Tuesday, October 16, 2012

Nasema tena kama nilivyowahi ksema ili msijesema mi sikusema wakati watakaposema wale waliosema mapema, kuchanganya "si hasa" na taaluma ndiyo ugonjwa unaowaumiza wadanganyika walipa kodi na mimi humu Simo. Haya tena, Dk. Robert Ntakamulenga awafungulia SBS baada ya kuwa wamefungiwa kwa tuhuma za kuchafua mazingira. Chokoraa nilikuwapo kushuhudia na humu mi simo.
Dk. Ntakamulenga akitoa maelekezo kwa mkurugenzi Mtendaji wa Supply Base Solutions (SBS) Ltd kuhusu hatua za kuchukua kuhakikisha usalama wa mazingira kwenye eneo la Mdenga, kata ya Likonde wilaya ya Mtwara Mikindani.

Dk. Ntakamulenga (kushoto), Mkurugenzi Mtendaji wa SBS Bw. Ganeshani Vedagiri na mshauri mwelekezi wa mazingira Bw. Abel Sikaona wakitazama bwawa maalumu la kuchuja maji kwenye kiwanda cha kutekeketeza takataka kinachomilikiwa na SBS.

Afisa Mwandamizi wa mazingira kutoka baraza la mazingira Tanzania (NEMC) Bi. Nengia Mollel (kushoto), mwanasheria wa NEMC Bw. Heche (kulia) na mtaalamu kutoka ofisi ya mkemia mkuu (mwenye Tshirt ya blue bahari) wakisikiliza maelekezo kutoka mmoja wa Wakurugenzi wa NEMC Dk, Robert Ntakamlenga.
Mafundi wa kampuni ya SBS wakiwa kazini kwao wakati wa ziara ya Dk. Ntakamlenga kwenye kiwanda chao.
Afisa Mwandamizi kutoka NEMC Bi. Nengia Mollel akirekodi kumbukumbu zake wakati wa ziara ya wataalamu hao kwenye kiwanda cha uchomaji taka cha SBS kwenye mtaa wa Mdenga, Manispaa ya Mtwara Mikindani.



Mkurugenzi Mtendaji wa kampuni ya SBS Bw. Ganeshan Vedagiri akitoa maelezo kwa mkurugenzi wa NEMC wakati wa ziara ya mkurugenzi huyo kiwandani hapo.
Bi. Nengai Mollel akitoa maelekezo kwa wenyeji wake wakati wa ziara hiyo. Huyu Mrembo, duh!!!. Sisemi. Kushoto kwake ni Mkurugenzi Mtendaji wa SBS akimsikiliza kwa makini.

Mshauri mwelekzi wa mazingira wa SBS Bw. Abel akijieleza mbele ya Dk. Ntikamlenga.

Sikiliza hii. Simo.

NA KUTOKA MKOANI MWANZA UCHAGUZI WA NDANI WA CHAMA CHA MAPINDUZI (CCM) WAIBUA MAMBO MAZITO.

Jiji la mwanza, hasa huku kwetu uswazi, Ha ha ha ha ha ha!!! Simo.

Waziri na Mbunge wa Zamani wa Jimbo la Ilemela mkoani Mwanza Bw. Antony Diallo, aibuka mshindi wa kiti cha mwenyekiti.
"Muishiwa" sana Antony Diallo akitoa neno la shukurani kwa wajumbe baada ya kuchaguliwa, kulia kwake ni 'Muishiwa' wazi hili Lukuvi.

Mh. Lukuvi naye alikuwa na neno kwa wajumbe.


Mstahiki Meya wa Jiji la Mwanza na Diwani wa Kata ya Mkolani Mh. Stanslausi S. Mabula naye alikuwapo kushuhudia kinyang'anyiro hicho. Sihusiki.


Thursday, October 11, 2012

Chokoraa nahama 'Mjini'.



Nawaomba msihoji uzalendo wangu na wala msinione mwoga ila nasema wazi Chokoraa nahama mjini.  Naapa kwa jina lake mama yangu Shida wa Matatizo binti Huzuni wa Sikitiko wa Taabu Mateso Mengi humu simo , tena simo kabisaaa. 

Nasema tena msijesema sikusema na naweka kumbukumbu sawa kabla sijafunga vilango kurejea zangu shamba kwenye kile kibanda cha marehemu bibi yangu alichoachiwa na marehemu mumewe Kabwela wa Mdanganyika, na hapo ni ikiwa hakijauzwa kwa bei chee kwa mkulima wa matuta hamsini ya nyanya ila mwenye umaarufu wa harufu kwa vile anapaka yale marashi ya siku hizi yajulikanayo humu mjini kwenu kama ‘Ukewenzaji’ na humu simo.  Simo.
Salaale!! Mwanitisha enyi wana na sasa sijui ikiwa nikitoka kwenye pagala langu kwenda kuokoteza majalalani niwaambieje wadogo zangu akina Mzembe na Mzururaji ama kwamba ‘tutaonana jioni’ ama niage kabisa!? 

Ati washangaa!? Washangaa nini ikiwa siku hizi kukiwako tu na taarifa za “kiintelijensia” kwamba Chokoraa wa Muhangaikaji wa Mlalahoi wa Pangupakavu wa Kabwela wa Mdanganyika anaunda mabomu ya ‘nyuki hulia’ hakuna anayejali hata kutaka kutumia walau sehemu kiduchu ya ‘intelijensi’ yake kupima ikiwa kweli ‘intelijensia’ hizo ni sahihi anachofanya ni kuvuta  “manati ya ndhungu” na halengi miguu bali kichwa!? Naapa, kaya ya wadanganyika si salama kwa akina Chokoraa, labda kaka zetu akina Mstahiki na Muishiwa wao kwa vile wanafanya makosa yaliyofanyiwa upembuzi yakinifu. Wallahi twahitaji tena akina Nyerere na Kwame Nkurumah na humu mi naapa sihusiki. 

Kwani mmeanza leo enyi walinzi wa amani mliogeuka kuwa wavuruga amani na sasa mmekuwa tishio la raia!? Nani hajui  Wambeya walivyopoteza vitegemezi vyao kwenye ‘risero’ na bado tukaambiwa na ‘kamati teule’ juu ya ‘makosa ya kiufundi’ na kwamba hatua za miguu zimechukuliwa kukomesha vifo hivi!? Hamkutosheka enyi wana na sasa kila aliye na “manati ya ndhungu” akijisikia anadungua yeyeote amtakaye!  Naapa kwa Muumba wa mbingu na ardhi Chokoraa nina mashaka na kichwa changu maana mawe ya manati zenu yanaviona zaidi vichwa vya Kunguru kuliko Mbuni kisa si kwamba Kunguru ni mwizi sana, lakini anawanyima usingizi akina Mbuni waishio kwenye majumba ya starehe na humu miye simo. 

Kwani nini tofauti kati ya Punda na Farasi au Kunguru na Mbuni isipokuwa aina ya maisha waishiyo ilhali wote wakiwa ni ndege na wayama na humu miye nahusika kwani!? Kama haikuwatosheni enyi wenye dhamana ya uhai na mamlaka ya kuutwaa wa kwetu na kuutoa sadaka huku mkijisafi kwa ‘mizimu weupe’ kwa damu zetu na wao wakiwapa ‘manati’ zaidi kwa vile hilo hasa lawaongezeeni ninyi uishiwa na wao ‘shekeli’ zitokanazo na ‘mali asili’ za ardhi yenu hii ya wana wa Hamu, mkawachukua baadhi ya kaka zetu na kuwapeleka kwenye ule msitu mkuubwa mtoleako sadaka za damu ya wana wa Adamu na kuwachinjilia mbali na kisha mkatwambia  “yarikuwa yakipambana na ‘hofu ya raia” tukakaa kimya si kwa vile tuliwakubalia bali kwa vile tuliogopa kesho isiwe zamu yetu. 

Nasema hata pale mlipoanza kuchunguzana huku mkikonyezana na kuzungumza kwa uchungu wa kujifanya, Chokoraa nilijua igizo hili limemkosa tu Muhogo Mchungu lingenoga lakini sikufumbua kinywa hadi ati “siri kali” ilipopoteza kwenye shauri hilo watoto na wake wa ‘wajasiria mlo’ wale wakabaki wajane na yatima likaisha. Nina uchungu lakini simo. 

Kama haikuwatosha ni hivi majuzi tu mkaamua kumuua sisimizi kwa risasi ya Tembo ati kwa vile sisimizi huyu ni mmoja wa wale wenye kupanda kwa siri kwenye nguo zenu na kuyajua yale tusiyoyajua na kisha kuyaanika hadharani, naapa hii tabia ya “hivi unanijua!” itawamaliza wanaobaki mjini maana Chokoraa siji tena mjini na humo wala msinihusishe maana simo. 

Haya, jiosheni muosheke basi kwa wana na mjane wa Yule mliyemtandika bomu la machozi na kumtoa damu ya uhai kama mwaweza.  

Haya, tena juzi juzi  tu wanafunzi wakiwa kwenye michezo ya kujificha kwenye eno la hifadhi, wenye manati za ndhungu, tena za ‘siri kali’ ya kaya yao, wamewakomelea hadi umauti na Chokoraa nauliza, hivi mwawapima vyema hawa mnaowakabidhi hizi manati au kila mmoja sasa anaweza kubeba manati na akiogopa kidogo tu basi anadungua!? Jibu msinipe, lakini wafundeni basi walau kwamba watumia ‘intelijensi’ zao kuamua ikiwa intelijensia wanazopata zinatosha kuwapa kibali cha kudungua ama lah, vinginevyo Chokoraa sirudi mjini na humu mi sihusiki.


Ni mimi ndugu yenu Chokoraa wa Muhangaikaji wa Mlalahoi wa Pangupakavu wa Kabwela wa mDanganyika nawasalimia. Simo.

Thursday, September 27, 2012

Mji wa Mafia (Kilindoni) na viunga vyake.

Nauliza hivi! Mafia si mji wa utalii!!? Inakuwaje mwaliacha soko la mji huu kuwa chafu kiasi hiki? Haya siyo maji yaliyotuama kwa sababu ya mvua maana msimu wa mvua kisiwani hapa bado, lakini ni maji kutoka kwenye vibanda vya 'Mama Lishe' walioko ndani ya soko kuu la Mafia. Simo humu naapa.

Tungali bado kwenye viunga vya mji wa Mafia na hapa ni sokoni. Ha ha ha ha ha ha!!! Nicheke ninenepe Chokoraa wa watu.
Huku ni mwendo wa "ushungi" aisee, Usije na vimini na vipedo vyenu mnavyovalishana mkituonyesha siri zenu enyi wana na humu mi simo.

Chokoraa nilipata pia nafasi ya kutembelea ofisi ya Mkurugenzi Mtendaji wa Wilaya ya Mafia na hili ndilo jengo la "Muishiwa" huyu. Ha ha ha ha ha! Ati hapo inapopepea bendera ya kaya yetu hii, miaka kadhaa kabla ya 1961 ilipepea bendera ya "mkoloni". Simo humu miye.

Usiache kunitumia barua na hata kifurushi kutokea huko kwenu ughaibuni kwa anuani ifuatayo: Mheshimiwa Chokoraa wa Muhangaikaji wa Mlalahoi wa Pangupakavu wa Kabwela wa Mdanganyika, S.L.P .....Mafia, Pwani ya Wadanganyika. Pia biashara ya kuuza vocha inaendelea hapa na mimi nauliza haya makampuni ya simu yanalipia ushuru!!!!? Simo.
'Prezidenti' wa Wilaya, D.C ama ukipenda Mkulu wa Kaya wa Mafia ana ofisi zake hapa na hili lote ni jengo la ofisi za "muishiwa" huyu. Ati! Mtu mmoja jengo lote hili na mwalimu aliwahi kuuliza "...kwani mi tembo?". Na hii je!!!!!? Sihusiki naapa, simo.
Usitie shaka kuja na Njuluku, Pesa, Sinyingi, Hela, Chokoraa naita "Shekeli" zako huku kwetu maana hata sisi tunayo "Nyumba ya hela" na inayo "Ei tii Emu" inayofanya kazi saa 24 mfululizo. Sihusiki bado.
Uwanja wa ndege wa Mafia. Jengo hili halitumiki kwa sasa kwa sababu uwanja uko kwenye matengenezo makubwa ukitarajiwa kuwa na jengo la kisasa kabisa lakini hii ndiyo hali halisi miaka 50 baada ya uhuru. Sihusiki mimi humu..
'Muishiwa' Batuli, Diwani wa Kata ya Kirongwe, Kata ya Kaskazini Mafia akielezea jambo tulipokutana naye kwenye kijiji cha Jimbo huko Mafia. Wa kwanza kulia ni Dk. Kiwia, mtaalamu wa Uvuvi wenyewe twaita Fisheries. Nahusika kwani miye humu!!!? Simo.
 Dk. Kiwia kutoka Fisheries, Ndg Makongoro mtaalamu wa mazingira, Chokoraa wa Muhangikaji wa Mlalahoi wa Pangupakavu wa Kabwela wa Mdanganyika, 'Muishiwa Diwani wa Kirongwe, Muishiwa Mwenyekigoda wa Kijiji cha Banja wakimsikiliza mwananchi akidadavua mada kwenye mkutano. Ha ha ha ha ha!!! Nijitoe na humu?. Simo.

FOTOA FOTO YA CHOKORAA KISIWANI MAFIA.

Nasema humu Chokoraa sihusiki na simo tena simo kabisaaaaa!!! Ala! Nani kakwambia Chokoraa nakaa jalala moja!? Nilikwenda kisiwa cha Mafia juma lililopita na katika pita pita yangu kwenye majalala yangu nikakutana na hali hii, nikaamua kufanya katabia kangu kaleeee ka zamani nilikokatazwa nisisikie yaanI "FOTOA FOTO". We kuwamo humu japo mi simo tena simo kabisaaaaaaa.
Kwanza ni "Usafiri" wetu. Hapa kwetu Mafia hatuna "Teksi" na wala huo upuuzi wenu wa kutumia magari hata kwa safari fupi kisa mwaonyesha ufahari wa kuwa na mafedha kedekede sisi hatumo na humu Chokoraa nilikataa kuhusika. Kuna njia mbili tu za kuingia kisiwa hiki chenye utajiri wa mali na utu na mara unapofika ama kwenye bandari yetu kongwe isiyoendelezwa bado ukitumia usaifiri wa "boti" kutokea Nyamisati au wale "waishiwa" msiochoka kuishiwa mkijifanya kutumia "ulozi wa ndhungu" kwa kupanda 'ungo' mchana kweupeeeee! Na humo simo, hata hivyo usaifiri wako wa kuzunguka mjini humu ni pikipiki iwe ya matairi mawili almaarufu "Bodaboda" ama matairi matatu almaarufu "Bajaji". Teksi zenu tupa kule!!! Simo nasema.
Halafu! Huku kwetu ule uchafu wenu muutiao barabarani mkiifanya nyeusi tiii kama mkaa ati wenyewe mwaita lami huku sisi upuuzi huo hatuna hata mmoja. Huu mji wa kitalii bwana lazima uwe "nechuro". Ha ha ha ha ha ha!!! Sihusiki miye humu naapa.
Halafu nani kasema ati wanawake wa Pwani hawajui kutafuta pesa ila akina "Manka" peke yao!!!? Nyooo!! Simo. Hapa kwetu sokoni kwa lugha ya 'Ami' yangu wa kule Mchambawima paitwa "Malikiti" akina mama wanauza kitoweo. Yaani akina baba wavua, na akina mama wauza na wote watia kipato ndani ya nyumba sasa hilo la haki sawa mwalikataa kwanini!!!? Simo humu miye.


"Si hasa" za Kaya yetu nazo zatuhusu na sisi twahusika. Hapa ni kikao cha kamati za vijiji vya Banja na Jojo kilichofanyika shule ya msingi Banja ambapo wanavijiji hawa walikutana na wataalamu wa mazingira na hapa mmoja wa wanakamati akihoji swali na kutoa maoni yake. Ha ha ha ha ha!! Nisifurahi kwanini Chokoraa miye.


Kwenye kikao hiki, ndugu yenu Chokoraa wa Muhangaikaji wa Mlalahoi wa Pangupakavu wa Kabwela wa Mdanganyika nilikaribishwa niketi na mimi pamoja na wakuu na sikufungua kinywa kunena bali kusikiza yale yaliyosemwa na wana kaya maana simo.

 Huyu si mgonjwa jamani kwamba anakandwa mkono umevunjika ama kakutwa na madhila. La hasha! Anapambwa mtoto wa kike kabla ya harusi na kama huyajui haya basi hujafika Pwani weye na mi humo simo, tena simo kabisaaaaaaaa.

 Haya tena, kishapendeza mtoto wa kike asubiriwa somo hapa mambo yaanze. Ha ha ha ha ha ha! Tembea ulishe macho yako wewe! Kila siku kumshangaa Chokoraa, ohoo! mara Chokoraa ana maneno mengi! Si nimeona mengi!!!? Simo humu miye.

Somooooooooo!!!! Yuko wapi somoye harusi jamani aje hapa tuhangaike naye, nasema aje hapaa, nasema aje hapaa, nasema aje hapaaa!!!!!!!! Nahusika humu kwani miye!? Simo.



Haya, kwa leo nakomea hapa. Ni mimi ndugu yenu Chokoraa wa Muhangaikaji wa Mlalahoi wa Pangupakavu wa Kabwela wa Mdanganyika, nawasiliamia.

Saturday, July 14, 2012

Chokoraa na 'Fotoa Foto'

Hapa ni "Ng'wanza" wenyewe mwaita 'Mwanza'. Tumekuja kushuhudia mchakato wa BSS chini ya udhamini wa Zantel.
Ha ha ha ha ha ha!!! Ati wajiuliza namaanisha nini? Kwani mbona wewe hutambai tena siku hizi!? Ndiyo, nasema na Chokoraa anakua na kuongezeka na hizo ni baraka za jalali na kama unabisha basi kwenye huo ubishi mi simo tena simo kabisa. Ala!. Haya basi, kuanzia sasa naanza kuwaletea picha kadha wa kadha ambazo Chokoraa wa Kabwela amekutana nazo kwenye kuchakulachakula majalalani huku na huko, walau kila mwisho wa Wiki.

Wiki hii, meli maarufu kwa kusaifirisha mizigo toka Bandari Salama hadi kisiwa cha Mafia iliteketea kwa moto baada ya mmoja wa wafanyakazi wake kujaribu kuwasha jenereta ili ku-pump nje shehena ya mafuta ya Tanesco yaliyokuwa ndani ya meli hiyo.

Wananchi wakishuhudia meli hiyo ikiteketea kwa moto. Wananchi wamekitupia lawama kikosi cha Zimamoto wilayani Mafia kwa kushindwa kuonyesha makeke yoyote kwenye tukio hilo. Hata hivyo, shehena ya mafuta iliyokuwemo kwenye meli hiyo iliokolewa yote ilhali kiasi cha pikipiki mbili, na gari moja vilivyokuwa mali ya watu binafsi vinaripotiwa kuteketea kabisa. Hili ni tukio la pili kwa meli iliyobeba shehena ya mafuta ya Tanesco kupata mushkeli ambapo miaka kadhaa meli nyingine ikiwa na shehena ya mafuta ya Tanesco ilizama baharini ikitokea Dare salaam kwenda kisiwani Mafia.


Wednesday, June 27, 2012

Rafiki yangu kipenzi Udadisi Chautundu - 2

Najua! Naam, bado nakumbuka ahadi niliyokuahidi kwamba nitakueleza zaidi kuhusu yule jamaa maarufu wa harufu hapa mjini kwa jina la Maisha Magumu, lakini ngoja kwanza nimalizie kila kisa cha Chokoraa wa Muhaingaikaji wa Mlalaohi wa Pangupakavu wa Kabwela wa Mdanganyika kufikishwa kwenye kituo kikuu cha walinzi wa ‘muishi miwa’ saaaaana Dola.

 Bila shaka unakumbuka nilipokomea kwenye kukuhadithia tukio zima na jinsi ambavyo nilitandikwa kibuti cha mgongo na kuishia kunyamaza kimya ili kuokoa uhai wangu, lakini nakuapia ndugu yangu bado nigali na hasira kwa kitendo kile japo kadhia nzima imepita sasa. Aala! Yaani kufikishwa tu kituoni tena si mahala pa usalama bali kashfa matusi na vipigo? Naapa humu miye simo. Ati kila anayefikishwa kwenye “sentro” basi ni mhalifu hata kama hajaonana na pilato na hawa walinzi wanaanza kumpa majina kwa kadri watakavyo mara wakuite Mhalifu wa Mkosaji, mara wakuite Kibaka wa Mwizi, mara Jambazi wa Sugu na mengine mengi, naapa kwenye yote hayo hakuna hata jina langu.

 Nilitamani nikuite ndugu yangu Udadisi ili uwaambie hawa jamaa kwamba mimi naitwa Chokoraa wa Mdanganyika lakini nikahofia kukuingiza na wewe kwenye msambwe na kadhia ya kupachikwa majina ya ajabu ajabu huku ukitandikwa kwa kadri watakavyo wanaotaka katika kutaka kwao na humu simo. Basi ndugu yangu, baada ya kuulizwa maswali kadha wa kadha ya kuudhi nikasukumizwa ‘lokapu’ bila hata kujua kosa langu na kama nilivyokuahadithia hapo awali, nikaamua kukaa kimya kwa vile nilijua tu kwamba kesho yake wababe hawa wangenipeleka tu kwa pilato na huko ningesema bila hofu wala mashaka kwa sababu huko hawaruhusiwi kunifanyia ubabe wao huu.

Yaliyonikuta humo ndani hata sitaku kukuhadithia ndugu yangu Udadizi na nakuonya kwa sababu ya jina lako usije ukajaribu kuingia huko kwa ajiri ya kujua kunani maana naapa hakufai. Kesho ilifika hata hivyo, asubuhi na mapema nikaamshwa na kukabidhia tena “kobazi” zangu niziitazo viatu na sehemu ya vikaratasi vyangu vilivyokuwa mfukoni na ambavyo nilinyang’anywa wakati nikitiwa ‘lokapu’, noti yangu ya shekeli kadha wa kadhaa iliyokuwa mpya niliikuta imebadilishwa na moja iliyokuwa chakavu karibu na kuchanika, lakini walau kuzeeka kwa noti hakuondoa thamani ya fedha humu namo simo, nikaitia mfukoni na kupakiwa kwenye gari na watu wengine niliowakuta ‘lokapu’ jana yake.

Kilichonishangaza hadi nakaribia kuanguka na kuzimia si kufika kwa pilato na kugundua jinsi ambavyo wababe hawa wa muishi miwa sana Dola walivyogeuka kuwa wapole na waungwana ghafla, hapana, hilo nililitaraji lakini nilishangazwa na mashtaka niliyosomewa mbele ya Pilato wa Mwamuzi. Nakwambia ilikuwa kama mchezo wa kuigiza, mshitaki akajipanga vizuri na kurekebisha ‘ulimi wa mbwa’ shingoni mwake na kisha akajikohoza kidogo kuweka sauti sawa, kisha kwa sauti yenye mikwaruzo kidogo, na nadhani mikwaruzo hii ni kwa sababu ya kunywa sana mvinyo ila humo namo simo, akasema; “Chokoraa wa Mdanganyika, unashitakiwa mbele ya ‘kilinge’ hiki cha ‘muheshimiwa’ Pilato kwa kosa la Uzembe na Uzururaji, kwamba siku ya juzi mnamo saa tatu na dakika kidogo za usiku ulikutwa ukitenda kosa la Uzembe na Uzururaji kwenye mitaa ya kaya yetu hii kinyume na kifungu cha sheria…..” sikupata hata nafasi ya kumsikiliza hili amalize nikaamua kumkatisha’

 “...Kwanza mimi Jina langu halisi ni Profesa Chokoraa wa Muhangaikaji wa Mlalahoi wa Pangupakavu wa Kabwela wa Mdanganyika, halafu umenishitaki kwenye ‘kilinge’ hiki kwa makosa ya wadogo zangu wawili yaani Kulwa na Doto maana wamezaliwa mapacha kwa mama yetu Shida wa Matatizo na ndiye aliyemwita Kulwa Uzembe na Doto akamwita Uzururaji, na hivyo nafikiri ama ukawatafute waje wajibu makosa yao ama unipe mimi muda nitawaleta hata nyumbani kwako ukitaka”.

Nakwambia “kilinge” chote kilikaa kimya kwa muda maana nilizungumza kwa jazba na kujihamini sana. Aala! Yaani kwanza ati nashitakiwa kwa makosa ya watu wengine! Huu sasa si uonevu? Yaani Uzembe na Uzururaji wafanye makosa halafu nishitakiwe mimi Chokoraa kwa lipi hasa!? Halafu hayo makosa yenyewe waliyoyafanya mimi hata siyafahamu, nitajibuje sasa kuhusu makosa yao ambayo hata sikuwapo wakati wakiyatenda kama kweli waliyatenda na siyafahamu? Naapa huu sasa ni uonevu. Namshukuru mwenyezi kwamba Pilato naye ni mtoto wa Muungwana na bila shaka unakumbuka jinsi yule mzee naye alivyowalea watoto wake na kuwafunza kuwa na huruma na kutenda haki, baada ya kusikiliza maneno yoote ya mlalamikaji, akalifutilia mbali shitaka lenyewe kwa vile ati aliliona halina msingi. Mimi nasema halikuwa hata na ngazi, madiirisha, milango wala paa.

 Basi bwana, nikaondoka mahakamani na kujaribu kupita dukani mgahawani ili walau nijipatie chochote kitu kwa ajiri ya kula maana njaa ilikuwa ikiniuma, lakini kutahamaki hata ile noti yangu mbovumbovu ilishakwapuliwa haikuwamo mfukoni. Nikaona sina jinsi, nikaamua kujikongoja kidogo kidogo hadi kwa yule rafiki yake na marehemu baba yetu mzee Mkulima ili walau nipate embe nitulize njaa wakati nikiangalia uelekeo na ndipo nikapitia posta na kukuta barua yako.

 Bila shaka sasa umefahamu chanzo cha ugomvi kati yangu na wadogo zangu hawa wawili Uzembe na Uzururaji. Nitakapokuandikia tena nitakueleza ni kwa nini nimekasirikia zaidi Uzembe uliko uzururaji ile kwa sasa nahitaji kwenda hospitali kumtazama mtoto wa Uzembe yule mdogo aitwaye Ulalamishi maana nasikia ni mgonjwa, damu nzito kuliko maji nakwambia.

Ati! Hujui kama Uzembe ana mtoto? Kweli wewe sasa unazeeka vibaya rafiki yangu. Haya nitakuhadithia yahusuyo huyo mtoto kwenye waraka wangu utakaofuata ila kwa sasa nikusalimie tu.

Wasalaamu, nduguyo Chokoraa wa Muhangaikaji wa Mlalahoi wa Pangupakavu wa Kabwela wa Mdanganyika, nakusalimia.

Saturday, June 9, 2012

 Rafiki yangu kipenzi Udadisi Chautundu


Nimepata barua yako rafiki yangu kipenzi tuliyekua pamoja na kucheza pamoja “kidaso” yaani naona hata aibu kukuita rafiki maana wewe ni ndugu yangu. Umenilaumu kweli kwenye barua yako kwamba ndugu yako nimekusahau na hata jina lako huna hakika kama ningali nikilikumbuka, lakini nakuhakikishia hata ningeamshwa usingizini ghafla na kutakiwa nimtaje rafiki yangu wa karibu, ningekutaja wewe kwanza kaka yangu Udadisi Chautundu. Hata hivyo ni siku nyingi kweli tangu tulipoonana na nimegundua baada ya kusoma barua yako, kwamba kuna mambo mengi uliyoyasahau kuhusu mimi na kuna mengi pia yametokea ambayo hujayajua na inawezekana kama ungekuja mjini kunitafuta basi bila shaka ungenikosa.

 Nakupongeza hata hivyo ulivyoamua kubaki kijijini. Ndiyo, nakupongeza kwa sababu huku mjini kuna watu wana roho mbaya sana kiasi ningekuwa sina tetesi kuhusu wazazi wao, basi nisingesita kukwambia hawa si binadamu na hawakuzaliwa lakini kwa bahati kuna tetesi nyingi kuhusu wazazi wao. Kuna huyu Maisha Magumu. Huyu jamaa unapoingia tu mjini ndiye wa kwanza unayekutana naye na nakwambia huyu jamaa ni maarufu humu mjini kuliko hata ‘mkulu wa kaya’ yetu na kila siku umaarufu wake unaongezeka.

Ha ha ha ha!! Unaona sasa, umeanza kumfananisha huyu jamaa na yule mzee pale kijijini ambaye wewe rafikiri yangu Udadisi ulinifanya kila siku nifikirie maana ya jina lake bila majibu mpaka nilipokuja huku mjini. Si yule mzee alikuwa na koti lefu jeusi na kofia ambayo japo hatukujua aliifua saa ngapi lakini haikuwa ikionekana chafu kila alipoivaa!! Usijifanye umemsahau bwana, mzee Malingumu wa Maliyatabu.

Huyu maisha magumu wala hana uhusiano na hao wawili. Yeye huyu hajulikani vizuri hasa nasaba yake maana wako wanaosema anatoka kwenye ukoo wa yule mzee mwenye kitambi mheshimiwa Kiongozi Mrafi na eti ni mtoto wa mke mkubwa wa huyu mzee Bi Rushwa wa Mlungula.

 Wangine wanasema hapana, Mheshimiwa Kiongozi Mrafi anasaidia tu kumlea huyu mtoto kwa sababu wakati anamuoa mke wake Bi Rishwa wa Mlungula, Bi Rushwa alikuja na huyu mtoto kutoka kwenye ndoa yake ya kwanza kwa yule mzee kiburi sana hapa mjini Bw. Ubadhirifu wa Maliyauma. Vyovyote iwavyo, huyu jamaa amejifunza vyema kwa mama yake maana tabia zake mnh! Nitakueleza siku nyingine, leo nataka tu kujibu barua yako.

 Kwanza nikuhakikishie kwamba sijakusahau ndugu yangu na unapoona sikuandikii hata barua, ni kwa sababu ndugu yako siku hizi naishi kwenye kitongoji kimoja hapa mjini ambacho ni maarufu kwa kuwa na shughuli nyingi wenyewe wanaita “bize”. Basi mwenzako nashinda bize tangu asubihi hadi jioni na kila uzingizi ukinizidia ‘naangusha gari’ hapo hapo ninapokuwa na nikaimka naendeleza libeneke. Lakini pia yule mdogo wangu Uzembe naye anachangia hii hali ya mimi kutokukuandikia barua, lakini usijari kwa sababu sasa hivi mimi na uzembe tuna ugomvi tena mkubwa, basi nadhani kwa muda mrefu kidogo ataniacha peke yangu na hivyo nitapata nafasi ya kukuandikia kila mara.

 Unashangaa tuna ugmvo gani!!? Si ndo hayo sasa ninayokwambia ndugu yangu kwamba siku hizi kuna mambo mengi yamenitokea na wewe huyajui!! Hata! Wala sikulaumu. Najua unanipenda sana na ungependa kujua kila kinachonipata swahiba wako Chokoraa wa Muhangaikaji, lakini mara nyingine huwa nalazimika kukuficha mengine maana najua yatakuumiza hasa kwa vile wewe ulivyo Mdadisi kama jina lako, najua utaumia sana moyo ndiyo maana huwa mengine namezea.

 Haya basi, kwa vile umelazimisha, wacha nikwambia tuna ugomvi gani na Uzembe halafu hayo mengine nitakuandikia waraka ujao. Ilikuwa usiku kamaa saa tatu na nusu hivi na tulikuwa watatu tunatokea kwenye soko la “bize” kurejea ‘gheto’ kwa ajiri ya kupumzisha mbavu zetu. Basi bwana, mara ghafla tukakutana na watumishi wa ‘siri kali’ wenye jukumu la kulinda amani. Mimi soga zilikuwa zimenikolea mwenyewe hata sikuwaona hadi walipokuwa wameshatufikia karibu, kutahamaki, Uzembe na Uzururaji wakatimua mbio na kuniwacha peke yangu. Kwanza sikufahamu kwa nini walikimbia, lakini kama unijuavyo ndugu yako Chokoraa huwa sina hofu na walinzi wa mheshimiwa Dola.

 Nikasimama kwa ujasiri kabisa tena kwa kujiamini si ninajua sina matatizo mimi na mwenyekiti wetu Mheshimiwa Dola! Wapi!! Nakwambia yaani hawa walinzi hata kabla hatujasilimiana nikasikia mmoja ambaye nadhani alikuwa kubwa wao akisema kwa sauti ya ukali na ya kushutumu “Hivi hili si ndiyo linaitwa Chokoraa litoto na yule mzee marehemu Mhangaikaji?”. Akajibiwa “Ndiyo” hata sikujua ni nani aliyejibu maana tayari alishaanza kunitandika makofi huku akinipa amri mfululizo “kaa chini kachini…mikono juu.. una nini mfukoni we Chokoraaa?... huna majani mfukoni kweli wewe….?”.

Sikujua hata nijibu swali lipi kwanza na sikujua hata kosa langu, mara nikawasikia wakizungumza maneno fulani kwenye vilongalonga vyao na lugha yenyewe hata sikuifahamu ila nahisi kitakuwa ni kigagagigikoko maana sikuambulia hata sentensi moja, mara gari hilo likaja limejisheheneza walinzi wengine na hata mmoja wao akiwa amebeba ‘manati ya ndhungu’. Niliogopa nilipoiona hiyo manati wewe!!! Asikudanganye mtu ndugu yangu, manati ya ndhungu inatisha ikiwa kwenye mikono ya watu wenye hasira kama hawa walinzi wa dola. Basi bwana, nikapakiwa kwenye gari tena kwa kusukumizwa kama mzigo hadi kwenye kituo kikuu cha hawa walinzi, hapa napo nikapokelewa na maneno kadhaa ya kejeli “Mmelitoa wapi hili Chokoraa!!?” mmoja wao akauliza huku akinikwida na kunizungusha nyuma ya meza kuuubwa ajabu! Mwingine akadakia, “kwani ni Chokoraa au Jambazi kabisa hili?”.

Ala! Sasa hasira zangu zikanipanda na povu likaanza kunitoka mdomoni. Yaani wananifananisha na yule adui yangu mkubwa ambaye ndiye aliyemuua baba yangu marehemu Muhangaikaji? Nimekuwa nikimtafuta huyu jamaa na hata walinzi wa Dola waliniahidi kwamba wangemtia mbaroni sasa ni mwaka sijui wa ngapi hajapatikana na nasikia anaishi mjini humu humu tena rafiki zake wengine wanajulikana na ati ndiyo sababu ameshindikana kukamatika, leo hawa wananifananisha naye! Haiwezekani.

Nikafumbua kinywa hivyo hivyo na mapovu mdomoni. “Mimi siyo jambazi, mimi ni Chokoraa wa Muhangaikaji. Hata mimi namtafuta huyu Jambazi kwa sababu alimuua baba yangu miaka kadhaa iliyopita…” hata sikumaliza, sori ya kiatu ikatua mgongoni na kunituliza chini, nikaona ili kuokoa uhai wangu bora nikae kimya hadi nitakapofika kuonana na liwali kesho maana hawa jamaa hata hawatakki kunisikiliza. Itaendelea