoingia kijijini humo kuwa ‘waishiwa’ na kusahau udanganyika wao na humu nakataa kuwamo.
Wacha nicheke miye maana najua sasa wakati u karibu. Ndiyo, wakati wa Chokoraa kuambiwa anyamaze na asiseme anayosema na kama bado anataka kusema basi aseme watakayosema wale wenye mamluki na si mamlaka ya kusema na humu nasema sitakuwamo maana simo. Nasema wakati wanaosema sasa watakapotakiwa kunyamaza na walionyama kutakiwa kusema, wanaodanganyika sasa watakapotakiwa kuambiwa ukweli na wakweli kudanganywa, wakati huo mjomba shangazi na binamu hawatafanya tena maamuzi kwenye jumba kuu la mashauri na hapo walau hadhi na heshima ya mdanganyika itarejea, lakini kwa vile njia ni ndefu yenye kugharimu machozi jasho na damu, Chokoraa najitoa, simo, tena simo kabisaaaaaaa!!
Salaam, ni mimi nduguyo wa damu, Chokoraa wa Muhangaikaji wa Mlalahoi wa Pangu pakavu wa Kabwela wa Mdangayika, nakusalimia.
Saturday, January 14, 2012
Wadanganyika na Kelele za Mlango.
Ngoja kwanza nicheke. Ha ha ha ha ha ha ha!!! Nacheka miye Chokoraa wa Muhangaikaji wa Mlalahoi wa Pangu Pakavu wa Kabwela wa Mdanganyika. Leo, tofauti na siku zote ni furaha. Ndiyo, mwaka huu umeanza kwa mafanikio makubwa na kwa hilo namshukuru ‘Mulungu’. Ona huyu naye anakereka ati kwa vile nimemwita kikwetu huyu ambaye yeye angetaka aitwe “God” ili ajiridhishe kwamba yeye ni mtumwa. Naapa simo.
Nina furaha kwa vile mwaka huu Chokoraa nimepanda daraja, halafu nimepanda daraja mwanzoni mwa mwaka, ha ha ha ha ha ha!! Unashangaa!! Kwa sasa Chokoraa silali tena kwenye mitaro na huko hunikuti, nimepanga kichumba changu kimoja huku kwetu Uswazi kwenye kajumba ka mama Chausiku na hivyo silali tena chini ya daraja. Nani kasema hilo ni jambo dogo!?
Japo misosi yangu ni kule kule majalalani kama kawaida, lakini mara hii nafikiri hata majalala yangu itabidi yabadilike kidogo hasa kwa vile inabidi niwe kibiashara zaidi ili niweze kulipa kodi. Hilo nitakuhadithia ila leo, nataka kukueleza kero moja tu iliyonikuta. Kero ya mlango.
Kila mara “Ng’waaaaa!! Ng’waaaaaa!! Mlango huu wa bati unapiga kelele kila unapofunguliwa na Chokoraa hili linanikera lakini kinachonishangaza ni kwamba mama Chau na watoto wake wala hilo haliwasumbui, nasema kweli mi nashangaa sana. Ene wei, baada ya kuishi hapa walau kwa wiki mbili, nimeanza kuzoea hali hii na hivyo na mimi sasa naweza kulala na hiyo kelele hainisumbui sana isipokuwa pia hunisaidia nyakati fulani fulani, hilo nitakueleza siku nyingine.
Ndipo siku moja nikiwa nimejilaza hapa kwenye kitanda change cha kamba na hasa kwa vile siku hiyo nilikuwa sijatia kitu kinywani hadi hiyo saa sita ya usiku, nikabaki kuhesabu ‘kenchi’ na misumari na kupata nafasi ya kutafakari na hata kuzilinganisha kero za hapa kwa mama Chau na kero za kelele za wadanganyika walipa kodi kama ambavyo nimekuwa nikishuhudia kwenye kurasa za magazeti.
Ngoja kwanza! Nani kasema Chokoraa huwa sisomi magazeti!? Mwongo. Huwa sinunui magazeti hasa kwa vile matukio mengi yanayotokea huku mtaani huwa nayaona mwenyewe na sitaki kuyanunua tena yakishatiwa nakshi za wino hasa kwa vile huwa tayari yamechakachuliwa ili kuleta radha ya si hasa, lakini huwa nasoma magazeti na hapa kwangu si ajabu ukakuta magazeti kadha wa kadha kuanzia yale yaliyofungiwa maandazi, vitumbua, samaki au hata chips dume na kila nipatapo nafasi huwa najisomea hivyo vipande na usiniambie eti siyo magazeti.
Ndiyo. Nakumbuka Wadanganyika walivyokuwa wamedanganyika na kuhamasika hadi kutaka kuingia barabarani kuandaa mana ili iliwe na watoto wao baada yao ati kwa vile walichoshwa kula nyama ilhali wakifyatua matofari ya utumwa na hivyo wakajiandaa kuandaa mana. Weeee!!! Koma. Kwani waliandaa mana hata hivyo!? Wapiii!! Walifanya maandalizi yao yoote na matangazo na kila kitu halafu ati kuna jamaa mmoja mwema katika wema wake akagundua kuna mashababi mjini wanataka ati kuwadungua wadanganyika wote watakao andaa mana, basi kwa wema wake akawaonya wadangayika na wao wakanyewa kimyaaa!! Ama kweli rahisi sana kuwadanganya wadanganyika.
Ni juzi tu wakati nasoma hiki kipande cha gazeti kuhusu hayo maandalizi ya kuandaa mana na jinsi yalivyozimwa kwa wema wa mwema na vijana wake, ndipo nilipogundua kumbe wadanganyika wengi wanaishi kama milango ya nyumba ya mama Chausiku. Nasema usidhani nakutusi ewe mdanganyika mlipa kodi, lakini nakuuliza, ziko wapi zile hasira ulizokuwa nazo na kampeni kubwa ulizofanya ili kuandaa mana kwa ajiri ya kizazi kijacho baada yako hasa kwa kuzingatia kwamba ikiwa hivyo vijisenti yako uchwara vingelipwa kwa ajiri ya kusafisha hilo “Doa la Nzi” kwenye shati jeusi lenye harufu ya kinyesi, basi vizazi vijavyo vingepata hasira itokanayo na hasara na hata kufikia kuukana udanganyika wao?! Kwani hao mashababi walikuwa wangapi hata nchi nzima inasiamama wima kuwaacha hawa jamaa wapite!? Hata kama walikuwa wengi na waliojisheheneza sira nzitonzito na za maangamizi, walikuwa wapi na walikusudia kukaa muda gani au ndiyo wamehamia na hivyo sasa hatuwezi kufanya lolote kwa sababu kila tutakapojaribu kutoka nje ya milango yetu basi tutapambana na hawa mashababi!!? Nafikiri katika wema wake, huyu nduyu yetu mwema angetwambia basi kwamba hawa mashababi ama wamedibitiwa au wamekwishaondoka na hivyo tuendelee na maandalizi yetu ya kuandaa mana ili kizazi chetu kisifie jangwani kwa ukosefu wa chakula!. Humu mimi simo.
Nikakumbuka pia kwamba baada ya maandalizi ya mana kushindikana, waheshimiwa wawili akina Mbu na Nge nao wakaja kwa umoja wao wa Mbu-Nge kutaka nyogeza ya posho na hapa wadanganyika wakakasirika hadi povu kuwatoka midomoni. Nikahisi labda mara hii, wadanganyika hawa hawatadangayika. Wapi!! Kwa mara nyingine wakazidiwa na kile kibinti huwa nakiona kwenye vile visanduku vya picha kikisema kwa sauti kubwa “Sidanganyikiii” maana wandanganyika ghafla wakadanganyika na matukio ya mafuriko na mengineyo na kusahahu kwamba kuna visenti vyao kibao vyaliwa na ule umoja wa “Mbu-Nge” na wao wakibakia kuwa wadanganyika walipa kodi.
Mara mlango wa nje wa hapa nyumbani kwa mama chiku ukasukumwa ila mara hii polepole nafikiri kwa vile huyu anayefungua anajua kwamba watu wameanza kulala na hataki kuwasumbua na hivyo japo ulipiga kelele kama kawaida yake, lakini bado nasikia mikoromo ya usingizi ya mama Chiku na vitegemezi vyake ndipi nikakumbuka, kweli kele za mlango, hazimzuii mwenye nyumba kuuchapa.
Mi ninaomba kuuliza, hivi Wadanganyika mnaugua ugonjwa gani huu!!? Nasema usikasirike na wala usininune na hata ukinuna mi nina manati ya ndhungu sikuogopi ng'o! wacha nikuuliza na jibu nalitaka. Kwanza, mlitaka kuandamana ili kushinikiza sirikali isiwalipe "Doa la Nzi" mabilioni ya visenti vyenu vya madafu, mkachapwa mkwara na yule jamaa mwema mwenye kuwatendea wema hata wasio wema akiwaambia ati kulikuwa na tishio la wale mashababi, mkanywea. Hivi hilo tishio halijesha au ndo mmekubali kuliwa enyi 'wapinga kula'!? Nasema yule mwema katika wema wake atwambie kama wale mashababi wamekwishaondoka na kurudi kupamba na Kenya na Amisomi ili Chokoraa niandamane maana bado nataka kuandamana. Hamtaki kuhoji nawauliza wadanganyika mwaumwa ugonjwa gani?!. Wabunge walipojiongezea posho, mkaandika mpaka kwenye bulogu zenu, mkanuna hadi sura kuwavimba na kisha haoooo mkanywea. Nawauliza, hivi juhudi zenu zimefikia wapi ama mmebakia kuwa milango ya bati na bawaba kavu zenye kupiga kelele nyingi hata kwa kuguswa na mende ilhali mkiwaacha wenye nyumba yenye siri kali walele fofofo!!? Simo, nasema simo tena mntioe humu simo kabisaaaaaaaa.
Salaam nakusamilia, ni mimi nduguyo Chokoraa wa Muhangaikaji ,wa Mlalahoi, wa Pangu Pakavu, wa Kabwela ,wa Mdanganyika.
Tuesday, January 3, 2012
Usalama usio salama wa Barabarani.
Kiherehere hiki!
Leo ati Chokoraa na mimi nimejikusanya na baadhi ya wananzengo hapa mtaani kwetu, tumekazunguka haka kasanduku kanakoonyesha sura za watu wakiongea na sauti zao twazisikia ati ninyi mwaita tivii. Uliza sasa tunaangalia nini! Duh! Nachoka miye mwana wa Muhangakaji kitukuu wa Kabwela.
Tumekaa tunaangalia Taarifa na Habari. Wewee!! Nani kasema nimekosea?! Nani!!! Tena!!! Angalia usiniudhi mapema nikazira kukuhadithia hata tukio lenyewe. Kwani ile ni “Taarifa ya Habari, Taarifa za Habari, Taarifa na Habari?!!. Nadhani lile baraza la wanaokifahamu Kiswahili kuliko sisi wengine inabidi watusaidie kwenye hili.
Ala! Unaona sasa!! Hadi nimesahau nilichotaka kukwambia kwa vile umenitia hasira. Hata hivyo nadhani nimejaribu sana kutumia lugha yenu ya kistaarabu sana ilhali mi siifahamu hiyo lugha yenyewe. Wacha nitwange kichokoraa sasa ndo tuelewane. Simo.
Nasema kwenye hili la kulalamika na kunung’unika kwa kila kitu simo, tena simo hata kidogo, simo kabisaaaaa! Ala! Hivi, si kila mwisho na mwanzo wa mwaka kumekuwapo na lundo la ajari barabarani na nyingi zikisababishwa pamoja na mambo mengine uzembe wa madereva na kukosa ujuzi na sifa stahiki za kuendesha magari!? Kwani kuna mtu kati yetu hajui kwamba hali hii imechangiwa kwa kiasi kikubwa na uzembe wa vyombo vyetu vya ulinzi na usalama hasa wa barabarani yaani ile mamlaka ya kuzibiti barabara na maji almaarufu kama ‘chuma tule’ na vikosi vya ‘usaha alama za barabarani’ kwa umoja wao? Hilo halinikasirishi hata hivyo.
Linalonikasirisha hadi nimewaandikia waraka huu, ni hili la wadanganyika walipa kodi kujifanya kulaumu “sirikali” kwa kila kinachofanywa hata kama ni kizuri. Hivi si nimeona mkipaza sauti mishipa ya shingo kuwasimama mkilalamikia kukatizwa safari zenu kwa sababu ya zoezi la ukaguzi wa “liseni’ za udereva ili kujua wale walio ‘liseni’ darasani kabla ya kuanza kuendesha na wale ambao wanaendesha bila kuanza ‘kuliseni’!! Nasema kwa hili mnitoe.
Ona sasa. Yaani wakati watendanaji wa ‘sirikali’ walipojipanga ki ‘stratejiki’ kabisa kwa kuzingatia ‘taimingi’ ya muda ambao ajari zinazidi na kujaribu kuokoa maisha ya wadanganyika, mwalalama! Mwalalama nini enyi wana wa danganyika yetu!? Naapa simo humu. Ona hyu naye anachukia ati kwa vile nachanganya kikoloni katikati ya sentensi zangu. Utajuaje kwamba “Nshomile mpaka fomu fooo!!!” Kalagabaho kama hujaelewa, kwani hilo mi Chokoraa lanihusu!? Simo nasema.
Nasema kwenye hili, badala ya hasira zangu kuzielekeza kwa hawa wana usalama japo si salama, ningezielekeza kwa wamiliki wa haya madude yaliyofanyika wajumbe wa malaika mtoa roho kila mwanzoni mwa kila mwaka. Washangaa nini!! Ningezielekeza hasira zangu kwao kwa vile kila mwajiri anapomwajiri dereva anamuuliza kuhusu leseni na ikiwa mwenye gari anaruhusu dereva asiye na leseni kuendesha gari lake, mwataka nisimwelekezee hasira zangu kwa nini!!? Naapa kwa hili tutashindana sana, lakini simo.
Halafu!! Ebu niwaulize enyi wana wa usalama japo si salama, huu utaratibu wenu wa kuvamia tu maeneno na kuanza kutekeleza majukumu yenu bila hata kuzingatia kwamba Chokoraa miye mwana wa Muhangaikaji, naam, mimi huyu mjukuu wa Mlalahoi kilembwe wa Kabwela, mara nyingine ninatoka nyumbani na tiketi tu na ziada ya shilingi elfu mbili kwa ajiri ya maji na nauli ya ‘bodaboda’ nikifika huko niendako na hayo mengine namuachia maulana, mmeianza lini!?
Naapa kwa ubabe huu sina hakika kama mnafanya ‘upolisi jamii’ kwa sababu mnashindwa kuzingatia mahitaji ya jamii yenyewe katika utekelezaji wa majumu yenu kwa sababu hasa mahitaji ya Chokoraa miye hayaishii kwenye kusafiri na kufika salama bali pia kuzingatia matumizi ya kila ‘shekeli’ (iite ‘sinyingi’ kama hilo ndilo jina ulipendalo) ninayoitumia na ninavyoitumia wakati wa safari na ndiyo maana japo naona kama lengo lilikuwa zuri lakini kwenye utekezaji wake simo, tena simo kabisaaa!.
Nasema iweni na huruma na maisha ya sisi wajukuu wa Pangu Pakavu kwa sababu kila mara tumekuwa tukisema tieni mchuzi lakini hamtaki, naapa simo. Hivi mnadhani wale wadogo zangu akina Mzembe na Mzururaji ambao walikuwa wameng’ng’ana kuishi mjini humu kwa kuningezea shughuli ya kuwalinda na kuwahudumia mimi kaka yao Mkubwa, tajiri wa ukoo kwa kipato cha kunanga, Chokoraa wa Kabwela, na sasa walikuwa wameamua kurudi kijijini, si wamehairisha baada ya magari kuchelewa kuondoka na wamerudi kwenye lile pagala tunakojikusanya usiku na kujirundika tukipitiwa na usingizi ilhali tukiita huko ni kulala!?. Nasema hamjui ni kiasi gani ya gharama na maumivu ya moyo mmeniongezea mwaka huu na ndiyo kwanza unaanza. Naapa mpaka umelizike, tutaonana wabaya. Simo.
Na nyie ‘chuma tule’ hivi kweli na akili zenu zoote mmeshindwa kutengeneza ‘mpango mkakati’ (naogopa kusema ‘sitrateji’ msijesema napenda sana kikoloni) wa jinsi ya kukagua walio ‘liseni’ na kuwa lessen wale wasio nazo bila kunisumbua miye Mdanganyika Mlipa kodi!!? Naapa utaalamu umesafiri kwenye inchi ya wadanganyika walipa kodi. Simo, tena simo kabisaa.
Haya, tekelezeni majukumu yenu na wala msijesema mimi nawakataza kutekeleza majukumu yenu maana nafahamu mnayo sheria ya kuitumia kuniyamazisha miye hati kwa vile nimekuwa domo kaya wakati huyo ni mpwa wangu mimi jina langu ni lile lile le siku zote, Chokoraa wa Mdanganyika wa Muhangaikaji wa Mlalahoi wa Pangu pakavu wa Kabwela.
Haha ha ha ha ha ha ha! Nicheke niongeze siku miye.
Salaam nawasalimia,
Chokoraa wa Muhangaikaji.
Subscribe to:
Posts (Atom)